Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Porojo Ina Ubaya Gani?

Porojo Ina Ubaya Gani?

SURA YA 12

Porojo Ina Ubaya Gani?

“Siku moja nilienda katika karamu. Kesho yake kukatokea uvumi kwamba nililala na mvulana fulani huko. Ulikuwa uwongo mtupu!”—Linda.

“Nyakati nyingine mimi husikia uvumi kwamba nina urafiki wa kimapenzi na mtu fulani, mtu ambaye hata simjui! Watu wengi wanaopiga porojo hawatafuti ukweli wa mambo.”—Mike.

POROJO inaweza kufanya maisha yako yaonekane kama sinema. “Karibu kila siku ninasikia porojo kunihusu,” anasema Amber mwenye umri wa miaka 19. “Kulikuwa na uvumi kwamba nina mimba, nimetoa mimba mara kadhaa, mimi ni mlanguzi wa dawa za kulevya, nami hutumia dawa za kulevya. Mbona watu waseme mambo kama hayo kunihusu? Sielewi hata kidogo!”

Mvulana au msichana mwenye nia mbaya anaweza kukuharibia sifa yako akitumia barua-pepe na ujumbe mfupi pasipo hata kufumbua kinywa chake. Uvumi mbaya sana unaweza kuenea haraka kwa kuandika maneno machache tu na kuyasambaza! Katika visa fulani, wengine wameanzisha tovuti (Web site) ili kumwaibisha mtu fulani. Kwa kawaida blogu kwenye Intaneti huwa na porojo chungu nzima ambazo mtu hangeweza kuzisema uso kwa uso.

Lakini je, sikuzote ni vibaya kuongea juu ya wengine? Je, kuna . . .

Porojo Nzuri?

Tia alama taarifa inayofuata, kuonyesha kama ni kweli au si kweli.

Hakuna porojo nzuri. □ Kweli □ Si kweli

Ni jibu gani lililo sahihi? Inategemea unavyoelewa neno “porojo.” Ikiwa ni mazungumzo ya kupisha wakati tu, basi kuna pindi inapofaa. Biblia inatuhimiza ‘tupendezwe na maisha ya wengine.’ (Wafilipi 2:4, New Century Version) Haimaanishi kwamba tujiingize katika mambo ambayo hayatuhusu. (1 Petro 4:15) Hata hivyo, mazungumzo ya kawaida hutusaidia kupata habari, kama vile, ni nani anayeoa au kuolewa, au ni nani aliyepata mtoto. Ukweli ni kwamba hatuwezi kusema tunawajali wengine ikiwa hatuzungumzi kamwe kuwahusu.

Pamoja na hayo, mazungumzo ya kawaida yanaweza kugeuka kwa urahisi na kuwa porojo mbaya. Kwa mfano, mtu akisema “Bob na Sue wanaweza kufaana sana katika ndoa” maneno hayo yanaweza kutiwa chumvi na kuwa “Bob na Sue wanachumbiana,” ijapokuwa Bob na Sue hawana habari hata kidogo. Huenda ukasema, ‘Ah si kitu!’ Lakini, ingekuwaje ikiwa maneno hayo yangesemwa kukuhusu?

Porojo kama hiyo ilienezwa kumhusu Julie, aliye na umri wa miaka 18, naye aliumia sana. Anasema: “Nilikasirika sana na kuanza kumshuku kila mtu.” Jane, mwenye umri wa miaka 19, alikuwa katika hali kama hiyo. “Nilianza kumwepuka mvulana ambaye ilisemekana tunachumbiana,” anasema huku akiongezea, “Sikupaswa kumtendea hivyo, alikuwa rafiki yangu, na kwa maoni yangu tunapaswa kuwa na uhuru wa kuzungumza pasipo mtu yeyote kuanzisha uvumi kutuhusu!”

Endesha Mazungumzo kwa Busara!

Unaweza kuongoza jinsi gani ulimi wako unaposhawishiwa kupiga porojo? Ili kujibu swali hilo, wazia ustadi unaohitajiwa ili kuendesha gari katika barabara yenye magari mengi. Bila kutarajiwa, hali fulani inaweza kukulazimu kutoka upande mmoja wa barabara hadi mwingine, kupisha gari lingine, au kusimama kabisa. Ukiwa macho, utaona kilicho mbele na kuchukua hatua inayohitajika.

Ndivyo ilivyo kuhusiana na mazungumzo pia. Kwa kawaida unaweza kujua iwapo mazungumzo yanaanza kuwa porojo yenye kudhuru. Hilo linapotukia, je, unaweza ‘kutoka upande huo wa barabara’? Usipofanya hivyo, tahadhari, porojo inaweza kutokeza madhara. Mike anaeleza hivi: “Bila kufikiri, nilisema kwamba msichana mmoja anapendezwa sana na wavulana, nazo habari hizo zikamfikia. Sitasahau kamwe uchungu aliokuwa nao alipozungumza nami, jinsi alivyoumizwa na maneno niliyosema. Ingawa tulitatua jambo hilo, ninasikitika ninapokumbuka kwamba nilimuumiza hivyo!”

Hakuna shaka kwamba maneno yanaweza kuumiza. Hata Biblia inasema “kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma.” (Methali 12:18) Ndiyo sababu unapaswa kupima maneno yako! Ni kweli kwamba baada ya mazungumzo kupamba moto ujasiri unahitajika ili kuyakatiza. Ni kama vile tu Carolyn mwenye miaka 17 anavyosema: “Unahitaji kuwa mwangalifu unasema nini. Ikiwa hujasikia jambo kutoka chanzo kinachotegemeka, huenda ukawa unaeneza uwongo.” Kwa hiyo, unaposikia mambo yanayoweza kugeuka na kuwa porojo yenye kudhuru, fuata shauri la Paulo la ‘kufanya iwe shabaha yako kuishi kwa utulivu na kukazia akili mambo yako mwenyewe.’—1 Wathesalonike 4:11.

Ni kwa njia gani unaweza kupendezwa na wengine na wakati uleule kukazia akili mambo yako mwenyewe? Kabla ya kusema jambo fulani juu ya mtu, jiulize: ‘Je, nina habari kamili? Kwa nini ninaeneza habari hiyo? Wengine watanionaje wakijua kwamba ninaeneza porojo?’ Swali hilo la mwisho ni la maana, kwa sababu kujulikana kuwa mweneza porojo kunafunua mengi zaidi kukuhusu wewe kuliko yule anayezungumziwa.

Porojo Ikienezwa Kukuhusu

Unaweza kufanya nini porojo ikienezwa kukuhusu? Andiko la Mhubiri 7:9 linasema hivi: “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako.” Badala yake, jaribu kuzuia hisia zako na kutochukua mambo kwa uzito kupita kiasi. Biblia inasema: “Usiweke moyoni mwako maneno yote ambayo huenda watu wakasema, . . . kwa maana moyo wako mwenyewe unajua vema kwamba hata mara nyingi wewe, naam hata wewe, umewalaani wengine.”—Mhubiri 7:21, 22.

Bila shaka, hakuna udhuru wa kueneza porojo yenye kudhuru. Hata hivyo, kujiachilia uongozwe na hisia kunaweza kukuharibia sifa kuliko porojo yenyewe! Kwa nini usiwe na maoni kama ya Renee? Anasema: “Kwa kawaida mimi huumia mtu anaposema jambo baya kunihusu, hata hivyo mimi hujaribu kudumisha usawaziko. Leo ni mimi, kesho ni mwingine au jambo lingine.” *

Basi, tenda kwa hekima kwa kubadili mazungumzo yanapoanza kuwa porojo yenye kudhuru. Na mambo mabaya yanaposemwa kukuhusu, onyesho ukomavu kwa kutoachilia hisia zikuongoze. Acha ujulikane kwa matendo yako mema. (1 Petro 2:12) Ukifanya hivyo, utadumisha uhusiano mzuri pamoja na wengine na kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Katika hali fulani, huenda likawa jambo la hekima kuzungumza kwa busara na mtu anayeeneza porojo kukuhusu. Hata hivyo, katika visa vingi, hakuna haja kwa sababu “upendo hufunika dhambi nyingi.”—1 Petro 4:8.

MAANDIKO MUHIMU

“Anayelinda kinywa chake anaitunza nafsi yake. Anayefungua wazi midomo yake —yeye atapata uharibifu.”—Methali 13:3.

PENDEKEZO

Mtu akianza kukusimulia porojo, unaweza kumwambia: “Sifurahii mazungumzo haya. Kwanza, hata mhusika mwenyewe hayuko hapa ajitetee.”

JE, WAJUA . . .?

Kusikiliza tu porojo kunaweza kukufanya uwe na hatia kwa kiasi fulani. Kumruhusu mpiga-porojo aendelee kukusimulia ni kama kuongeza kuni kwenye moto.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikishawishiwa kueneza porojo, nita ․․․․․

Watu wakisema mambo yanayoniumiza, nitashughulikia hali hiyo kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Ni mambo gani yanayofaa tunayoweza kuzungumza kuhusu wengine?

● Je, porojo imewahi kuenezwa juu yako, ikiwa ndivyo, ulijifunza nini kutokana na kisa hicho?

● Kueneza porojo juu ya wengine kunaweza kuharibu jinsi gani sifa yako?

[Blabu katika ukurasa wa 107]

“Nilijuta sana wakati ambapo mtu niliyeeneza porojo kumhusu alipokuja kuzungumza nami. Sikuwa na njia ya kukimbilia! Bila shaka nilijifunza kwamba ni afadhali kuzungumza na mtu moja kwa moja badala ya kumsengenya!’’—Paula

[Picha katika ukurasa wa 108]

Kama silaha hatari, porojo yenye kudhuru inayoweza kumuumiza na kumharibia mtu sifa