Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KUHUBIRI NA KUFUNDISHA DUNIANI KOTE

Ulaya

Ulaya
  • IDADI YA NCHI 47

  • IDADI YA WATU 741,892,871

  • IDADI YA WAHUBIRI 1,601,915

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 862,555

“Je, Umekosea Mahali Ulipokuwa Ukienda?”

Mwanamke fulani Msomali nchini Sweden alialikwa ahudhurie mkutano kwenye Jumba la Ufalme, naye akaamua kwenda. Hata hivyo mambo hayakwenda vizuri. Hakuna aliyemkaribisha; watu wote walikuwa wakimtazama tu. Alijihisi vibaya sana. Mtu fulani ambaye huenda aligundua kwamba mwanamke huyo alikuwa na wasiwasi,  alimwuliza hivi, “Je, umekosea mahali ulipokuwa ukienda?”

“Ndiyo, nafikiri nimekosea!” akamjibu. Halafu akaondoka. Baadaye, mwanamke huyo alipokutana na Mashahidi waliomwalika, alikuwa amevunjika sana moyo na kuwaambia kwamba hangerudi tena. Walijiuliza ni nini kilichokuwa kimetukia, kwani hawakumwona kwenye Jumba la Ufalme. Baada ya mazungumzo mafupi, walitambua kwamba alikuwa ameenda katika kanisa fulani pasipo kujua!

Mashahidi hao walimtia tena moyo aende kwenye Jumba la Ufalme. Alikubali, lakini akasema kwamba  hangekaa zaidi ya dakika 10 ikiwa hangejihisi huru. Hata hivyo, alipoingia katika Jumba la Ufalme, kila mtu kutanikoni alimkaribisha kwa uchangamfu! Alifurahia sana kuwa kwenye Jumba la Ufalme hivi kwamba alikuwa wa mwisho kuondoka baada ya mikutano. Tangu wakati huo, amekuwa akihudhuria mikutano kwa ukawaida, na sasa yeye ni mhubiri ambaye amebatizwa.

Aliokota Mwaliko Barabarani

Ugiriki: Sasa Stergios anawaambia watu wengine kweli aliyopata

Stergios ni kijana anayeishi nchini Ugiriki. Asubuhi moja alipokuwa akirudi kutoka kazini, aliamua kupita barabara tofauti na ile aliyokuwa akipita kila siku. Alipokuwa akitembea aliona kitu fulani chini. Ulikuwa ni mwaliko wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Ulikuwa na swali: “Unamwonaje Yesu?” Kwa kuwa kulikuwa na watu karibu, Stergios alisita kuokota mwaliko huo. Alipofika nyumbani, alianza kufikiria swali hilo na alitamani kujua zaidi.

Stergios alikuwa amepanga kwenda kwenye mkahawa na baadhi ya rafiki zake alasiri hiyo. Alipokuwa akienda kukutana nao, aliamua kupita njia ambayo alikuwa ameuona mwaliko huo, akitumaini kwamba ataupata. Aliuona, lakini bado kulikuwa na watu, hivyo akasita tena kuuokota. Alipokuwa akirudi nyumbani baada ya kufurahia na rafiki zake, Stergios alipita njia ileile, na mwaliko ule bado ulikuwepo barabarani. Wakati huu, aliuokota na kuusoma. Baada ya kusoma, aliamua kuhudhuria Ukumbusho.

Baada ya Ukumbusho, Stergios alikubali kufundishwa Biblia bila malipo. Alianza kuhudhuria mikutano na kufanya maendeleo ya kiroho. Alibatizwa kwenye kusanyiko la pekee Machi 2013.

 Kipindi cha Redio Chamsaidia Kuacha Chuki

Mnamo Januari 2010, Finn, ndugu kutoka Copenhagen, Denmark, alienda matembezi na kuamua kuchukua baadhi ya magazeti yetu. Alipokuwa akitembea kwenye barabara fulani nyembamba, alimwona mwanaume mzee akija mbele yake. Finn alimpa gazeti la Desemba 2009, lililokuwa na makala kadhaa kuhusu Krismasi. Mzee huyo alipomshukuru, Finn alitambua sauti yake. Alikuwa msomi na mtayarishaji wa kipindi cha mahojiano redioni. Siku iliyofuata, Finn alisikiliza kipindi chake na alishangaa kumsikia mtangazaji huyo akieleza kwamba alikubali magazeti yetu. Kisha akasoma redioni sehemu za makala fulani. Mojawapo ya mambo aliyosoma ni kuhusu ile “nyota” iliyoonekana baada ya Yesu kuzaliwa. Akakiri kwamba lazima iwe ilitumwa na Shetani.

Alipoona kuwa mtangazaji huyo amependezwa sana na magazeti yetu, Finn aliamua kumtembelea. Katika mazungumzo yao, Finn alimwomba ikiwa ingewezekana kuwa na kipindi cha mazungumzo ya Biblia. Majuma mawili baadaye alijibiwa. Zaidi ya vipindi 30, kila kimoja kikiwa na urefu wa saa mbili, vilivyohusu Mashahidi wa Yehova na Biblia vilirushwa hewani. Mtangazaji huyo na Finn walizungumzia habari mbalimbali na wakajibu maswali mengi sana yaliyoulizwa na wasikilizaji waliopiga simu.

Msikilizaji mmoja alimpigia simu fundi wa mitambo wa kituo hicho cha redio na kumpa namba yake ya simu. Alitaka kuwasiliana na akina ndugu. Mipango ya kuwasiliana naye ilifanywa haraka sana. Kwa miaka mingi mtu huyo alikuwa amesikia porojo kuhusu Mashahidi wa Yehova kutoka kwa marafiki na watu wa familia  yake, lakini kwa sababu ya yale aliyosikia redioni aliacha kuwachukia Mashahidi. Funzo la Biblia lilianzishwa, na mwaka wa 2013 alihudhuria Ukumbusho na hotuba ya pekee. Anahudhuria mikutano yote ya Jumapili na kutoa maelezo mazuri kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Watu wengine pia katika eneo hilo wameitikia vizuri kweli za Biblia kwa sababu ya mambo waliyosikia kwenye vipindi hivyo vya redio.

Aliacha Mwaliko Mlangoni

Ilikuwa siku ya mwisho ya kusanyiko la wilaya nchini Italia. Lucio alipokuwa akiagana na rafiki zake, wenzi fulani wa ndoa waliwakaribia. Lucio akawauliza, “Mnashirikiana na kutaniko gani?” Wakajibu, “Hatushirikiani na kutaniko lolote.”

“Je, kuna mtu fulani aliyewaalika?” Lucio akawauliza.

“Hapana, tulikuja sisi wenyewe,” wakajibu.

Lucio alitaka kujua zaidi, hivyo akawauliza, “Ni nini kilichowachochea mhudhurie?”

Wakasema, “Tulipata mwaliko mlangoni, na tukaamua kuja.”

Walipomwambia Lucio mahali wanapoishi, mke wake, Ester, alisema hivi kwa msisimko: “Ni mimi niliyeacha mwaliko huo! Ilikuwa siku ya mwisho ya kugawa mialiko, kwa hiyo niliona afadhali niache milangoni mialiko iliyobaki badala ya kuitupa.” Walipopata mwaliko huo wenzi hao waliamua kusafiri hadi kwenye Jumba la Kusanyiko ili kuhudhuria programu siku ya Jumapili. Baada ya mazungumzo mafupi, Lucio na Ester waliwaalika wenzi hao nyumbani kwa ajili ya mlo, na wakaendelea na mazungumzo. Wenzi hao walikubali funzo la Biblia. Siku zote wanajiandaa vizuri kwa ajili ya funzo lao na sasa wanahudhuria mikutano na kutoa maelezo.