Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JAMHURI YA DOMINIKA

Uhuru, Kisha Marufuku

Uhuru, Kisha Marufuku

Uhuru Usiotazamiwa

Manuel Hierrezuelo aliuawa alipokuwa akihojiwa na wenye mamlaka

Katika kipindi chote cha miaka ya marufuku, Lennart na Virginia Johnson na Roy na Juanita Brandt walibaki katika migawo yao ya umishonari. “Mimi na Roy Brandt tuliitwa ili kuhojiwa na wenye mamlaka,” alikumbuka Lennart. “Mapema, maofisa wa serikali ya Trujillo walikuwa wamemwagiza Ndugu Manuel Hierrezuelo akutane nao ofisini.” Inasikitisha kwamba Manuel aliuawa wakati wa mahojiano hayo, hata hivyo alibaki mwaminifu hadi mwisho. Kwa hiyo, ni nini kilichowapata Lennart na Roy? Lennart aliendelea kusema: “Tulipowasili kila mmoja wetu alihojiwa peke yake, na yawezekana majibu yetu yalirekodiwa. Hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa wakati huo, lakini miezi miwili baadaye magazeti yalitangaza kwamba serikali ya Trujillo imeondoa marufuku dhidi ya Mashahidi wa Yehova na kwamba tulikuwa huru kuendelea na kazi yetu.”

Kabla ya marufuku mwaka wa 1950, kulikuwa na wahubiri 261 katika Jamhuri ya Dominika. Marufuku ilipoondolewa Agosti 1956, kulikuwa na wahubiri 522. Akina ndugu walifurahi sana kujua kwamba walikuwa huru kuhubiri hadharani baada ya kipindi cha miaka sita ya kufungwa gerezani, kuwekewa vizuizi, na kuchunguzwa kila mara.

Watu wa Yehova walitendaje mambo yalipobadilika? Mara moja, walianza kupanga kazi upya! Walitafuta mahali pa kufanyia mikutano ya kutaniko na kupanga ramani mpya za maeneo na faili za kutaniko. Sasa akina ndugu walifurahia kuagiza na kupokea machapisho. Walitumia vizuri sana uhuru wao wa kuhubiri. Matokeo ni kwamba baada ya miezi mitatu, mnamo Novemba 1956, wahubiri 612 walikuwa wakihubiri habari njema.

Makasisi Waeneza Chuki

Barua ya Toledano ilitaja mipango ya kuzuia machapisho yetu kuingia nchini

Hata hivyo, mara moja makasisi Wakatoliki walianza kutunga njama ya kuwakashifu Mashahidi. Kwa msingi wa makubaliano kati ya Trujillo na Vatikani, makasisi walizidisha bidii yao ya kushawishi serikali ikomeshe kabisa kazi ya Mashahidi. Kasisi Mkatoliki Oscar Robles Toledano alimtumia barua Waziri wa Mambo ya Ndani, Virgilio Álvarez Pina, akiiomba serikali iunge mkono jitihada zake za “kuamsha dhamiri za watu wa Dominika ili kuwalinda dhidi ya hatari kubwa ya dhehebu la ‘Mashahidi wa Yehova’.”

Toledano alieleza kwamba lengo lake kuu lilikuwa “kukomesha kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuwageuza watu imani.” Vilevile barua ya Toledano ilipendekeza kwamba machapisho yetu yasiingizwe nchini humo, “hasa kitabu ‘The Truth Shall Make You Free’ na gazeti la Mnara wa Mlinzi.”

Kupigwa Marufuku Tena

Viongozi wa kidini na wafuasi wao waliokuwa katika serikali ya Trujillo waliunga mkono njama ya kuwashambulia Mashahidi. Juni 1957, Francisco Prats-Ramírez, rais wa Chama cha Dominika alimwandikia Trujillo barua iliyosema: “Ninapanga mikutano kadhaa ili kupambana na msimamo hatari na usio wa kizalendo wa Mashahidi wa Yehova.”

Kampeni hiyo ya uchochezi ilifaulu mara moja, kama ilivyoelezwa katika kitabu Trujillo—Little Caesar of the Caribbean: “Mwaka wa 1957 magazeti nchini Dominika yalichapisha mashtaka kadhaa yaliyotolewa na maofisa wenye vyeo Serikalini wakidai kwamba Mashahidi wa Yehova walijihusisha na shughuli ‘hatari na uchochezi.’ Mambo yaliharibika zaidi kasisi Mjesuti aitwaye Mariano Vásquez Sanz alipopinga dhehebu hilo kupitia kituo cha redio cha La Voz Dominicana [Sauti ya Dominika], kilichomilikiwa na Trujillo, akidai kuwa ni watumishi wa Ukomunisti na akasema kwamba wafuasi wake ni ‘wajanja, wakaidi, wahalifu, na maadui wasaliti.’ Mara moja, barua iliyotiwa sahihi na Maaskofu Wakuu Ricardo Pittini na Octavio Antonio Beras iliwahimiza makasisi wawalinde waumini wao dhidi ya ‘uasi huo mbaya wa kidini.’”

Jitihada za pamoja za Kanisa na Serikali zilitimiza lengo lililokusudiwa. Mwezi wa Julai, Bunge la Jamhuri ya Dominika lilitunga sheria iliyopiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Kisha, polisi wakaanza kuwapiga na kuwatendea kikatili ndugu na dada zetu. Kwa ujumla, ndugu na dada 150 hivi walikamatwa.