Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?

Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?

SURA YA 32

Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?

Kila mwaka, mamilioni ya watu hubakwa au kutendewa vibaya kingono, na kulingana na uchunguzi, vijana ndio wanaolengwa hasa. Kwa mfano, inakadiriwa kwamba nchini Marekani, karibu nusu ya watu wote wanaotendewa vibaya kingono wako chini ya umri wa miaka 18. Kwa sababu ya kuenea kwa uovu huo, ni muhimu kuchunguza habari hii.

“Alinishika na kabla ya kujua kilichokuwa kinaendelea, akaniangusha chini. Nilijaribu kila niwezalo kumzuia. Nilivuta mkebe uliokuwa na pilipili lakini akaugonga kutoka mkononi mwangu. Nilijaribu kupiga mayowe, lakini wapi. Nilimsukuma, nikatupa mateke, nikampiga ngumi, na kumkwaruza. Ndipo nikasikia kisu kikinidunga. Mwili wangu wote ukadhoofika kabisa.”—Annette.

WASHAMBULIAJI wa kingono ni wengi leo, na mara nyingi wanawalenga vijana. Vijana fulani, kama Annette, wanatendewa vibaya na watu wasiowajua. Wengine wanashambuliwa na jirani. Ndivyo ilivyokuwa katika kisa cha Natalie, ambaye alipokuwa na umri wa miaka 10 tu, alitendewa vibaya kingono na kijana aliyekuwa akiishi karibu na kwao. Anasema: “Niliogopa na kuona haya sana hivi kwamba mwanzoni sikumwambia yeyote.”

Vijana wengi wametendewa vibaya na mtu wa familia. “Nilipokuwa na umri wa kati ya miaka 5 na 12, nilitendewa vibaya kingono na baba yangu,” asema mwanamke anayeitwa Carmen. “Mwishowe nilizungumza naye kuhusu jambo hilo nilipokuwa na umri wa miaka 20. Aliomba msamaha, lakini miezi kadhaa baadaye, alinifukuza kutoka nyumbani.”

Inasikitisha sana kwamba leo, ni jambo la kawaida kutendewa vibaya kingono na jirani, rafiki, au mtu wa familia. * Hata hivyo, vijana wametendewa vibaya tangu zamani. Hata nyakati Biblia ilipokuwa ikiandikwa, mwenendo huo wenye kusikitisha ulikuwako. (Yoeli 3:3; Mathayo 2:16) Leo, tunaishi katika nyakati za hatari. Watu wengi hawana “upendo wa asili,” na ni kawaida wasichana (na hata wavulana) kutendewa vibaya kingono. (2 Timotheo 3:1-3) Ingawa hakuna tahadhari inayoweza kukuhakikishia usalama, kuna mengi unayoweza kufanya ili kujilinda. Fikiria mapendekezo yafuatayo:

Kuwa macho. Unapotembea, kuwa macho kujua kinachoendelea mbele yako, nyuma yako, upande huu na upande ule. Maeneo fulani ni hatari, hasa usiku. Ikiwezekana, epuka kabisa maeneo hayo au usitembee ukiwa peke yako.—Methali 27:12.

Epuka kueleweka vibaya. Epuka kuchezea hisia za wengine au kuvalia kwa njia inayowavutia kingono. Matendo kama hayo yanaweza kufanya watu wakuelewe kimakosa kwamba ungependa kufanya ngono, au huwezi kukataa nafasi ya kufanya hivyo ikitokea.—1 Timotheo 2:9, 10.

Zungumzia mipaka. Ikiwa mna uhusiano wa kimapenzi, zungumza na mwenzako kuhusu mwenendo unaofaa na usiofaa. * Baada ya kuweka mipaka, epuka hali zinazoweza kukuhatarisha.—Methali 13:10.

Usinyamaze. Hakuna ubaya kusema hivi kwa uthabiti, “Usifanye hivyo!” au “Usiniguse!” Usinyamaze eti kwa sababu unaogopa mpenzi wako atakuacha. Akivunja uhusiano wenu kwa sababu hiyo, basi hakufai! Isitoshe, unahitaji mwanamume anayeheshimu mwili wako na kanuni zako. *

Kuwa mwangalifu unapotumia Intaneti. Hupaswi kutoa habari za kibinafsi au kuweka picha zinazoonyesha mahali ulipo. * Ukipokea ujumbe unaozungumzia ngono waziwazi, kwa kawaida jibu bora ni kutojibu. Watu wengi wanaoshambulia kupitia Intaneti hukosa la kufanya wasipojibiwa.

Hatua hizo zinaweza kukusaidia usishambuliwe kwa urahisi. (Methali 22:3) Hata hivyo, jambo la hakika ni kwamba, huenda nyakati zote mambo yasiwe kama unavyotaka. Kwa mfano, huenda kila wakati isiwezekane kuwa na mwandamani au isiwezekane kuepuka maeneo hatari. Labda hata unaishi katika eneo hatari.

Huenda kutokana na hali yenye kusikitisha iliyokupata, unajua kwamba mambo mabaya yanaweza kutokea hata baada ya kujaribu sana kuepuka matatizo. Kama Annette, aliyetajwa mwanzoni, labda ulishambuliwa bila kutarajia na ukashindwa nguvu. Au kama Carmen, labda ulishambuliwa ukiwa mtoto, na kwa hiyo hukuwa na uwezo wa kuzuia hali hiyo, au hata hukuelewa kabisa yaliyokuwa yakitokea. Unaweza kushughulikia jinsi gani hisia za hatia ambazo mara nyingi huwasumbua watu ambao wamewahi kutendewa vibaya kingono?

Kupambana na Hisia za Hatia

Mpaka sasa Annette anapambana na hisia za hatia kuhusu mambo yaliyompata. “Najiona kuwa adui yangu mwenyewe,” anasema. “Naufikiria usiku huo tena na tena. Nahisi nilipaswa kujaribu zaidi kumzuia mtu huyo. Ukweli ni kwamba, baada ya kudungwa kisu, niliogopa sana. Sikuweza kufanya lolote, lakini nahisi kwamba nilipaswa kufanya jambo fulani.”

Natalie pia anapambana na hisia za hatia. Anasema: “Sikupaswa kumwamini mtu yeyote. Wazazi wetu walituamuru mimi na dada yangu tuwe tukicheza pamoja, lakini sikutii. Kwa hiyo, nahisi kwamba nilimpa jirani yangu nafasi ya kuniumiza. Mambo yaliyonipata yaliumiza familia yetu, nami najilaumu kwa kuwasababishia uchungu mwingi. Hilo linaniumiza hata zaidi.”

Unaweza kupambana jinsi gani na hatia ikiwa hisia zako ni kama za Annette au Natalie? Kwanza, kumbuka kwamba ikiwa ulilalwa kinguvu, hukutaka kufanya hivyo. Watu fulani hupunguza uzito wa kosa hilo kwa kusema kwamba ni kawaida kwa wanaume kufanya hivyo na kwamba wanaolalwa kinguvu ndio wenye kulaumiwa. Hata hivyo, hakuna mtu anayepaswa kulalwa kinguvu. Ikiwa ulitendewa uovu huo, huwezi kulaumiwa!

Ni kweli kwamba ni rahisi kusoma taarifa inayosema “huwezi kulaumiwa,” lakini si rahisi kuiamini. Wengine hawasemi kuhusu mambo yaliyotokea nao wanaumia kutokana na hisia za hatia, na hisia nyingine mbaya. Hata hivyo, kukaa kimya kunamsaidia nani—wewe au mshambuliaji wako? Unahitaji kuchukua hatua nyingine.

Sema Yaliyokupata

Biblia inasema kwamba Ayubu, yule mwanamume mwadilifu, akiwa amechanganyikiwa sana alisema: “Nitaonyesha hangaiko langu kujihusu mwenyewe. Nitasema kwa uchungu wa nafsi yangu!” (Ayubu 10:1) Utafaidika kwa kufanya hivyo pia. Kuzungumza na mtu ambaye unamtumaini kuhusu mambo yaliyokupata kunaweza kukusaidia kupambana na hali hiyo na kupata kitulizo kutokana na hisia zako zenye kuumiza.

Ikiwa wewe ni Mkristo, ni muhimu kuzungumza na mzee wa kutaniko kuhusu mambo yaliyokupata. Maneno yenye kufariji ya mchungaji mwenye upendo yatakuhakikishia kwamba kwa kulalwa kinguvu hutaonwa kuwa mchafu kutokana na dhambi ya mtu mwingine. Hivyo ndivyo Annette alivyotambua. Anasema: “Nilizungumza na rafiki yangu wa karibu, naye akanihimiza nizungumze na wazee wawili Wakristo katika kutaniko letu. Nafurahi nilifanya hivyo. Walizungumza nami mara kadhaa na kuniambia kwamba yaliyotokea hayakuwa makosa yangu. Sikufanya kosa lolote.”

Kuzungumza kuhusu mambo yaliyotokea na kueleza hisia zako kunaweza kukusaidia usilemewe na hasira na kinyongo. (Zaburi 37:8) Huenda pia kukakusaidia kupata kitulizo, labda kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi. Natalie aliona ukweli wa maneno hayo baada ya kuwaambia wazazi wake kuhusu jinsi alivyotendewa vibaya. Anasema: “Walinisaidia. Walinitia moyo kuzungumza, na hilo likanisaidia kutohuzunika sana na kuwa na hasira nyingi.” Pia, Natalie alipata faraja kwa kusali. Anasema: “Kuzungumza na Mungu kulinisaidia hasa nyakati ambazo niliona kwamba siwezi kuzungumza na mwanadamu. Ninaweza kuzungumza kwa uhuru ninaposali. Kufanya hivyo kunanipa amani ya kweli na utulivu.” *

Huenda wewe pia ukatambua kwamba kuna ‘wakati wa kupona.’ (Mhubiri 3:3) Tegemea marafiki wanaoweza kukusaidia ambao ni kama wazee Wakristo wanaofafanuliwa kuwa sawa na “mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua.” (Isaya 32:2) Jitunze kimwili na kihisia. Pumzika vya kutosha. Na zaidi ya yote, mtegemee Mungu wa faraja yote, Yehova, ambaye karibuni ataleta ulimwengu mpya ambamo “watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.”—Zaburi 37:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Visa fulani vinatokea wakati wa matembezi ya kimapenzi, ambapo msichana hulazimishwa kufanya ngono au anakubali baada ya kulishwa dawa za kulevya.

^ fu. 10 Pata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 4.

^ fu. 11 Bila shaka, shauri hilo linatumika pia ikiwa msichana anamlazimisha mvulana wafanye ngono.

^ fu. 12 Pata habari zaidi katika Buku la 2, Sura ya 11.

^ fu. 23 Nyakati nyingine watu ambao wametendewa vibaya wanashuka moyo sana. Katika hali kama hizo, huenda ikafaa kumwona daktari. Pata habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na hisia zenye kuumiza katika Sura ya 13 na 14 ya kitabu hiki.

ANDIKO MUHIMU

“Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na upendo wa asili, . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema.”—2 Timotheo 3:1-3.

PENDEKEZO

Ikiwa umewahi kutendewa vibaya kingono, hifadhi orodha ya maandiko yanayoweza kukufariji. Maandiko hayo yanaweza kutia ndani Zaburi 37:28; 46:1; 118:5-9; Methali 17:17; na Wafilipi 4:6, 7.

JE, WAJUA . . . ?

Nchini Marekani, zaidi ya asilimia 90 ya vijana wanaotendewa vibaya kingono wanawajua washambuliaji wao.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikihisi hatia kuhusu mambo yaliyotendeka nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Kuna faida gani kuzungumza na mtu fulani unapotendewa vibaya?

● Ni nini kinachoweza kukupata wewe na wengine usipozungumza kuhusu jambo hilo?

[Blabu katika ukurasa wa 232]

“Si rahisi kumwambia mtu kwamba umetendewa vibaya kingono, hata hivyo, ni vizuri kufanya hivyo. Kumwambia mtu kunakusaidia kuondolea mbali huzuni na hasira na kurudia hali yako ya kawaida.”—Natalie

[Sanduku katika ukurasa wa 230]

“Ikiwa Unanipenda . . . ”

Washambuliaji fulani hawawalazimishi wasichana wafanye ngono nao lakini kwa ujanja wanachezea hisia zao. Jinsi gani? Kwa kuwaambia maneno kama, “Kila mtu anafanya ngono,” “Hakuna atakayejua,” au, kama ilivyotajwa katika Sura ya 24 ya kitabu hiki, “Ikiwa unanipenda, utafanya ninavyokuambia.” Usidanganywe na mvulana anayejaribu kukufanya uamini kwamba ikiwa unampenda mtu lazima ufanye ngono naye. Ukweli ni kwamba, yeyote anayefikiria hivyo anataka tu kutosheleza tamaa yake. Hakujali wala hajali hali yako. Tofauti na mtu huyo, mwanamume mzuri atatanguliza faida zako na ataonyesha kwamba anashikamana na kanuni za maadili za Mungu. (1 Wakorintho 10:24) Mwanamume halisi hawatendei wasichana kama vyombo vya ngono. Badala yake, anawaona “wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.”—1 Timotheo 5:1, 2.

[Picha katika ukurasa wa 233]

Hisia zinazotokana na kutendewa vibaya ni nzito sana, huwezi kuzibeba peke yako. Kwa nini usitafute msaada kwa kuzungumza na mtu fulani?