Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ugumu wa Utofautiano wa Kidini

Ugumu wa Utofautiano wa Kidini

Ukiwa mwelimishaji, wewe wakabili ugumu ambao waelimishaji katika karne zilizotangulia walikabili mara haba—utofautiano wa kidini.

MUDA wote wa Enzi za Kati, kwa kawaida raia wa nchi ileile walifuata dini ileile. Karibuni zaidi kufikia mwisho wa karne ya 19, Ulaya ilijua dini chache tu zilizo kuu: Ukatoliki na Uprotestanti katika magharibi, Uorthodoksi na Uislamu katika mashariki, na Dini ya Kiyahudi. Bila shaka, utofautiano wa kidini ni jambo la kawaida zaidi leo katika Ulaya na kotekote ulimwenguni. Dini zisizojulikana zimeanzishwa, ama kwa kufuatwa na baadhi ya wenyeji wenyewe wa nchi ama kwa kuletwa na wahamiaji na wakimbizi.

Hivyo, leo katika nchi kama vile Australia, Uingereza, Ufaransa, Ujerumani, na Marekani, twapata Waislamu, Wabuddha, na Wahindu wengi. Wakati uleule, Mashahidi wa Yehova, wakiwa Wakristo, wanahudumu kwa bidii katika nchi zaidi ya 239. Katika kila moja ya nchi 14, washiriki wao watendaji wafikia idadi ya zaidi ya 150,000.—Ona sanduku, “ Mashahidi wa Yehova—Dini ya Ulimwenguni Pote.”

Utofautiano wa mazoea ya kidini ya mahali-mahali waweza kutokeza ugumu kwa mwelimishaji. Kwa kielelezo, huenda maswali fulani ya maana yakatokezwa kuhusu sherehe zinazopendwa na wengi: Je, kila mwanafunzi alazimishwe kufuata miadhimisho yote—awe yeye ni wa dini gani? Huenda walio wengi wasione ubaya wowote katika sherehe hizo. Hata hivyo, je, maoni ya familia zilizo washiriki wa kikundi kidogo cha kidini hayapasi kustahiwa pia? Na kuna jambo jingine pia la kufikiriwa: Katika nchi ambazo sheria yatenganisha dini na mambo ya Serikali na mafundisho ya kidini hayatiwi ndani ya utaratibu wa masomo, je, wengine wasingeliona kuwa jambo lisilopatana kufanya sherehe hizo kuwa za lazima shuleni?

Siku za Kuzaliwa

Kutoelewana kwaweza hata kutokea kuhusiana na sherehe zinazoonekana kuwa na uhusiano mdogo wa kidini ikiwa kuna wowote. Hilo ni kweli kuhusu siku za kuzaliwa, zinazosherehekewa katika shule nyingi. Ingawa Mashahidi wa Yehova hustahi haki za wengine za kusherehekea siku za kuzaliwa, bila shaka wewe wajua vema kwamba wao huchagua kutoshiriki katika sherehe hizo. Lakini labda hujui sababu kwa nini wao na watoto wao wameamua kutoshiriki katika sherehe hizi.

Le livre des religions (Kitabu cha Dini Mbalimbali), ambayo ni ensaiklopedia iliyogawanywa sana Ufaransa, yaita desturi hii sherehe na yaiorodhesha miongoni mwa “mazoea ya kilimwengu.” Ingawa zaonwa leo kuwa desturi ya kilimwengu isiyodhuru, kwa kweli sherehe za siku za kuzaliwa zilitokana na upagani.

The Encyclopedia Americana (Chapa ya 1991) yasema hivi: “Ulimwengu wa kale wa Misri, Ugiriki, Roma, na Uajemi ulisherehekea siku za kuzaliwa kwa miungu, wafalme, na wakuu.” Watungaji wa vitabu Ralph na Adelin Linton wafunua sababu ya msingi ya kufanya hivyo. Katika kitabu chao The Lore of Birthdays, wao waliandika hivi: “Mesopotamia na Misri, vyanzo vya ustaarabu, vilikuwa pia nchi za kwanza ambazo watu walikumbuka na kuheshimu siku za kuzaliwa kwao. Kuweka rekodi za siku ya kuzaliwa kulikuwa jambo la maana katika nyakati za kale kwa sababu hasa tarehe ya kuzaliwa ilikuwa muhimu kwa ajili ya kupigwa kwa falaki.” Uhusiano huo wa moja kwa moja na unajimu ni chanzo cha hangaiko kubwa kwa wowote ambao huepuka unajimu kwa sababu ya yale ambayo Biblia husema juu ya huo.—Isaya 47:13-15.

Basi, haishangazi tusomapo hivi katika The World Book Encyclopedia: “Wakristo wa mapema hawakusherehekea siku ya kuzaliwa Kwake [Kristo] kwa sababu waliiona sherehe ya kuzaliwa kwa mtu yeyote kuwa desturi ya wapagani.”—Buku 3, ukurasa 416.

Mashahidi hufurahia kuwa na nyakati nzuri wakiwa pamoja

Wakizingatia habari hiyo iliyo juu, Mashahidi wa Yehova huchagua kutoshiriki katika karamu za siku za kuzaliwa. Kwa hakika, kuzaliwa kwa mtoto ni jambo lenye furaha, lililo zuri ajabu. Kwa asili, wazazi wote hushangilia watoto wao wanapokua na kusitawi kila mwaka upitapo. Mashahidi wa Yehova hupata pia shangwe nyingi katika kuonyesha upendo wao kwa familia na rafiki zao kwa kutoa zawadi na kuwa na nyakati nzuri wakiwa pamoja. Hata hivyo, kwa sababu ya chanzo cha sherehe za siku za kuzaliwa, wao hupendelea kufanya hivyo katika nyakati nyinginezo muda wote wa mwaka.—Luka 15:22-25; Matendo 20:35.

Krismasi

Krismasi husherehekewa ulimwenguni pote, hata katika nchi nyingi zisizo za Kikristo. Kwa kuwa sikukuu hiyo inakubaliwa na dini zilizo nyingi za Jumuiya ya Wakristo, huenda ikaonekana kuwa jambo la kushangaza sana kwamba Mashahidi wa Yehova huchagua kutoisherehekea. Kwa nini ni hivyo?

Kama vile ensaiklopedia nyingi zisemavyo kwa wazi, siku ya kuzaliwa kwa Yesu iliwekwa bila kufuata kanuni yoyote kuwa Desemba 25 ili ilingane na sikukuu ya kipagani ya Kiroma. Ona taarifa zifuatazo zilizochukuliwa kutoka katika vitabu tofauti-tofauti vya marejezo:

“Tarehe ya kuzaliwa kwa Kristo haijulikani. Gospeli hazionyeshi wala siku wala mwezi.”—New Catholic Encyclopedia, Buku 3, ukurasa 656.

“[Sherehe ya] Saturnalia katika Roma ilitolea mfano desturi zilizo nyingi zenye furaha za wakati wa Krismasi.”—Encyclopædia of Religion and Ethics

“Nyingi kati ya desturi za Krismasi zinazoenea sasa katika Ulaya, au zilizorekodiwa kutoka nyakati zilizopita, si desturi za Kikristo zilizo za kweli, bali ni desturi za kipagani ambazo zimefuatwa au kuvumiliwa na Kanisa. . . . [Sherehe ya] Saturnalia katika Roma ilitolea mfano desturi zilizo nyingi zenye furaha za wakati wa Krismasi.”—Encyclopædia of Religion and Ethics (Edinburgh, 1910), iliyohaririwa na James Hastings, Buku 3, kurasa 608-609.

“Krismasi imesherehekewa mnamo Desemba 25 katika makanisa yote ya Kikristo tangu karne ya nne. Wakati huo, hiyo ilikuwa ni tarehe ya sikukuu ya kipagani iliyoitwa ‘Kuzaliwa (Kilatini, natale) kwa Jua,’ ya kusherehekea majira ya baridi kali ya upeo wa jua, kwa kuwa jua lilionekana kuzaliwa upya siku zilipoanza tena kuwa ndefu zaidi. Katika Roma, Kanisa lilianza kufuata desturi hii iliyopendwa sana . . . kwa kuipa maana mpya.”—Encyclopædia Universalis, 1968, (ya Kifaransa) Buku 19, ukurasa 1375.

“Ukuzi wa sikukuu ya Krismasi uliathiriwa na utofautiano wayo na sherehe za kipagani za Sol Invictus (Mithra). Kwa upande ule mwingine, Desemba 25, ikiwa ndiyo siku ya majira ya baridi kali ya upeo wa jua, ilionwa kuwa yafanana na ile nuru iliyotokea ghafula ulimwenguni kupitia Kristo, hivyo ule ufananisho wa Sol Invictus ukapitishwa kwa Kristo.”—Brockhaus Enzyklopädie, (ya Kijerumani) Buku 20, ukurasa 125.

Wanapojifunza mambo ya hakika juu ya Krismasi, wengine wameitikiaje? The Encyclopædia Britannica ilionelea hivi: “Katika 1644 warekebishaji wa kidini Waingereza walikataza kusiwe na sherehe yoyote wala ibada za kidini kupitia amri ya Bunge, kwa msingi wa kwamba [Krismasi] ilikuwa sikukuu ya kipagani, nao wakaamuru isherehekewe kwa kufunga. Charles wa 2 alianzisha tena sikukuu hiyo, lakini watu wa Scotland walishikamana na maoni ya Warekebishaji wa Kidini.” Wakristo wa mapema hawakusherehekea Krismasi, wala Mashahidi wa Yehova hawaisherehekei leo wala kushiriki katika utendaji mbalimbali unaoshirikishwa na Krismasi.

Hata hivyo, Biblia husema kwa upendeleo juu ya kutoa zawadi au kualika familia na marafiki kwa ajili ya mlo wenye shangwe kwenye pindi nyinginezo. Hiyo hutia moyo wazazi wazoeze watoto wao wawe na ukarimu wenye moyo mweupe, badala ya kutoa zawadi wanapotazamiwa tu kufanya hivyo kijamii. (Mathayo 6:2, 3) Watoto wa Mashahidi wa Yehova hufundishwa kuvumilia na kuwa wenye staha, na hilo latia ndani kutambua haki ya wengine ya kusherehekea Krismasi. Kisha, wao huthamini wakati uamuzi wao wa kutoshiriki katika sherehe za Krismasi unapostahiwa.

Sherehe Nyinginezo

Mashahidi wa Yehova huchukua msimamo uo huo kuelekea sikukuu nyinginezo za kidini au zinazohusiana na dini ambazo hutukia katika mwaka wa shule katika nchi mbalimbali, kama vile sikukuu za Juni katika Brazili, Epiphany katika Ufaransa, Carnival katika Ujerumani, Setsubun katika Japani, na Halloween katika Marekani. Kwa habari ya sherehe hizi au nyingine yoyote hususa isiyotajwa hapa, wazazi Mashahidi au watoto wao wangefurahi kwa hakika kujibu maswali yoyote ambayo huenda ukawa nayo.