Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Njoni Yatazameni Matendo ya Mungu”

“Njoni Yatazameni Matendo ya Mungu”

“Njoni Yatazameni Matendo ya Mungu”

TUKIWA Mashahidi wa Yehova, kwa uhakika twawaalika watu wa duniani pote waje waone matendo ya Mungu. (Zab. 66:⁠5) Matendo ya Yehova ni dhahiri sana si kwa asili tu bali pia katika kazi ya watu wake. Baada ya wewe kusoma ripoti ya ulimwenguni pote iliyotangulia, sisi twauliza, Ni nani ila Mungu ambaye angeweza kutusukuma na kutupa nguvu kutimiza yote yaliyofanywa wakati wa mwaka wa utumishi wa 1993? Kwa kielelezo, jumla ya muda wa saa zilitotumiwa kuhubiri ulikuwa zaidi ya 1,057,341,000, ambazo ni saa 32,431,000 zaidi ya mwaka uliotangulia. Wastani wa idadi ya mafunzo ya Biblia ulikuwa juu kwa 237,460, kufikia jumla ya 4,515,587. Yote hayo yalihitaji “nguvu ipitayo ile ya kawaida” isiyo na kifani. (2 Kor. 4:⁠7, NW) Ni Mungu tu ndiye angetoa nguvu ihitajiwayo. Mtume Paulo alijulisha hivi: “Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.” (Flp. 2:13) Kwa hiyo, sifa yote yamwendea yule Mungu aishiye, atiaye roho takatifu yake ndani yetu!

Twawaalika wote waje waone jinsi kani ya utendaji ya Yehova inafanya kazi miongoni mwa Mashahidi wake. Upendo na amani ni matunda ya kani ya utendaji ya Yehova, roho takatifu yake. (Gal. 5:​22, 23) Njoni katika Afrika Kusini yenye mchafuko wa kijamii, muone vikundi vya ujenzi vya kutoka jamii mbalimbali vya Mashahidi wa Yehova vyashirikiana kujenga Majumba ya Ufalme mapya na kukutana pamoja kwa amani. Njoni katika Israel muone Wayahudi na Waarabu walio Mashahidi wakihubiri pamoja habari njema za Ufalme wa Kimesiya kwa shangwe. Katika Ailandi ya Kaskazini yenye vita-vita, njoni muone Mashahidi wa Yehova ambao hapo awali walikuwa Wakatoliki na Waprotestanti wenye kupigana wakiendelea vizuri sasa wakiwa ndugu Wakristo. Katika mabara ya ile iliyokuwa Yugoslavia​—⁠Bosnia na Herzegovina, Kroatia, na Serbia, ambako utukuzo wa taifa na chuki ya kidini zimetokeza vita vibaya sana⁠—​njoni, muone Mashahidi wa Yehova waliounganika kwa amani na upendo, wakiwa si sehemu ya mapigano hayo makatili.

Katika 1993, maelfu ya wajumbe kutoka nchi nyingi mbalimbali walisafiri hadi kwenye “Ufundishaji wa Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya katika sehemu nyingi za dunia. Wao waliona nini? Wao walijionea wenyewe matendo ya Yehova katika Stediamu ya Lokomotivu ya Moscow na katika Kiev, Ukrainia. Walisisimuka kukutana na ndugu na dada waliokuwa wamevumilia miongo mingi ya utawala wa Kikomunisti. Hao walio waaminifu waweza kusema kwa Yehova, kama vile mtunga-zaburi alivyosema: “Uliwapandisha watu juu ya vichwa vyetu. Tulipita motoni na majini; ukatutoa na kutuleta kunako wingi. Njoni, sikieni, ninyi nyote mnaomcha Mungu, nami nitayatangaza aliyonitendea roho [“nafsi,” NW ] yangu.” (Zab. 66:​12, 16) Mioyo yetu yashangilia kuona jinsi mkono wenye nguvu wa Yehova ulivyofanyiza mambo hivi kwamba watu wengi zaidi katika mabara haya ya ile iliyokuwa Sovieti wawe na fursa ya kuja kumjua yeye. Wasikivu wanachukua msimamo wao upesi kama nini! Kwa kushangaza, kulikuwa na 8,891 waliobatizwa kwenye mikusanyiko hiyo miwili tu katika Moscow na Kiev! Kwa kweli, Neno la Mungu lasonga mbele haraka, na watu wanasema juu ya mambo yake matukufu!​—⁠Mdo. 2:11; 2 The. 3:⁠1.

Matendo ya Yehova yanaonekana wazi katika upanuzi wa haraka wa vifaa vipya vya tawi kotekote duniani. Katika Brooklyn, New York, jengo jipya la makao lenye orofa 30 la Sosaiti lakabili majengo ya Manhattan kwenye Barabara ya 90 Sands. Wakati wa Oktoba, familia ya Betheli ilitalii kwa furaha orofa kumi za chini, zilizokuwa tayari kutumiwa. Kitakapokamilishwa, kifaa hiki kipya kifaacho kitatoshea wajitoleaji wa Betheli karibu elfu moja. Yehova amekuwa nasi, si katika makao makuu tu, bali pia kotekote duniani katika miradi ya ujenzi, akifanya iwezekane kupata mahali pa kujenga na majengo kwa ajili ya vifaa vya tawi na Majumba ya Makusanyiko na kukodi vifaa kwa ajili ya matumizi ya Sosaiti katika mahali pengi. Nchi zaidi ya 57 zimehusika! Kujapokuwa hali za kiuchumi zenye msukosuko kotekote ulimwenguni, mkono wa Yehova haujakuwa mfupi katika kuandalia tengenezo lake nyenzo za kifedha na za kibinadamu zihitajiwazo ili kuendeleza kazi ya Ufalme.​—⁠Isa. 59:⁠1.

Kitengenezo, Yehova amekuwa mtendaji katika kutia nguvu watu wake. Uthibitisho wa hilo ungeweza kuonwa katika mikutano ya pekee ya washiriki wa Halmashauri ya Tawi iliyofanywa wakati wa 1993 katika sehemu nane, kutia na Watchtower Farms kwenye Wallkill, New York, iliyotia ndani ndugu kutoka matawi yapatayo 100. Washiriki wa Baraza Linaloongoza na wengineo walishiriki katika kutoa mafundisho. Wale ndugu wenye kuchukua daraka waliohudhuria walipewa vifaa bora zaidi ili kuandaa mwelekezo uleule wa kitheokrasi katika matawi yao mbalimbali.

Tuingiapo katika 1994, acheni tuendelee kujishughulisha na matendo ya Yehova. “Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi,” Yesu Kristo akasema. (Yn. 5:17) Kwa hakika, Yehova Mungu na Yesu Kristo wataendelea kuwa wafanyakazi watendaji, wakiwavuta maelfu zaidi ya wale walio mfano wa kondoo waingie katika lile kundi moja chini ya yule mchungaji mmoja. (Yn. 6:44; 10:16) Wewe utahusika jinsi gani katika utendaji wa Mungu na wa Mwanae? Twayahimiza hivi yale maelfu ya vijana na wengineo katika makutaniko: Tumieni nishati zenu kumletea Mungu utukufu. Panga maisha yako yahusu utendaji wa kuhubiri na kufanya wanafunzi, utakaotokeza uhai wa milele kwako wewe na kwa wale wanaokusikiliza. (1 Tim. 4:16) Na kwa wote ambao wamevumilia katika kazi hiyo kwa miaka mingi, twawahimiza: “Nanyi jipeni nguvu, wala mikono yenu isilegee; kwa maana kazi yenu itakuwa na ijara.”​—⁠2 Nya. 15:7; Kol. 3:⁠24.

Dhiki kubwa ikaribiapo, ulimwengu utakuwa wenye ukosefu wa usalama na wenye msukosuko zaidi ya vile ulivyo. Acheni sisi sote tuazimie kutumia kwa ukamili zaidi shauri lenye hekima la andiko la mwaka la 1994: “Mtumaini BWANA [“Yehova,” NW ] kwa moyo wako wote.” (Mit. 3:⁠5) Twaweza kutumaini kikamili kwamba Yehova atatenda kwa niaba yetu tusalipo na kufanya kazi kwa upatano naye katika kufanya mapenzi yake.

Yehova na awabariki ninyi nyote.

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova