Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 6

Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?

Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?

MUNGU aliumba dunia iwe makao yanayowafaa wanadamu. Neno lake linasema: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.”—Zaburi 115:16.

Kabla ya kumuumba mtu wa kwanza, Adamu, Mungu alichagua sehemu ndogo ya dunia iliyoitwa Edeni na huko akatengeneza bustani nzuri. Maandiko yanasema kwamba mto Efrati na mto Tigri (Hidekeli) ilitoka katika bustani ya Edeni. * Inadhaniwa kwamba bustani ya Edeni ilikuwa katika sehemu ambayo leo ni mashariki mwa Uturuki. Ndiyo, bustani ya Edeni ilikuwa duniani!

Mungu alimuumba Adamu na kumweka katika bustani ya Edeni “ailime na kuitunza.” (Mwanzo 2:15) Baadaye, Mungu akamuumbia Adamu mke—Hawa. Mungu akawaamuru wenzi hao: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28) Bila shaka, Mungu “hakuiumba [dunia] tu bila sababu, [bali] aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.

Hata hivyo, Adamu na Hawa walimwasi Mungu kwa kuvunja sheria yake kimakusudi. Hivyo, Mungu akawaondoa kutoka katika bustani ya Edeni. Paradiso ikapotea. Nayo madhara yaliyosababishwa na dhambi ya Adamu yakaendelea. Maandiko yanasema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Je, Yehova alitupilia mbali kusudi lake la awali—kwamba dunia iwe paradiso inayokaliwa na watu wenye furaha? Hapana! Mungu anasema: ‘Neno langu linalotoka katika kinywa changu, halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.’ (Isaya 55:11) Paradiso itarudishwa duniani!

Maisha katika Paradiso yatakuwa namna gani? Fikiria ahadi za Kimaandiko zinazoonyeshwa katika kurasa mbili zinazofuata.

^ fu. 4 Andiko la Mwanzo 2:10-14 husema: “Kulikuwa na mto unaotoka katika Edeni ili kuinywesha bustani maji, na kutoka hapo ukaanza kugawanyika na kuwa vichwa vinne. Jina la ule wa kwanza ni Pishoni . . . jina la mto wa pili ni Gihoni . . . jina la mto wa tatu ni Hidekeli [au, Tigri]; ndio unaoelekea upande wa mashariki wa Ashuru. Na mto wa nne ni Efrati.” Mito miwili ya kwanza haijulikani wala mahali ilipokuwa hapajulikani.