Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIERRA LEONE NA GUINEA

1991-2001 ‘Tanuru ya Mateso’—Isa.48:10 (Sehemu ya 1)

1991-2001 ‘Tanuru ya Mateso’—Isa.48:10 (Sehemu ya 1)

 Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe

Matatizo ya kijamii, kisiasa, na ya kiuchumi yaliyotokea miaka ya 1980, yalisababisha machafuko katika nchi nyingi za Afrika Magharibi. Vita vilipotokea katika nchi ya Liberia, watu wengi walikimbilia nchini Sierra Leone. Ofisi ya tawi iliandaa nyumba na Majumba ya Ufalme ili kuwahifadhi wakimbizi ambao ni Mashahidi, na akina ndugu wakawapa ndugu zao vitu walivyohitaji.

Ingawa nyakati hizo zilikuwa ngumu sana kwa wakimbizi, kulikuwa na pindi za kuchekesha. Isolde Lorenz, mmishonari ambaye ametumikia kwa muda mrefu anasema hivi: “Mvulana mmoja alitumwa na baba yake akapashe moto chakula kwenye jiko lililokuwa bustanini katika eneo lililo nyuma ya Jumba la Ufalme (jumba hilo lilikuwa sehemu ya majengo ya ofisi ya tawi). Mvulana huyo aliporudi, alimwambia baba yake kwamba hakungekuwa na chakula siku hiyo. Baba yake akamuuliza, kwa nini? Mvulana huyo akasema, ‘Kwa sababu leo, Yehova amenikomboa kutoka katika mdomo wa simba! ’ Ni nini kilichotokea? Alipokuwa akirudi na chakula, mvulana huyo alikutana na mbwa wa ofisi ya tawi aliyeitwa Lobo, wa jamii ya German shepherd, ambaye alikuwa mkubwa lakini hakuwa mkali. Mvulana huyo aliogopa sana. Akiwa ameshika sahani ya chakula, mvulana huyo alijitahidi kadiri alivyoweza kuunyoosha mkono mbali ili mbwa asile chakula hicho. Hata hivyo, Lobo, aliona hiyo kuwa ishara ya kukaribishwa ale chakula hicho. Na hivyo ndivyo Lobo alivyofanya!”

Mnamo Machi 23, 1991, mapigano yaliyokuwa yakiendelea nchini Liberia yaliingia nchini Sierra Leone, na kuanzisha vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miaka 11. Kikundi cha waasi kilichotwa Revolutionary United Front (RUF) kilisonga mbele kwa kasi hadi kwenye mji wa ­Kailahun na Koindu, na kufanya wenyeji wengi wakimbilie nchini Guinea. Kati ya wakimbizi hao kulikuwa na ndugu na da­da 120 hivi. Wakati huohuo, Mashahidi wengine kutoka Liberia walikimbilia mapema nchini Sierra Leone na hivyo kuwatangulia waasi.

Billie Cowan, ambaye alikuwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi wakati huo anasema hivi: “Kwa miezi kadhaa, makundi ya akina ndugu yaliwasili Betheli ya Freetown wakiwa wamechoka, wamedhoofika, na wenye njaa. Wengi walikuwa wameshuhudia ukatili wenye kuogopesha sana na waliponyoka kufa kwa njaa kwa kula mimea ya porini. Bila kukawia tuliwapa chakula na nguo na tuliwatunza ndugu zao wa ukoo na watu waliokuwa wakipendezwa ambao waliandamana nao. Ndugu na dada wenyeji waliwatendea kwa fadhili na kuwakaribisha ndugu zao wakimbizi kwenye nyumba zao. Mara moja Mashahidi hao wakimbizi wakawa na shughuli nyingi katika huduma ya shambani, wakiyasaidia makutaniko ya wenyeji. Baada ya muda, wengi wao waliondoka, lakini walipokuwa hapa, walituimarisha sana!”

Vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Sierra Leone vilipiganwa kwa miaka 11

Kutoa Faraja na Tumaini

Ofisi ya tawi iliwatumia chakula, dawa, vifaa vya ujenzi, na vyombo Mashahidi waliokuwa katika kambi zilizokuwa kusini mwa Guinea. Msaada huo ulitia ndani nguo nyingi zilizotoka Ufaransa. Baba mmoja aliandika, “Watoto wangu walicheza, wakaimba, na kumsifu Yehova. Walikuwa wamepata nguo mpya za kuvaa kwenye mikutano!” Baadhi ya ndugu na dada walisema kwamba hawajawahi kuwa na nguo nzuri kama hizo!

Hata hivyo, wakimbizi walihitaji mengi zaidi ya msaada wa kimwili tu. Yesu alisema hivi: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Hivyo, ofisi ya tawi ilituma machapisho yanayotegemea Biblia katika eneo hilo na kuandaa makusanyiko kwa ukawaida. Pia, mapainia na waangalizi wanaosafiri walitumwa katika eneo hilo.

Mwangalizi wa mzunguko André Baart alipotembelea mji wa Koundou, nchini Guinea, alikutana na ofisa mmoja wa kambi ambaye alimwomba awatolee wakimbizi hotuba inayotegemea Biblia. Karibu watu 50 walimsikiliza André akitoa hotuba yenye kichwa ‘Mkimbilie Yehova,’ iliyotegemea Zaburi ya 18. Alipomaliza, mwanamke mmoja mzee alisimama na kusema hivi: “Umetufurahisha sana. Mchele hautatui matatizo yetu, lakini Biblia inatuonyesha jinsi tunavyoweza kumtegemea Mungu. Tunakushukuru sana kwa kutufariji na kutupatia tumaini.”

Wamishonari William na Claudia Slaughter walipopewa mgawo katika mji wa Guékédou, nchini Guinea, kutaniko lililokuwa na zaidi ya wakimbizi 100 liliwaka roho. (Rom. 12:11) William anasema hivi: “Vijana wengi wadogo walikuwa wakijitahidi kukua kiroho. Ikiwa mtu aliyegawiwa hotuba kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi hangekuwepo, ndugu vijana wapatao 10 hadi 15 wangejitolea kutoa hotuba hiyo. Makundi makubwa ya wahubiri yangetoka na kuhubiri kwa bidii. Baadaye, baadhi ya vijana hao wenye bidii wakaja kuwa mapainia wa pekee na waangalizi wanaosafiri.”

Ujenzi Wakati wa Machafuko

Muda mfupi baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe kuanza, akina ndugu jijini Freetown walinunua kiwanja chenye ukubwa wa ekari moja na nusu kwenye Barabara ya 133 ya Wilkinson, mita kadhaa kutoka mahali ilipo ofisi ya tawi. Alfred Gunn anasema, “Tulitaka kujenga Betheli mpya mahali hapo hata hivyo tulihangaishwa na vita. Kwa kuwa Lloyd Barry wa Baraza Linaloongoza alikuwa akitutembelea wakati huo, tulimweleza hangaiko letu. Ndugu Barry alitueleza hivi: ‘Ikiwa tutairuhusu vita ituzuie, hatutafanikisha jambo lolote!’ Maneno yake yenye kutia moyo yakatupa ujasiri wa kuendelea na mradi huo.”

Kulikuwa na mamia ya ndugu katika mradi huo, kutia ndani wajitoleaji zaidi ya 50 kutoka nchi 12, na wajitoleaji wengine wengi kutoka kwenye makutaniko mbalimbali nchini. Kazi ilianza Mei 1991. Msimamizi wa ujenzi huo, Tom Ball anasema, “wapita njia walivutiwa sana na ubora wa matofali yaliyokuwa yakifyatuliwa katika eneo la ujenzi. Vyuma vilivyotumiwa kama nguzo vilijengwa kwa njia tofauti na majengo mengine katika eneo hilo. Lakini watu walishangazwa zaidi kuona wageni weupe na wenyeji weusi wakifanya kazi katika mradi huo kwa umoja na shangwe.”

Mnamo Aprili 19, 1997, umati wa watu kutoka katika mataifa mbalimbali ulikusanyika kwa furaha kwa ajili ya kuiweka wakfu ofisi mpya ya tawi. Mwezi mmoja baadaye, kufuatia mapigano makali yaliyodumu kwa miaka mitano katika maeneo ya vijijini, kikundi cha waasi wa RUF kikalishambulia jiji la Freetown.

Ujenzi wa ofisi ya tawi jijini Freetown; ofisi ya tawi ilivyo sasa

Vita Jijini Freetown

Maelfu ya wapiganaji wa kikundi cha RUF wenye nywele zilizojisokota na waliojifunga vitambaa vyekundu kichwani waliingia kwenye mitaa ya jiji, wakipora, kubaka, na kuua. Alfred Gunn anakumbuka hivi: “Hali ilikuwa mbaya sana. Wamishonari wengi kutoka nchi za nje walihamishwa haraka. Wamishonari wa mwisho kuondoka walikuwa Billie na Sandra Cowan, Jimmie na Joyce Holland, mimi na Catherine.

“Tulisali pamoja na Wanabetheli wenyeji ambao walijitolea kubaki, kisha tukaondoka haraka kwenda kwenye kituo kilichohusika na kuwahamisha watu. Tukiwa njiani tulisimamishwa na wanajeshi waasi karibu 20 hivi wenye mwonekano mbaya sana, na waliokuwa wamelewa. Tulipowapa magazeti na pesa, walituruhusu tupite. Tukiwa na watu wengine zaidi ya 1,000 waliokuwa wakihamishwa, tulifika kwenye kituo cha ukaguzi kilichokuwa kikilindwa na wanajeshi wa Marekani waliokuwa na silaha nzito. Tulipanda helikopta ya kijeshi na kisha tukapelekwa kwenye meli ya kivita ya Marekani. Ofisa mmoja kwenye meli hiyo alituambia kwamba Jeshi la Majini la Marekani halijawahi kuhamisha raia wengi kadiri hiyo tangu Vita vya Vietnam. Siku iliyofuata, tulisafirishwa kwa helikopta hadi jijini Conakry, nchini Guinea. Tulipofika jijini Conakry tulianzisha ofisi ya tawi ya muda.”

Alfred na Catherine Gunn walikuwa miongoni mwa watu waliohamishwa

Wamishonari waliendelea kusubiri kwa wasiwasi habari kutoka jijini Freetown. Hatimaye, barua ilifika ambayo ilisema hivi: “Licha ya machafuko tunaendelea kugawanya trakti Habari Njema za Ufalme Na. 35, ‘Je, Watu Wote Watapata Kupendana?’ Watu wanaitikia vizuri, na hata baadhi ya wanajeshi waasi wanajifunza Biblia pamoja nasi. Hivyo, tumeazimia kuongeza utendaji wetu katika kazi ya kuhubiri.”

Jonathan Mbomah, ambaye alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko, anakumbuka hivi: “Hata tulifanya kusanyiko la pekee jijini Freetown. Programu hiyo ilituimarisha sana kiroho hivi kwamba nilisafiri hadi jijini Bo na Kenema ili kufanya kusanyako hilo katika maeneo hayo pia. Akina ndugu katika miji hiyo iliyoathiriwa na vita walimshukuru Yehova kwa chakula hicho kizuri sana cha kiroho.

“Mwishoni mwa mwaka 1997, tulifanya kusanyiko la wilaya kwenye Uwanja wa Taifa jijini Freetown. Katika siku ya mwisho ya programu hiyo, wanajeshi waasi waliingia uwanjani na kutuamuru tuondoke. Tuliwasihi sana tukiwaomba waturuhusu tumalizie programu ya kusanyiko. Baada ya majadiliano ya muda mrefu walikubali na wakaondoka. Zaidi ya watu 1,000 walihudhuria kusanyiko hilo, na 27 walibatizwa. Ndugu kadhaa walifunga safari hatari ili wafike jijini Bo na kuisikiliza programu hiyo tena. Hayo yalikuwa makusanyiko yenye kusisimua sana!”

Haikuwa rahisi kuandaa na kutimiza mahitaji ya kiroho na kimwili ya akina ndugu