Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 3

Mashauri Yenye Hekima Yanayoboresha Maisha

Mashauri Yenye Hekima Yanayoboresha Maisha

WAZIA kwamba daktari mpya amehamia eneo lenu. Huenda mwanzoni usimwamini. Lakini namna gani ikiwa baadhi ya rafiki zako wametibiwa naye na afya yao imekuwa nzuri? Huenda wewe pia ungefikiria kumwona daktari huyo, sivyo?

Kwa njia fulani, Maandiko Matakatifu ni kama daktari huyo. Watu fulani huogopa kutafuta mashauri ya Maandiko hayo. Lakini wanapoyatumia mashauri yaliyomo, maisha yao huwa mazuri sana. Ona mifano kadhaa.

Kutatua Matatizo Katika Ndoa

“Mapema katika ndoa yetu, nilihisi kwamba mume wangu, Dumas, alikuwa akinipuuza,” akumbuka Sumiatun. “Mara nyingi kwa sababu ya kutamaushwa, nilimtukana, nikamtupia vitu, na hata kumpiga. Nyakati nyingine ningekasirika sana mpaka ningezirai.

“Dumas alipoanza kujifunza Maandiko Matakatifu, nilimdhihaki. Hata hivyo, nilikuwa nikisikiliza kwa siri yale aliyokuwa akijifunza nikiwa katika chumba kingine. Siku moja, nilisikia mistari fulani ikisomwa: ‘Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana . . . Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.’ (Waefeso 5:22, 33) Maneno hayo yalinigusa moyo. Nikamwomba Mungu anisamehe kwa kumtukana mume wangu, na nikamwomba Mungu anisaidie kuwa mke bora. Muda si muda, Dumas nami tukaanza kujifunza Maandiko pamoja.”

Dumas na Sumiatun

Pia, Maandiko matakatifu yanasema: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28) Sumiatun asema: “Kujifunza mambo hayo kulikuwa na matokeo mazuri kwetu. Nilianza kumpa Dumas chai alipofika nyumbani kutoka kazini na nilizungumza naye kwa fadhili. Dumas naye alinipenda zaidi na kunisaidia kufanya kazi za nyumbani. Sote tulijitahidi ‘kuwa wenye fadhili, wenye huruma nyororo, wenye kusameheana kwa hiari.’ (Waefeso 4:32) Hivyo, hatua kwa hatua tukaanza kupendana na kuheshimiana. Kwa zaidi ya miaka 40 sasa, ndoa yetu imekuwa yenye furaha. Mashauri yenye hekima katika Neno la Mungu yaliokoa ndoa yetu!”

Kudhibiti Hasira

“Nilikuwa mwenye hasira kali,” asema Tayib. “Mara nyingi nilijiingiza katika ugomvi na kuwatisha wengine kwa bunduki. Pia nilizoea kumpiga mke wangu, Kustriyah, na kumwangusha sakafuni. Watu wengi waliniogopa.

Kustriyah na Tayib husali pamoja kila usiku

“Siku moja, nilisoma maneno haya ya Yesu: ‘Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi.’ (Yohana 13:34) Maneno hayo yalinigusa moyo sana, nami nikaazimia kubadilika. Nilipopandwa na hasira, nilimwomba Mungu anisaidie niwe mtulivu. Baada ya muda, hasira yangu ilipungua. Mimi na mke wangu, tulitumia shauri hili la Waefeso 4:26, 27: ‘Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.’ Tulisoma Maandiko na kusali pamoja kila usiku. Kufanya hivyo kulituondolea mahangaiko ya siku na kutusaidia kuwa na uhusiano wa karibu.

“Sasa ninajulikana kuwa mtu mwenye amani. Mke na watoto wangu wananipenda na kuniheshimu. Nina marafiki wengi, na ninahisi kuwa karibu na Mungu. Kwa kweli mimi ni mwenye furaha.”

Kushinda Mazoea ya Kutumia Dawa za Kulevya

Goin

“Nilikuwa nikishirikiana na genge la vijana, nilikuwa mvutaji sugu wa sigara, na mara nyingi usiku nililala barabarani nikiwa mlevi,” asema Goin. “Pia nilitumia na kuuza dawa haramu—bangi na dawa nyingine za kulevya—ambazo nilificha ndani ya fulana yangu ya kuzuia risasi. Ingawa nilionekana na kutenda kama jasiri, nyakati zote niliishi kwa woga.

“Kisha mtu fulani akanionyesha andiko hili: ‘Mwanangu, usiisahau sheria yangu . . . kwa sababu utaongezewa urefu wa siku na miaka ya uzima na amani.” (Methali 3:1, 2) Nilitamani maisha marefu na yenye amani! Pia nilisoma: ‘Wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.’ (2 Wakorintho 7:1) Hivyo basi, nikaacha kutumia dawa za kulevya, nikavunja uhusiano wangu pamoja na lile genge, nami nikaanza kumtumikia Mungu.

“Kwa zaidi ya miaka 17 sasa, sijatumia dawa za kulevya. Nina afya nzuri, familia yenye furaha, marafiki wazuri, na dhamiri safi. Na badala ya kulala barabarani nikiwa mlevi, mimi hulala kitandani kwa utulivu kila usiku.”

Kushinda Ubaguzi

“Nikiwa kijana, nilikuwa mhalifu,” akumbuka Bambang, “nami niliwachukia sana watu wa kabila fulani dogo.

“Hata hivyo, baada ya muda, nilianza kumtafuta Mungu. Katika harakati zangu za kumtafuta, nikakutana na kikundi fulani kilichokuwa kikijifunza Maandiko Matakatifu. Nilisalimiwa kwa shauku na watu wa kabila lilelile nililokuwa nikilichukia! Pia nilitambua kwamba katika kikundi hicho cha kujifunza, watu wa jamii tofauti-tofauti walichangamana kwa furaha. Nilishangaa! Ndipo nikaelewa andiko linalosema: ‘Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.’—Matendo 10:34-35.

“Leo, sina chuki kuwaelekea wengine. Baadhi ya rafiki zangu ni wa kabila nililokuwa nikilichukia. Kupitia Maandiko Matakatifu, Mungu amenifundisha kuwa na upendo.”

Sasa, Bambang, hufurahia kushirikiana na watu wa jamii tofauti-tofauti

Kuacha Jeuri

“Nilipokuwa ningali kijana, nilifungwa gerezani mara tatu—mara mbili kwa kuiba na mara moja kwa kumdunga mtu kisu,” asema Garoga. “Baadaye, nikajiunga na kikundi cha waasi na kuwaua watu wengi. Baada ya mapigano hayo, niliongoza kikundi cha wahalifu kilichofanya unyang’anyi wa kimabavu. Niliandamana na walinzi wangu kila mahali. Nilikuwa mtu jeuri na hatari sana.

Garoga si jeuri tena bali sasa yeye ni mwalimu anayeheshimika wa Neno la Mungu

“Kisha, siku moja, nikasoma andiko hili: ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya.’ (1 Wakorintho 13:4, 5) Maneno hayo yaligusa moyo wangu. Nilihamia eneo lingine, nikajifunza Maandiko, na kutumia mashauri yake maishani mwangu.

“Mimi si mjeuri tena. Badala yake, ninaheshimiwa nikiwa mwalimu wa Neno la Mungu. Maisha yangu yana kusudi na ni yenye kuridhisha kwelikweli.”

Neno la Mungu Lina Nguvu

Masimulizi hayo na mengine mengi yanathibitisha kwamba “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Waebrania 4:12) Mashauri yake ni rahisi, yana hekima, na ni yenye kujenga.

Je, Maandiko Matakatifu yanaweza kukusaidia pia? Ndiyo, yanaweza kukusaidia kutatua tatizo lolote unalokabili. “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

Hivyo basi, acheni tuchunguze mafundisho kadhaa ya msingi yaliyo katika Maandiko Matakatifu.