Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kufanya Nini ili Nielewane na Mwalimu Wangu?

Ninaweza Kufanya Nini ili Nielewane na Mwalimu Wangu?

SURA YA 20

Ninaweza Kufanya Nini ili Nielewane na Mwalimu Wangu?

Andika jina la mwalimu unayempenda. ․․․․․

Kwa nini unampenda mwalimu huyo? ․․․․․

Andika jina la mwalimu ambaye unaona ni vigumu sana kuelewana naye. ․․․․․

UNAWEZA kuchagua rafiki zako, lakini hasa mwanzoni mwa maishani yako, huwezi kuchagua walimu wako. Huenda unawapenda wote. David, mwenye umri wa miaka 18, anasema: “Sikuwa na shida na walimu wangu. Niliwaheshimu, nao walinipenda.”

Kwa upande mwingine, huenda ukawa na mwalimu kama anayefafanuliwa na Sarah, wenye umri wa miaka 11. “Hana huruma hata kidogo. Nami simwelewi anapofundisha. Nyakati fulani hafafanui masomo vya kutosha, nyakati nyingine anaeleza mambo mengi kupita kiasi.” Ili uelewane na mwalimu wako, kwanza unahitaji kujua tatizo hususa ambalo unafikiri unakabili. Ukiisha kulijua, itakuwa rahisi kulishinda. Tia alama ya ✔ karibu na kisanduku (masanduku) hapa chini, au uandike sababu yako mwenyewe.

□ Nashindwa kumwelewa mwalimu wangu

□ Naamini ninastahili alama za juu zaidi

□ Nafikiri wengine wanapendelewa

□ Ninaadhibiwa bila sababu

□ Ninabaguliwa

□ Sababu nyingine ․․․․․

Unaweza kufanya nini? Hatua ya kwanza ni kutumia shauri la mtume Petro. Aliandika: “Nyinyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8) Ni nini kinachoweza kukuchochea uwe na hisia-mwenzi kumwelekea mwalimu unayemwona kuwa asiye na huruma? Fikiria mambo fulani ya hakika kuhusu walimu, yanayoweza kukusaidia.

Walimu wanaweza kukosea. Wana mapendezi, matatizo, na hata wanaweza kuonyesha upendeleo. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2) Brianna, mwenye umri wa miaka 19, anasema: “Mwalimu wangu wa hesabu hakuwa mwenye subira sana na mara nyingi angetupigia kelele. Kwa hiyo haikuwa rahisi kwetu kumheshimu.” Ni nini kilichochangia hali hiyo? “Nyakati zote kulikuwa na fujo darasani,” asema Brianna, “na wanafunzi walijiendesha vibaya ili tu kumuudhi mwalimu.”

Bila shaka ungependa mwalimu apuuze makosa na kupungukiwa kwako, hasa ikiwa umekuwa na mikazo mingi. Unaweza kumtendea vivyo hivyo mwalimu wako? Andika hapa kuhusu kisa cha karibuni shuleni na kile ambacho huenda kilichangia mwenendo fulani wa mwalimu wenu.

․․․․․

Walimu wanapendelea wanafunzi fulani. Fikiria matatizo ambayo walimu wenu wanakabili: Kati ya wanafunzi katika darasa lenu, ni wangapi wanaotaka kuwa darasani? Ni wangapi kati ya wale wanaotaka kuwa darasani walio tayari kukazia fikira somo moja kwa nusu saa au zaidi? Baadhi yao hata humtendea mwalimu isivyofaa kwa sababu ya hasira au mambo ambayo watu wengine wamefanya. Sasa wazia ungepewa kazi ya kufundisha wanafunzi wenzako 20, 30, au hata zaidi, tena somo lenyewe ni somo ambalo wengi wao hawalipendi. Je, hungependezwa na wanaoonekana wanapendezwa?

Ni kweli kwamba huenda ukaudhika unapoona upendeleo ulio wazi. Natasha anasema hivi kuhusu mmoja wa walimu wake: “Alikuwa akiweka wakati ambapo sote tulipaswa kukamilisha kazi kufikia wakati huo, lakini sikuzote alikuwa akiwaongezea muda wachezaji wa mpira tu, na si mwingine yeyote. Alikuwa kocha msaidizi wa timu ya mpira.” Jambo kama hilo likikupata, jiulize, ‘Mahitaji yangu ya kielimu yanapuuzwa?’ Ikiwa sivyo, kwa nini niudhike au niwe na wivu?

Andika hapa kile unachoweza kufanya ili kumwonyesha mwalimu wako waziwazi kwamba unapendezwa na mambo anayofundisha.

․․․․․

Walimu hawawaelewi wanafunzi. Nyakati nyingine, kutofautiana au kutoelewana kwa aina fulani kunaweza kumfanya mwalimu awe na maoni mabaya kukuelekea. Kuuliza maswali kwaweza kuonwa kuwa uasi, au kusema jambo lenye kuchekesha kwaweza kuonwa kama kukosa heshima au ujinga.

Ufanye nini usipoeleweka vizuri? Biblia husema: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” (Waroma 12:17, 18) Basi, jaribu kutomkasirisha mwalimu wako. Epuka mabishano yasiyo ya lazima. Usimpe mwalimu wako sababu za kulalamika. Jaribu kuwa mwenye urafiki. ‘Urafiki? Na mwalimu?’ huenda ukauliza. Ndiyo, onyesha adabu kwa kumsalimu mwalimu kwa heshima mnapokutana. Ukiendelea kumheshimu—hata tabasamu ya mara kwa mara—huenda akabadili maoni yake kukuelekea.—Waroma 12:20, 21.

Kwa mfano, Ken, alikuwa na walimu ambao mara nyingi walimwelewa vibaya. Anasema: “Mimi ni mwenye haya sana na singeweza kuzungumza na walimu wangu.” Alishughulikia tatizo hilo jinsi gani? “Mwishowe niligundua kwamba mara nyingi, walimu wangu walitaka kunisaidia. Kwa hiyo, nikaazimia kuwajua kibinafsi walimu wangu wote. Nilipofanya hivyo, alama zangu zilianza kuwa bora.”

Ni kweli kwamba nyakati nyingine hata tabia nzuri na kuzungumza kwa heshima bado hakutamfanya mwalimu akupende. Lakini uwe na subira. Mfalme Sulemani aliandika: “Kwa subira kiongozi [au mwalimu] hushawishiwa, na ulimi wa upole unaweza kuvunja mfupa.” (Methali 25:15) Uwe mtulivu na uzungumze kwa upole unapotendewa isivyo haki. Huenda mwalimu wako akabadili maoni yake.—Methali 15:1.

Ikiwa mwalimu wako hakuelewi au anakutendea isivyo haki, kwa kawaida wewe hufanya nini?

․․․․․

Badala yake, ingekuwa afadhali kufanya nini?

․․․․․

Kutatua Matatizo Hususa

Kumwelewa mwalimu wako ni mwanzo tu. Unaweza kufanya nini ili kutatua tatizo fulani hususa? Kwa mfano, huenda ukashughulikia jinsi gani malalamishi yafuatayo?

Nastahili alama bora. “Sikuzote nilipata alama za juu,” asema Katrina. “Lakini mwaka mmoja mwalimu wangu wa somo la sayansi alinipa alama za chini sana. Nilistahili alama bora. Wazazi wangu wakazungumza na mkuu wa shule. Hata hivyo, aliboresha alama zangu kidogo tu, hivyo bado nilikasirika sana.” Ukikabili tatizo kama hilo, usitangaze vita dhidi ya mwalimu wako. Badala yake, jifunze kutoka kwa Nathani anayetajwa katika Biblia. Alipewa kazi ngumu ya kufunua kosa zito la Mfalme Daudi. Nathani hakuingia kijeuri katika nyumba ya kifalme na kuanza tu kumtolea mashtaka, badala yake alizungumza na Daudi kwa busara.—2 Samweli 12:1-7.

Vivyo hivyo, unaweza kuzungumza na mwalimu wako kwa unyenyekevu na utulivu. Ukimkasirikia au kumlaumu mwalimu wako kwamba hajui chochote, hamtapatana. Jaribu kuzungumza naye kama mtu mzima. Anza kwa kumwomba mwalimu wako akueleze jinsi unavyoweza kuboresha alama zako. Sulemani aliandika: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” (Methali 18:13) Baada ya kusikiliza, unaweza kutaja mahali ambapo unaona makosa yalifanywa. Hata kama hatabadilisha alama zako, huenda ukomavu wako ukamvutia mwalimu.

Naona kwamba mwalimu wangu ananichukia. Mfikirie Rachel. Alikuwa akipata alama za juu shuleni. Kisha alipofika darasa la 7, mambo yakabadilika. Anasema: “Mwalimu wangu alijaribu sana kuniangusha katika somo lake.” Tatizo lilikuwa nini? Mwalimu alimweleza waziwazi Rachel na mama yake kwamba hapendi dini yao.

Ikawaje? Rachel anasema: “Kila wakati ilipoonekana wazi kwamba mwalimu alichochewa na chuki alipokuwa akikagua kazi yangu, Mama angeandamana nami hadi shuleni na kuzungumza naye kuhusu jambo hilo. Mwishowe, aliacha kunihangaisha.” Ikiwa una tatizo kama hilo, zungumza na wazazi wako. Bila shaka, watapenda kuzungumza na mwalimu na ikiwezekana na mamlaka ya shule ili kutafuta utatuzi.

Fikiria Siku za Baadaye

Ni kweli matatizo mengine hayatatatuliwa kwa urahisi. Nyakati nyingine, utalazimika kuvumilia. “Mmoja wa walimu wetu alikuwa na maoni mabaya kuelekea wanafunzi,” asema Tanya. “Mara nyingi alitutusi, na kutuita wapumbavu. Mwanzoni nililia, lakini baadaye nikamzoea na kutomchukulia kwa uzito. Nilikazia fikira kazi yangu na kujishughulisha na masomo anapofundisha. Kwa kufanya hivyo hakunisumbua sana, na nilikuwa kati ya wachache waliopata alama nzuri. Baada ya miaka miwili, mwalimu huyo alifutwa kazi.”

Jifunze kushughulika na mwalimu mgumu, nawe utapata ustadi wa maana katika maisha yako, ustadi utakaokusaidia utakapokuwa ukifanya kazi chini ya tajiri mgumu. Pia, utajifunza kuwathamini walimu wazuri wanapopatikana.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Unaona ni kama huna wakati wa kutosha? Jifunze jinsi ya kuona saa kuwa rafiki, wala si adui.

ANDIKO MUHIMU

“Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

PENDEKEZO

Ikiwa unaona kwamba mwalimu wenu hafundishi kwa njia yenye kupendeza, kazia fikira somo lenyewe, badala ya kumkazia fikira mwalimu mwenyewe. Andika habari, uliza habari zaidi kwa heshima, na uwe na maoni yanayofaa kuhusu somo lenyewe. Ukiwa na maoni yanayofaa, wengine watafuata mfano wako.

JE, WAJUA . . . ?

Huenda mwalimu wako amewafundisha wanafunzi wa madarasa mengine masomo yaleyale mara kadhaa au hata mamia ya mara. Kwa hiyo, yawezekana kwamba si rahisi kwake kufundisha kwa shauku jinsi alivyokuwa akifundisha mwanzoni alipoanza kazi ya ualimu.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili kupendezwa na somo lenye kuchosha, nita ․․․․․

Nikiona kwamba mwalimu wangu ananitendea isivyo haki, nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kukazia fikira somo badala ya mwalimu kuna faida gani?

● Ni kwa njia gani maoni yako kuhusu somo fulani yanaweza kumfanya mwalimu awe na maoni mazuri au mabaya kukuelekea?

[Blabu katika ukurasa wa 146]

“Nilijitahidi sana kufanya urafiki na walimu wangu wote. Ninajua majina yao, na ninapowaona barabarani, mimi huzungumza nao kwa dakika chache.”—Carmen

[Picha katika ukurasa wa 145]

Walimu ni kama daraja la kukuvusha kutoka ujinga na kukufikisha kwenye ujuzi, hata hivyo, lazima wewe mwenyewe uvuke