Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusudi la Broshua Hii

Kusudi la Broshua Hii

MWANAFALSAFA Mholanzi Spinoza aliandika hivi: “Nimejaribu kutoyacheka matendo ya binadamu, kutoyatolea machozi, wala kutoyachukia, bali kuyaelewa.” Ukiwa mwelimishaji, wewe hukabili ugumu wa kujaribu kuelewa maoni, malezi, na masadikisho ya wanafunzi unaowatunza, kutia na wanafunzi ambao ni watoto wa Mashahidi wa Yehova. Nyakati nyingine, wanafunzi hao huenda wakachukua msimamo ambao waonekana si wa kawaida juu ya masuala fulani. Lakini inapokuwa wazi kwamba matendo hayo yatokana na masadikisho ya mwanafunzi ya kidini na ya kiadili, yanastahili uangalifu wako. Broshua hii imetolewa na Watch Tower Bible and Tract Society (shirika la utangazaji la Mashahidi wa Yehova) na imekusudiwa kukusaidia uwaelewe vizuri zaidi wanafunzi Mashahidi. Twatumaini utachukua wakati kuisoma kwa uangalifu.

Kuelewa itikadi za kidini za mtu mwingine hakutaki kwamba uzikubali au uzifuate, na kumjulisha mtu si kumgeuza imani. Broshua hii haijaribu kukulazimisha wewe wala wanafunzi wako kukubali maoni fulani ya kidini. Tamaa yetu ni kukujulisha tu kanuni na itikadi ambazo baadhi ya wanafunzi wako wanafundishwa na wazazi wao ili iwe rahisi kwako kuwaelewa watoto Mashahidi na pia kushirikiana nao. Bila shaka, yale ambayo watoto wanafundishwa na yale wanayofanya hayapatani sikuzote, kwa kuwa kila mtoto anajifunza kusitawisha dhamiri yake mwenyewe.

Kama vile wazazi walio wengi, Mashahidi wa Yehova hutaka watoto wao wanufaike kikamili na elimu yao. Kwa kusudi hilo, wao huwafundisha watoto wao washirikiane na walimu wao. Kisha, wazazi Mashahidi na watoto wao huthamini wakati waelimishaji wanapowatendea kwa uelewevu na staha.

Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wanaojulikana ulimwenguni pote. Hata hivyo nyakati nyingine watu huwaelewa vibaya. Kwa hiyo, tumaini letu ni kwamba broshua hii itakusaidia uwaelewe vizuri zaidi watoto Mashahidi unaowatunza. Hasa, twatumaini utaona ni kwa nini, katika hali fulani hususa, huenda wakadai haki ya kuwa tofauti.