Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

INDONESIA

Matokeo Mazuri Katika Java Magharibi

Matokeo Mazuri Katika Java Magharibi

Theodorus Ratu

Mwaka wa 1933, Frank Rice alimwalika Theodorus Theo Ratu ambaye ni mzaliwa wa Sulawesi Kaskazini amsaidie kazi katika depo ya vitabu huko Jakarta. Theo anakumbuka hivi: “Nilipendezwa sana na kazi ya kuhubiri Ufalme, nami nilianza kuhubiri pamoja na Ndugu Rice. Baadaye nilijiunga na Bill Hunter kuhubiri huko Java, kisha tukaanza safari pamoja na wengine kuelekea Sumatra kwa kutumia mashua iliyoitwa Lightbearer.” Theo alikuwa Mwindonesia wa kwanza kukubali kweli, naye alifanya upainia kwa miaka mingi huko Java, Sulawesi Kaskazini, na Sumatra.

Mwaka uliofuata, Bill Hunter alimwachia Felix Tan, mwanafunzi aliyeishi Jakarta kijitabu Where Are the Dead? Felix aliporudi kwao Bandung, Java Magharibi alimwonyesha mdogo wake, Dodo, kijitabu hicho. Walishangaa walipojifunza kwamba mwanadamu wa kwanza, Adamu, hakuwa na nafsi isiyoweza kufa. Adamu mwenyewe alikuwa nafsi. (Mwa. 2:7) Felix na Dodo wakiwa na njaa ya kiroho, nao walitafuta kwa bidii vitabu vikuukuu vilivyochapishwa na Watch Tower kwenye maduka ya vitabu huko Bandung. Pia, waliwaeleza watu wa familia mambo waliyojifunza. Baada ya kumaliza kusoma vitabu na vijitabu vyote walivyopata, waliandika barua na kuituma Jarkata kwenye depo ya vitabu. Bila kutazamia, Ndugu Frank Rice aliwatembelea ili kuwatia moyo na kuwaletea vitabu vipya.

Familia ya Tan

Muda mfupi baada ya Ndugu Rice kurudi Jakarta, wenzi wapya wa ndoa, Clem na Jean Deschamp walitembelea Bandung kwa siku 15. Felix anasimulia hivi: “Ndugu Deschamp aliuliza familia yetu ikiwa tungependa kubatizwa. Mimi, Dodo, mdogo wangu wa kike Josphine (Pin Nio, mama yangu Kang Nio), tulijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.” * Baada ya kubatizwa, familia ya Tan walishiriki kampeni ya kuhubiri kwa siku tisa pamoja na Clem na Jean. Clem aliwaonyesha jinsi ya kuhubiri kwa kutumia kadi ya ushuhuda ambayo ilikuwa na ujumbe mfupi wa Biblia kwa lugha tatu. Muda mfupi baadaye, kikundi cha Bandung kikawa kutaniko la pili nchini Indonesia.

Kofia ya Papa

Kazi ya kuhubiri ilipoendelea kuongezeka, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walitambua utendaji wa Mashahidi. Makasisi na mawakala walitumia magazeti ya habari kuwashambulia Mashahidi na imani yao. Habari hizo zilifanya maofisa wa Idara ya Mambo ya Kidini wamwite Frank Rice ili wamhoji. Waliporidhika na majibu ya Frank Rice waliruhusu kazi yetu iendelee. *

Mwanzoni mwa miaka ya 1930 maofisa wengi wa kikoloni waliipuuza kazi ya kuhubiri. Lakini utawala wa Nazi ya Ujerumani ulipoenea huko Ulaya, baadhi ya maofisa na hasa Wakatoliki, walianza kuwapinga Mashahidi. Clem Deschamp anakumbuka hivi: “Siku moja ofisa wa Idara ya Forodha aliyekuwa Mkatoliki alizuia shehena ya vitabu akidai kwamba vilikuwa na habari zilizopinga utawala wa Nazi. Nilipopeleka malalamiko katika idara hiyo, ofisa aliyezuia vitabu hakuwepo kazini, badala yake nilimkuta ofisa mwingine mwenye urafiki ambaye hakuwa Mkatoliki, akaniruhusu nichukue vitabu, akisema ‘Chukua kadiri uwezavyo kabla mhusika hajarudi!’”

Jean Deschamp alisema hivi: “Katika kisa kimoja, maofisa walitulazimisha tuondoe picha mbili kwenye kitabu Enemies. Walipinga picha ya nyoka (Shetani) na kahaba mlevi (dini ya uwongo). Picha zote mbili zilikuwa na kofia ya papa. * Tulikuwa tumeazimia kugawanya kitabu hicho. Hivyo, sote watatu tulikaa bandarini tukifanya kazi ngumu ya kupekua maelfu ya vitabu ili kufuta picha zenye kofia ya papa.

Picha mbili za kitabu Enemies zilizokataliwa na maofisa

Vita vilipokaribia kutukia huko Ulaya, machapisho yetu yalifunua kwa ujasiri unafiki wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na jinsi zinavyojihusisha na siasa. Hivyo, makasisi waliongeza uchochezi kwa wenye mamlaka ili wazuie kazi yetu na baadhi ya machapisho yakapigwa marufuku.

Hata hivyo, ndugu waliazimia kuendelea na kazi na waliitumia vizuri mashine waliyopata kutoka Australia. (Mdo. 4:20) Akielezea mojawapo ya mbinu hizo, Jean Deschamp anasema hivi: “Kila tulipochapisha kijitabu au gazeti, tuliwapelekea wenye mamlaka nakala moja tu ili kupata idhini. Tulichapisha na kugawanya machapisho mwanzoni mwa juma. Kisha, mwishoni mwa juma tulipeleka nakala moja kwa mwanasheria mkuu. Chapisho lilipokataliwa, tulisikitika na kurudi haraka kiwandani ili kuchapisha machapisho mengine.”

Ndugu na dada waliogawa machapisho yaliyopigwa marufuku walijitahidi sana kuwakwepa polisi. Kwa mfano, Charles Harris alipokuwa akihubiri Kediri, Java Mashariki, bila kutazamia alimhubiria polisi.

Polisi huyo akamwambia hivi: “Sikuzote nimekuwa nikiwatafuta. Subiri nitafute orodha ya vitabu vyenu vilivyopigwa marufuku.”

Charles anasema hivi: “Polisi huyo alipoingia ndani, nilificha machapisho yaliyopigwa marufuku kwenye mifuko ya koti langu. Aliporudi nilimpa vijitabu 15 ambavyo havikuwa vimepigwa marufuku. Alinipa mchango wake wa hiari, kisha nikagawa yale machapisho yaliyopigwa marufuku katika mtaa huohuo.

Kuchapisha Chini ya Hali Ngumu

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoenea Ulaya, usafirishaji wa machapisho kutoka Uholanzi hadi Indonesia ulisitishwa. Hata hivyo, ndugu walitazamia tatizo hilo na walifanya mipango ili magazeti yachapishwe na kampuni ya biashara jijini Jakarta. Toleo la kwanza la gazeti Consolation (sasa Amkeni!) lilitolewa katika Kiindonesia Januari 1939, na Mnara wa Mlinzi lilitolewa baadaye. Kisha, ndugu wakanunua mashine ndogo na wakaanza kuchapisha wenyewe magazeti. Mwaka wa 1940 walipokea mashine kubwa kutoka Australia na waliitumia kuchapisha vijitabu na magazeti kwa Kiindonesia na Kiholanzi kwa gharama zao.

Mashine ya kwanza ya kuchapisha ikiwasili katika bohari la Jakarta

Mwishowe, Julai 28, 1941, serikali ilipiga marufuku machapisho yote ya Watch Tower Society. Jean Deschamp anakumbuka hivi: “Siku moja asubuhi nilipokuwa ofisini nikichapisha, polisi watatu wakiwa na ofisa mkuu Mholanzi aliyevaa sare kamili, walifungua mlango kwa nguvu. Hatukushtuka. Siku tatu zilizopita tulikuwa tumepata habari kwamba machapisho yetu yangepigwa marufuku hivi karibuni. Ofisa huyo mkatili alisoma tangazo na akatulazimisha tufunge kiwanda chetu. Lakini mume wangu akamwambia kwamba amechelewa. Kiwanda kilikuwa kimeuzwa siku moja iliyopita!”

Hata hivyo, Biblia haikupigwa marufuku. Hivyo, ndugu waliendelea kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa kutumia Biblia. Hata waliongoza mafunzo ya Biblia. Kwa kuwa kulikuwa na uwezekano wa vita kutokea Asia, mapainia wa kigeni waliombwa warudi Australia.

^ fu. 1 Baadaye, baba na wadogo zake Felix wakawa Mashahidi. Dada yake Josphine aliolewa na André Elias na wakahudhuria Shule ya Gileadi. Simulizi la maisha yake lilichapishwa katika gazeti la Amkeni! Septemba 2009

^ fu. 1 Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, Frank alirudi Australia na akapata familia. Ndugu Rice alikufa mwaka wa 1986.

^ fu. 3 Picha hizo zilitegemea Ufunuo 12:9 na 17:3-6.