Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Programu za Elimu

Programu za Elimu
  • Programu za Elimu

  • Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa ajili ya kazi yao ya elimu ya Biblia.

    KWA SABABU ya wao kuiona kazi yao ya elimu ya Biblia kuwa ya maana sana, huenda wengine wakafikiri kwamba hawapendezwi na elimu ya kilimwengu. Lakini sivyo. Ili kufundisha wengine, lazima mwalimu ajifunze kwanza, na hilo lataka mazoezi na maagizo yafaayo. Kwa hiyo zaidi ya kutumia ifaavyo elimu ya kilimwengu, Mashahidi wa Yehova wamenufaika kwa miaka mingi na programu za elimu na shule mbalimbali zinazoendeshwa na Watch Tower Society. Hizi zimewasaidia Mashahidi na wengine wajiboreshe kiakili, kiadili, na kiroho.

    Kwa kielelezo, katika nchi nyingi Mashahidi wamekabili ugumu wa pekee—jinsi ya kufundisha watu ambao wamekuwa na fursa ndogo au hawajawa na fursa yoyote ya kupokea elimu ifaayo na hivyo hawajui jinsi ya kusoma au kuandika. Ili kutimiza uhitaji huo, Watch Tower Society imepanga programu za kufundisha watu kusoma na kuandika.

    Mathalani, katika Nigeria madarasa ya kufundisha watu kusoma na kuandika yameendeshwa na Mashahidi wa Yehova tangu 1949. Kupitia madarasa kama hayo, makumi ya maelfu nchini Nigeria wamejifunza kusoma. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia zaidi ya 90 ya Mashahidi wa Yehova katika Nigeria walijua kusoma na kuandika, wakilinganishwa na asilimia isiyozidi 50 ya watu wengine wa nchi hiyo. Katika Mexico, Mashahidi wa Yehova wameendesha madarasa ya kufundisha watu kusoma na kuandika tangu 1946. Katika mwaka mmoja, watu zaidi ya 6,500 walifundishwa kusoma na kuandika. Kufikia sasa, tayari watu zaidi ya 100,000 wamesaidiwa kujua kusoma na kuandika. Madarasa ya kufundisha watu kusoma na kuandika yamepangwa pia katika nchi nyingine nyingi, kama vile Bolivia, Kamerun, Nepal, na Zambia. Mashahidi wa Yehova wamechapisha nakala zaidi ya millioni saba za broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika, katika lugha zaidi ya 100.

    Mara nyingi programu hizo za kufundisha watu kusoma na kuandika zimepewa utambuzi na wenye mamlaka wa elimu katika nchi ambako zimeendeshwa. Kwa kielelezo, katika Mexico mfanyakazi mmoja wa serikali aliandika hivi: “Nashukuru kwa ajili ya ushirikiano wenu, na kwa niaba ya serikali ninawapitishia hongera yao yenye moyo mweupe sana kwa ajili ya kazi yenu bora yenye maendeleo kwa manufaa ya watu katika kuleta nuru ya ujuzi kwa wale wasiojua kusoma na kuandika. . . . Nawatakia mafanikio katika kazi yenu ya elimu.”

    Mazoezi ya Ziada

    Wanafunzi hupokea mazoezi katika usomaji na usemaji wa hadharani

    Kwa sababu wao huiona kazi yao ya elimu ya Biblia kuwa ya maana sana, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuboresha uwezo wao wa kueleza wengine juu ya mafundisho ya Biblia. Kwa mfano, katika kila kutaniko, zaidi ya makutaniko 119,000 ulimwenguni pote, wanafunzi hupokea mazoezi katika stadi za usomaji na usemaji wa hadharani. Hata wale wachanga zaidi, mara wanapojua jinsi ya kusoma, waweza kujiandikisha na kupokea mazoezi hayo, ambayo huthibitika kuwa yenye mafaa kwao pia katika mambo mengine, na pia katika elimu yao ya kilimwengu. Waelimishaji wengi wamesema kwamba wanafunzi Mashahidi huelekea kujieleza wenyewe vizuri sana.

    Kusoma hutiwa moyo sana katika makutaniko yao, na kila familia hutiwa moyo vilevile kuwa na maktaba ya familia yenye vichapo vingi mbalimbali

    Kwa kuongezea, kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova linatiwa moyo liwe na maktaba yenye misaada ya kujifunza Biblia, kamusi, na vitabu vingine vya marejezo, katika Jumba la Ufalme lalo, au mahali palo pa kukutania. Maktaba hiyo inaweza kutumiwa na wote wanaohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Kusoma hutiwa moyo sana katika makutaniko yao, na kila familia hutiwa moyo vilevile kuwa na maktaba ya familia yenye vichapo vingi mbalimbali ili kutimiza mahitaji ya watoto na ya watu wazima.

    Mazoezi ya Kiwango cha Juu

    Watch Tower Society huendesha pia shule za kuzoeza wamishonari wa jinsia zote mbili, na pia shule za kuzoeza wanaume walio na madaraka ya kihuduma katika makutaniko ya mahali-mahali. Shule hizo ni uthibitisho zaidi wa kwamba Mashahidi wa Yehova huiona elimu kuwa ya maana sana.