Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mashahidi wa Yehova hujaribu kukaza katika watoto wao kanuni za Kikristo zilizo za kweli

Kanuni za Adili Zinazostahili Staha

Kanuni za Adili Zinazostahili Staha

Muda wote wa historia, wanaume na wanawake hodari wamechukua msimamo ulio kinyume cha fikira za wengi katika nyakati zao. Wamevumilia udhalimu wa kisiasa, wa kidini, na wa ubaguzi wa rangi, mara nyingi wakitoa uhai wao kwa ajili ya madhumuni yao.

WAKRISTO wa mapema walikuwa wenye moyo mkuu hasa. Wakati wa ile minyanyaso mibaya ya karne tatu za kwanza, wengi wao waliuawa na Waroma wapagani kwa sababu ya kukataa kumwabudu maliki. Nyakati nyingine, madhabahu ilijengwa katika uwanja wa michezo. Ili kupata uhuru wao, Wakristo walihitaji tu kuchoma kiasi kidogo sana cha uvumba kuonyesha utambuzi wa hali ya kimungu ya maliki. Hata hivyo, ni wachache walioacha imani yao. Walio wengi walipendelea kufa badala ya kukana imani yao.

Katika nyakati za kisasa, Mashahidi wa Yehova wa Kikristo huchukua msimamo uo huo kwa habari ya kutokuwamo kwa kisiasa. Kwa kielelezo, msimamo wao imara walipokabili Unazi waweza kuthibitishwa katika rekodi za kihistoria. Kabla ya, na wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, karibu robo ya Mashahidi Wajerumani walipoteza uhai wao, hasa katika kambi za mateso, kwa sababu waliendelea kutokuwamo nao walikataa kusema “Heil Hitler.” Watoto wachanga walitenganishwa kwa nguvu kutoka kwa wazazi wao Mashahidi. Ujapokuwa mbano huo, vijana waliendelea kuwa imara nao wakakataa kuchafuliwa na mafundisho yasiyo ya kimaandiko ambayo wengine walijaribu kuwalazimisha wakubali.

Kusalimu Bendera

Kwa ujumla Mashahidi wa Yehova si shabaha ya mnyanyaso mkali wa jinsi hiyo leo. Hata hivyo, nyakati nyingine kuelewa vibaya hutokea kwa sababu ya uamuzi wenye kudhamiria wa Mashahidi wachanga wa kutoshiriki katika sherehe za kizalendo kama vile kusalimu bendera.

“Rudishieni Kaisari vilivyo vya Kaisari—na Mungu vilivyo vya Mungu”—Mathayo 22:21, Jerusalem Bible

Watoto wa Mashahidi wa Yehova hufundishwa wasizuie wengine kusalimu bendera; hilo ni jambo la kuamuliwa na kila mtu mmoja-mmoja. Hata hivyo, msimamo wa Mashahidi wenyewe ni imara: Wao hawasalimu bendera ya taifa lolote. Hilo kwa hakika halina nia ya kuonyesha ukosefu wa staha. Wao huistahi bendera ya nchi yoyote wanamoishi, nao huonyesha staha hiyo kwa kutii sheria za nchi hiyo. Hawashiriki kamwe katika aina yoyote ya utendaji wa kupinga serikali. Kwa kweli, Mashahidi huamini kwamba serikali za binadamu zilizopo hufanyiza “mpango wa Mungu” ambao yeye ameruhusu uweko. Kwa hiyo wao hujiona kuwa chini ya amri ya kimungu ya kulipa kodi na kustahi “mamlaka [hizo] zilizo kubwa.” (Warumi 13:1-7, NW) Hilo lapatana na taarifa maarufu ya Kristo: “Rudishieni Kaisari vilivyo vya Kaisari—na Mungu vilivyo vya Mungu.”—Mathayo 22:21, Jerusalem Bible ya Katoliki.

‘Lakini, kwa nini,’ huenda wengine wakauliza, ‘Mashahidi wa Yehova hawaiheshimu bendera kwa kuisalimu?’ Ni kwa sababu wao huona kusalimu bendera kuwa tendo la ibada, na ibada ni ya Mungu; hawawezi kwa kudhamiria kuabudu yeyote au chochote isipokuwa Mungu. (Mathayo 4:10; Matendo 5:29) Kwa hiyo, wao huthamini wakati waelimishaji wanapostahi sadikisho hili na kuruhusu watoto Mashahidi wafuate itikadi zao.

Haishangazi kwamba si Mashahidi wa Yehova peke yao wanaoamini kwamba kusalimu bendera kuna uhusiano na ibada, kama vile maelezo yafuatayo yaonyeshavyo:

“Bendera za mapema karibu zilikuwa za aina ya kidini kabisa. . . . Msaada wa dini ulikuwa daima ukitafutwa ili kuzipa utakatifu bendera za kitaifa.” (Italiki ni zetu.)—Encyclopædia Britannica.

“Bendera ni takatifu, kama vile msalaba. . . . Kanuni na amri zinazohusu mtazamo wa binadamu kuelekea viwango vya kitaifa hutumia maneno yenye nguvu na yaliyo dhahiri, kama vile, ‘Utumishi kwa Bendera,’ . . . ‘Kicho kwa Bendera,’ ‘Ujitoaji kwa Bendera.’” (Italiki ni zetu.)—The Encyclopedia Americana.

“Wakristo walikataa . . . kutolea dhabihu roho ya kimungu ya maliki [Mroma]—karibu na vile leo kukataa kusalimu bendera au kurudia kiapo cha uaminifu wa kiraia.”—Those About to Die (1958), cha Daniel P. Mannix, ukurasa 135.

Vijana Waebrania watatu walikataa kuinamia sanamu iliyojengwa na mfalme Mbabiloni Nebukadreza

Tena, Mashahidi wa Yehova hawana nia ya kutostahi serikali yoyote wala watawala wayo kwa kukataa kusalimu bendera. Ni kwamba tu, hawatainamia wala kusalimu sanamu inayowakilisha Serikali katika tendo lolote la ibada. Wanaona hilo kuwa sawa na msimamo uliochukuliwa katika nyakati za Biblia na vijana Waebrania watatu waliokataa kuinamia ile sanamu iliyojengwa katika uwanda wa Dura na mfalme Mbabiloni Nebukadreza. (Danieli, sura ya 3) Kwa hiyo basi, ingawa wengine husalimu na kuapa uaminifu wa kiraia, watoto wa Mashahidi wa Yehova wanafundishwa kufuata dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia. Hivyo, kwa ukimya na kwa staha wao huepuka kushiriki. Kwa sababu zizo hizo, watoto Mashahidi huchagua kutoshiriki wakati nyimbo za kitaifa zinapoimbwa au kupigwa.

Haki ya Wazazi

Siku hizi, nchi zilizo nyingi hustahi haki ya wazazi ya kuwapa watoto wao maagizo ya kidini kwa kupatana na masadikisho yao. Dini zote huunga mkono haki hiyo, kama vile ionyeshwavyo na sheria iliyo halali bado katika Kanisa Katoliki: “Wakiwa wamewapa watoto wao uhai, wazazi wako chini ya ule wajibu imara wa kuwaelimisha, nao wana haki ya kufanya hivyo; hiyo ndiyo sababu ni lazima hasa waandalie watoto wao elimu ya Kikristo kulingana na fundisho la Kanisa.”—Sheria 226.

Watoto wanatiwa moyo wapendezwe na wengine

Mashahidi wa Yehova hawaombi jambo jingine zaidi. Wakiwa wazazi wenye kujali, wao hujaribu kukaza kikiki kanuni za Kikristo zilizo za kweli katika watoto wao na kukaza ndani yao upendo kwa jirani na staha kwa mali za watu wengine. Wao hutamani kufuata lile shauri ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo katika Efeso: “Wazazi, msiwatende watoto wenu kwa njia ya kuwakasirisha. Badala ya hivyo, waleeni kwa nidhamu na maagizo ya Kikristo.”—Waefeso 6:4, Today’s English Version.

Nyumba Zilizogawanyika Kidini

Katika familia fulani, mzazi mmoja tu ni Shahidi wa Yehova. Katika hali ya jinsi hiyo, mzazi Shahidi anatiwa moyo atambue haki ya yule mzazi ambaye si Shahidi ya kuagiza pia watoto kulingana na masadikisho yake ya kidini. Watoto wanaofunuliwa kwa maoni tofauti ya kidini hupatwa na madhara machache, ikiwa kuna yoyote. * Kwa kweli, ni lazima watoto wote wachague ni dini gani watakayofuata. Kwa asili, si vijana wote wanaochagua kufuata kanuni za kidini za wazazi wao, wawe ni Mashahidi wa Yehova au la.

Haki ya Watoto ya Kuwa na Uhuru wa Dhamiri

Wapaswa kujua pia kwamba Mashahidi wa Yehova huiona dhamiri ya Kikristo ya mtu mmoja-mmoja kuwa ya maana sana. (Warumi, sura ya 14) Kanuni juu ya Haki za Mtoto, iliyokubaliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa katika 1989, ilitambua haki ya mtoto ya kuwa na “uhuru wa fikira, dhamiri na dini” na haki ya “kueleza maoni yake kwa uhuru na maoni hayo kufikiriwa ifaavyo katika jambo lolote au taratibu yoyote inayomwathiri mtoto huyo.”

Hakuna watoto wawili walio sawasawa kabisa. Kwa hiyo, waweza kutazamia ifaavyo tofauti fulani katika maamuzi ambayo Mashahidi wachanga au wanafunzi wengine wanafanya kwa habari ya utendaji na migawo fulani shuleni. Twatumaini kwamba wewe wakubaliana pia na kanuni ya uhuru wa dhamiri.

^ fu. 18 Kuhusu watoto wa ndoa zenye dini tofauti, Steven Carr Reuben, Ph.D., katika kitabu chake Raising Jewish Children in a Contemporary World, aonelea hivi: “Watoto hufadhaika wakati wazazi wanapoishi maisha ya kujikana, ya kufadhaika, ya kisiri, na ya kuepuka masuala ya kidini. Wazazi wanapokuwa wazi, wanyoofu, dhahiri juu ya itikadi, kanuni, na njia zao wenyewe za kusherehekea, watoto hukua wakiwa na ile aina ya usalama na hisi ya kuwa wao ni wa maana katika mambo ya kidini ambayo ni ya maana sana kwa habari ya ukuzi wa hali yao ya ujumla ya kujistahi na kujua mahali pao ulimwenguni.”