Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

1915-1947 Siku za Mapema (Sehemu ya 1)

1915-1947 Siku za Mapema (Sehemu ya 1)

 Nuru ya Kweli Yaanza Kung’aa

Habari njema iliwasili nchini Sierra Leone mwaka 1915 wakazi wa Sierra Leone waliporudi kutoka Uingereza wakiwa na machapisho yanayozungumzia Biblia. Karibu Julai mwaka huo, mtumishi wa kwanza wa Yehova aliyebatizwa aliwasili jijini Freetown. Aliitwa Alfred Joseph. Alikuwa na umri wa miaka 31, na alikuwa mwenyeji wa nchi ya Guyana, Amerika Kusini. Alikuwa amebatizwa mapema mwaka huo katika kisiwa cha Barbados, West Indies, na alikuwa amesaini mkataba wa kuendesha gari moshi jijini Freetown. Alfred aliishi kwenye nyumba za shirika la reli mjini Cline Town, umbali wa kilometa tatu hivi kutoka mahali ulipo ule Mti wa Msufi jijini Freetown. Bila kukawia alianza kuzungumza na wafanyakazi wenzake kuhusu ujumbe wa Biblia.

Mwaka uliofuata, Alfred aliungana tena na mtu aliyefanya naye kazi hapo awali katika kisiwa cha Barbados, Leonard Black­man. Mama yake Leonard, Elvira Hewitt, ndiye aliyemhubiria Alfred. Leonard akawa jirani ya Alfred, nao walikutana kwa ukawaida ili kuzungumzia Biblia. Pia, waliwapatia rafiki zao na watu wengine waliopendezwa machapisho yanayozungumzia Biblia.

Alfred na Leonard waligundua kwamba mashamba ya Freetown yalikuwa “meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35) Mnamo 1923, Alfred alituma barua makao makuu jijini New York, akisema: “Watu wengi hapa wanapendezwa na ujumbe wa Biblia. Je, mnaweza kumtuma mtu fulani aje awafundishe na kusaidia kuendeleza kazi ya kuhubiri nchini Sierra Leone?”Alijibiwa hivi: “Tutamtuma mtu fulani!”

William “Bible” Brown na mke wake, Antonia

 “Jumamosi moja usiku, miezi kadhaa baadaye, nilipigiwa simu ambayo sikuitarajia,” Alfred anaeleza.

“‘Je, wewe ndiye uliyetuma barua kwa Watch Tower Society ukiwaomba watume wahubiri?’ Mtu aliyepiga simu akauliza.

“‘Ndiyo,’ nikajibu.

“‘Vizuri sana, wamenituma mimi,’ sauti hiyo ikaunguruma.

“Ilikuwa sauti ya William R. Brown. Yeye na mke wake, Antonia, na binti yao mdogo walikuwa wamewasili siku hiyo na kufikia kwenye Hoteli ya Gainford.

“Asubuhi iliyofuata, mimi na Leonard tulipokuwa katika funzo letu la Biblia la kila juma, mwanaume fulani mwenye mwili mkubwa akasimama mlangoni. Mtu huyo alikuwa William R. Brown. Aliipenda sana kweli hivi kwamba alitaka kutoa hotuba ya watu wote siku iliyofuata. Bila kuchelewa tulikodi ukumbi mkubwa zaidi jijini Freetown—Wilberforce Memorial Hall—kisha, tukapanga ratiba ya hotuba nne, ya kwanza ikitolewa jioni ya Alhamisi iliyofuata.

“Kikundi chetu kidogo kilikuwa na kazi nyingi sana ya kutangaza hotuba hizo kwenye gazeti, vipeperushi, na kuwajulisha watu ana kwa ana. Hatukujua jinsi ambavyo wakazi wa eneo hilo wangeitikia, lakini hatukuwa na sababu ya kuwa na wasiwasi. Karibu watu 500 walijaa kwenye ukumbi huo, kutia ndani viongozi wengi wa dini jijini Freetown. Tulikuwa na shangwe sana!”

Katika hotuba hiyo ya saa moja, Ndugu Brown alinukuu mara nyingi sana Maandiko na kutumia projekta ili kuonyesha maandiko hayo ya Biblia kwenye sinema. Katika mazungumzo yake yote alikuwa akirudia maneno haya tena na tena, “Si Brown anayesema bali Biblia ndiyo inayosema.” Wasikilizaji walistaajabu sana, na walipiga makofi kila baada ya jambo kuu kutajwa. Kilichowavutia watu, si ufasaha wa kuzungumza wa Ndugu Brown, bali hoja zake zenye nguvu zilizothibitishwa kwa kutumia Maandiko. Kijana fulani miongoni mwa wasikilizaji aliyekuwa akisomea ukasisi alitamka hivi: “Bw. Brown anaijua Biblia yake!”

Hotuba za Ndugu Brown ziliwachochea watu jijini hivi kwamba walikusanyika ili kuzisikiliza. Jumapili iliyofuata, watu wengi walijaa tena ukumbini ili kusikiliza hotuba yenye kichwa “Kwenda Helo na Kurudi—Nani Walio Humo?” Kweli zenye nguvu ambazo Ndugu Brown alizungumzia usiku huo ziliwachochea watu, kutia ndani wale waliokuwa na bidii ya kwenda kanisani hivi kwamba wakajiuzulu.

Hotuba ya nne na ya mwisho katika mfululizo wa hotuba hizo ilikuwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” ilihudhuriwa na umati mkubwa wa watu hivi kwamba muda fulani baadaye mkazi mmoja wa Freetown alieleza hivi: “Makanisa yalilazimika kuahirisha ibada za jioni kwa sababu waumini wote walienda kusikia hotuba ya Ndugu Brown.”

Kwa sababu Ndugu Brown alikuwa na kawaida ya kuitumia Biblia ili kuthibitisha mambo aliyosema, watu walianza kumuita “Bible” Brown. Jina hilo la utani lilizoeleka sana hivi kwamba likafahamika kotekote Afrika Magharibi. Hadi alipomaliza mwendo wake duniani, William R. Brown alifurahia sana kuitwa kwa jina hilo la utani.

1924