Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JAMHURI YA DOMINIKA

Watadumu

Watadumu

Waliipata Kweli

Juana Ventura alijifunza Biblia kazi ya kuhubiri ilipokuwa imepigwa marufuku, na akabatizwa mwaka wa 1960 katika Mto Ozama. Pindi fulani, kasisi wa kievanjeli jijini Santo Domingo alitaka Juana afungwe gerezani kwa sababu alikuwa “akichukua wafuasi wake.” Ili kuthibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova ni waongo na kumwaibisha Juana, kasisi huyo alimwalika kanisani ili amuulize maswali kuhusu imani yake mpya.

“Aliniuliza maswali matatu,” anasema Juana, “‘Kwa nini hampigi kura? Kwa nini hamwendi vitani? Kwa nini mnajiita Mashahidi wa Yehova?’ Nilipokuwa nikijibu kila swali kwa kutumia Biblia, wafuasi wake wote walikuwa wakisoma Maandiko hayo na kushangazwa sana na yale waliyosoma. Wengi wao walitambua kwamba wameipata kweli. Kikundi chote kilianza kujifunza, na mwishowe 25 kati yao walijiweka wakfu kwa Yehova.” Tukio hilo lilichochea kazi ya kuhubiri jijini Santo Domingo.

Mashahidi wa Yehova Watadumu

Kuuawa kwa Trujillo kulileta athari nyingi za kisiasa. Kitabu cha Mwaka wa 1963 kiliripoti: ‘Barabara zilijaa wanajeshi, kulikuwa na maandamano na vurugu karibu kila mahali.’ Licha ya misukosuko ya kisiasa, kazi ya kuhubiri na kufundisha ilisonga mbele, na kufikia mwisho wa mwaka wa utumishi wa 1963, kulikuwa na jumla ya wahubiri 1,155.

Nathan Knorr kutoka makao makuu alipotembelea Jamhuri ya Dominika mwaka wa 1962, alifanya mipango ya kununua uwanja wa kujenga ofisi kubwa ili kusimamia kazi ya kuhubiri iliyokuwa ikiongezeka kwa kasi. Jengo la ghorofa mbili na Jumba la Ufalme lilijengwa katika uwanja huo mpya. Jumamosi, Oktoba 12, 1963, Frederick Franz, naye kutoka makao makuu, alitoa hotuba ya kuweka wakfu majengo mapya ya ofisi ya tawi. Ilikuwa wazi kwamba Mashahidi wa Yehova wamekusudia kudumu katika Jamhuri ya Dominika. Muda mfupi baada ya majengo hayo kuwekwa wakfu, wamishonari Harry na Paquita Duffield, ambao walikuwa wa mwisho kufukuzwa kutoka Kuba, waliwasili nchini.

Ongezeko Licha ya Mapinduzi

Mapinduzi yalitokea nchini Aprili 24, 1965. Katika kipindi hicho cha misukosuko, watu wa Yehova waliendelea kusitawi kiroho. Kufikia mwaka wa 1970, kulikuwa na wahubiri 3,378 katika makutaniko 63. Zaidi ya nusu ya wahubiri walikuwa wamejiunga na tengenezo katika miaka mitano iliyopita. Kitabu cha Mwaka wa 1972 kiliripoti hivi: “Watu wenye taaluma mbalimbali: Mainjinia, wakulima, madereva, wahasibu, wajenzi, maseremala, wanasheria, madaktari wa meno, naam, hata wanasiasa wa zamani; wote walivutwa pamoja kwa sababu ya kuipenda kweli na kumpenda Yehova.”