Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

INDONESIA

Kazi Yaongezeka Eneo la Mashariki

Kazi Yaongezeka Eneo la Mashariki

Mwaka wa 1953, Peter Vanderhaegen alipewa mgawo wa kuzungukia nchini Indonesia. Mzunguko wake ulitia ndani nchi nzima yenye ukubwa wa kilometa 5,100 kutoka mashariki kwenda magharibi na kilometa 1,800 kutoka kaskazini kwenda kusini. Alipokuwa akizungukia eneo hilo kubwa, mara nyingi alijionea matukio mbalimbali yenye kusisimua.

Peter Vanderhaegen

Mwaka wa 1954, Ndugu Vanderhaegen alisafiri kuelekea eneo la mashariki ya Indonesia, eneo lenye dini nyingi kutia ndani visiwa vya Bali, vilivyo na idadi kubwa ya Wahindu; Lombok na Sumbawa vyenye Waislamu wengi; Flores, ni Wakatoliki; na Sumba, Alor, na Timor, wengi wakiwa Waprotestanti. Alipokuwa akisafiri kwa boti, alihubiri kwa ufupi katika visiwa kadhaa kabla ya kufika Kupang, mji mkuu wa Timor. Ndugu Vanderhaegen alisimulia hivi: “Nilihubiri Timor kwa majuma mawili. Licha ya mvua nyingi, niligawa machapisho yote niliyokuwa nayo, nilipata maombi 34 ya magazeti, na kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia.” Mapainia wa pekee waliendelea kuwafuatilia watu waliopendezwa na kuanzisha kutaniko huko Kupang. Kutoka huko habari njema zikaenea kufikia visiwa jirani vya Rotè, Alor, Sumba, na Flores.

Makasisi Waprotestanti huko Kupang walikasirika sana, walipowaona waumini wao wakiwasikiliza Mashahidi wa Yehova. Kasisi mmoja mwenye cheo kikubwa alimwagiza Thomas Tubulau, mzee aliyekuwa mfua vyuma, aache kujifunza na Mashahidi, na kwamba ikiwa hataacha kuwaambia wengine mambo aliyojifunza, basi damu itamwagika. Thomas alijibu hivi kwa ujasiri: “Hakuna Mkristo anayeweza kusema kama ulivyosema. Sitarudi tena kanisani kwako.” Thomas akawa mhubiri wa Ufalme mwenye bidii, na binti yake akawa painia wa pekee.

Hata hivyo, Makasisi wa Timor waliazimia kuwafutilia mbali Mashahidi wa Yehova. Mwaka wa 1961, walifanikiwa kuishawishi Idara ya Mambo ya Kidini na mamlaka ya jeshi ya eneo hilo ipige marufuku kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hivyo, ndugu wakabadili njia za kutoa ushahidi. Walizungumza na watu madukani na visimani, pia wavuvi kwenye fukwe za bahari, na familia zilizokuwa zinatunza makaburi. Baada ya mwezi mmoja, jeshi lilifuta msimamo wake na kutangaza redioni kwamba dini katika Timor zilikuwa huru. Idara ya Mambo ya Kidini iliposisitiza kwamba kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba bado ilikuwa imezuiwa, ndugu waliomba madai yaandikwe. Maofisa hao walikataa. Hatimaye, akina ndugu waliendelea na kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba bila kizuizi.

Wamishonari Piet na Nell de Jager na Hans, Susie, van Vuure walipowasili Papua mwaka wa 1962, wao pia walipingwa vikali na makasisi wa kidini. Makasisi watatu waliwazuia wamishonari na kuwataka wakahubiri mahali pengine. Makasisi hao waliwasingizia kwa uwongo Mashahidi wa Yehova kwenye majukwaa, machapisho, na redio kwamba wanasumbua serikali. Pia waliwarubuni, kuwatisha, au kuwahonga waumini wote walioanza kujifunza na wamishonari hao. Pia waliwachochea machifu wa eneo hilo wapinge kazi ya kuhubiri.

Jitihada hizo zilishindwa chifu mmoja alipowaalika wamishonari wazungumze na watu wa kijiji chake. Hans anasimulia hivi: “Baada ya chifu kuwakusanya wanakijiji, mimi na Piet tulitoa hotuba mbili fupi zilizofafanua kazi yetu. Kisha, wake zetu walionyesha jinsi tunavyobisha hodi, kukaribishwa, na kushiriki nao ujumbe mfupi wa Biblia. Chifu huyo na watu wake waliitikia vizuri maonyesho hayo na wakaturuhusu tuendelea kuhubiri.”

Tukio hilo lilifanana na matukio mengine katika sehemu nyingine. Waislamu walipinga kazi yetu ya kuhubiri mara chache sana; sikuzote upinzani ulitoka kwa makasisi wa dini zinazodai kuwa Kikristo. Hali hiyo imeendelea mpaka leo.

‘Kupelekwa Mbele ya Magavana . . . ili Kutoa Ushahidi’

Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtakokotwa na kupelekwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” (Mt. 10:18) Mara nyingi maneno hayo yamethibitika kuwa kweli nchini Indonesia.

Mwaka wa 1960, mwanatheolojia mashuhuri Mholanzi huko Jakarta aliandika kitabu chake kilichosema Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wa uwongo. Kitabu hicho kiliwachochea makasisi wengi waanze kuwashambulia Mashahidi. Kwa mfano, kasisi wa mji fulani aliandikia barua Idara ya Mambo ya Kidini akidai kwamba Mashahidi “wanawasumbua waumini wa makanisa yao.” Maofisa walipowaita ndugu ili kujibu mashtaka, walieleza ukweli wa mambo na kutoa ushahidi mzuri. Ofisa mmoja wa kidini aliwaambia hivi wenzake: “Waacheni Mashahidi wa Yehova. Wanawaamsha Waprotestanti waliolala.”

Wakishusha shehena la kitabu Paradise, 1963

Mwaka wa 1964, kikundi cha makasisi Waprotestanti cha Papua kilikata rufaa kwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Kidini na Kijamii ili iamuru kazi ya Mashahidi wa Yehova ipigwe marufuku. Hata hivyo, ofisi ya tawi iliomba ikutane na kamati hiyo ili kujitetea. Tagor Hutasoit alisema hivi: “Tulijadiliana na kamati hiyo kwa karibu saa moja hivi na kueleza waziwazi kuhusu kazi yetu ya elimu ya Biblia. Mwanasiasa mmoja Mprotestanti, alitushutumu kwamba tunasababisha machafuko ya kidini katika Papua. Hata hivyo, washiriki wengi wa kamati hiyo ambao ni Waislamu walitutetea. Walituambia hivi: ‘Katiba inaruhusu uhuru wa ibada, hivyo mna haki ya kuhubiri.’” Baada ya mkutano huo, ofisa mwenye cheo cha juu huko Papua alitangaza hivi: “Serikali mpya . . . inalinda uhuru wa kidini, na hilo linahusu pia dini mpya.”