Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Ubaya Gani Kuwa na Urafiki wa Kimapenzi wa Siri?

Kuna Ubaya Gani Kuwa na Urafiki wa Kimapenzi wa Siri?

SURA YA 2

Kuna Ubaya Gani Kuwa na Urafiki wa Kimapenzi wa Siri?

Jessica alijikuta mashakani. Kijana mmoja darasani anayeitwa Jeremy alianza kupendezwa naye. “Alikuwa na sura nzuri sana,” Jessica anasema, “na marafiki wangu walisema kwamba sitapata kamwe mvulana mwingine mzuri kama huyo. Wasichana wengi walikuwa wamejaribu kuanzisha urafiki naye, lakini hakupendezwa nao. Alipendezwa na mimi tu.”

Muda si muda, Jeremy alimwomba Jessica wawe marafiki. Jessica alijibu kwamba kwa kuwa yeye ni Shahidi wa Yehova hangeruhusiwa kuanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye si wa dini yake. “Hata hivyo,” Jessica anasema, “Jeremy alikuwa na wazo lingine. Aliuliza, ‘Kwa nini tusiwe na urafiki bila wazazi wako kujua?’”

IKIWA mtu fulani ambaye wewe unavutiwa naye angependekeza muwe na urafiki wa aina hiyo, ungefanya nini? Huenda ukashangaa kujua kwamba Jessica alikubali wazo la Jeremy. “Nilisadiki kwamba tukiwa marafiki, ninaweza kumsaidia ajifunze kumpenda Yehova,” Jessica anasema. Matokeo yalikuwa nini? Tutaona baadaye. Kwanza, acheni tuone jinsi ambavyo wengine wameingia katika mtego wa kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri.

Kwa Nini Wanafanya Urafiki Wao Uwe Siri?

Kwa nini wengine huanzisha urafiki wa siri? Kijana anayeitwa David anasema hivi waziwazi: “Wanajua kwamba wazazi wao hawatakubali, kwa hiyo hawawaambii.” Jane anaeleza sababu nyingine. Anasema: “Urafiki wa kimapenzi wa siri ni ishara ya uasi. Ukiona kwamba hutendewi kama mtu mzima, unaamua kufanya jambo lolote unalotaka bila kuwaambia wazazi wako.”

Je, unaweza kufikiria sababu nyingine zinazowafanya wengine wawe na urafiki wa kimapenzi wa siri? Ikiwa unajua, ziorodheshe hapa chini.

․․․․․

Bila shaka, unajua kwamba Biblia inakuagiza uwatii wazazi wako. (Waefeso 6:1) Na ikiwa wazazi wako wanaona kwamba hupaswi kuanzisha urafiki wa kimapenzi, bila shaka wana sababu nzuri. Hata hivyo, si ajabu ukiwa na maoni haya:

 ● Ninaona kwamba ninakosa kitu fulani kwa sababu kila mtu isipokuwa mimi ana mpenzi.

● Ninavutiwa na mtu ambaye si wa dini yangu.

● Ningependa kuwa na urafiki wa kimapenzi pamoja na Mkristo mwenzangu, hata ingawa sijafikia umri wa kufunga ndoa.

Huenda unajua maoni ya wazazi wako kuhusu taarifa zilizo juu. Nawe unajua moyoni kwamba wazazi wako wana haki ya kuwa na maoni hayo. Hata hivyo, huenda ukawa na maoni kama ya msichana anayeitwa Manami, anayesema: “Mkazo wa kuwa na urafiki wa kimapenzi ni wenye nguvu sana hivi kwamba nyakati nyingine mimi huwa na mashaka kuhusu msimamo wangu. Kwa maoni ya vijana wa leo, kutokuwa na mpenzi ni jambo lisilowazika. Isitoshe, hakuna raha yoyote maishani ukiwa peke yako!” Wengine walio katika hali kama hiyo wameanzisha urafiki wa kimapenzi na kuwaficha wazazi wao. Jinsi gani?

“Tuliambiwa Tusimwambie Yeyote”

Ili kuendeleza urafiki wa kimapenzi wa siri, udanganyifu fulani unahusika. Wengine wanadumisha urafiki wao ukiwa siri kwa kuwasiliana hasa kupitia simu au Intaneti. Wakiwa mbele ya watu wanaonekana kuwa marafiki tu, lakini barua-pepe, ujumbe mfupi wa simu, na mazungumzo yao kwenye simu yanaonyesha hali tofauti kabisa.

Njia nyingine ya ujanja ambayo vijana wanatumia ni kupanga tafrija huku wakiwa na lengo la kujitenga wakiwa wawili-wawili baadaye. James anasema hivi: “Siku moja tulialikwa mahali tukiwa kikundi, lakini baadaye tukagundua kwamba tafrija hiyo ilipangwa ili tu vijana fulani wawili waweze kuwa pamoja. Tuliambiwa tusimwambie yeyote.”

Kama James alivyosema, kwa kawaida marafiki husaidia kuendeleza urafiki huo ukiwa siri. Carol anasema: “Angalau rafiki mmoja hujua kinachoendelea lakini anaamua kunyamaza kwa sababu aliahidi kutomwambia yeyote.” Nyakati nyingine udanganyifu ulio wazi unahusika. Beth, mwenye umri wa miaka 17, anasema: “Wengi huendeleza urafiki wao wa siri kwa kuwadanganya wazazi wao kuhusu mahali ambapo wanaenda.” Misaki, mwenye umri wa miaka 19, alifanya hivyo. Anasema: “Ilinibidi nitunge hadithi za uwongo kwa makini. Nilikuwa mwangalifu nisiseme uwongo kuhusu mambo mengine isipokuwa tu yale yanayohusiana na urafiki wangu wa siri ili wazazi wangu waendelee kuniamini.”

Hatari za Urafiki wa Siri

Ukishawishiwa kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri, au ikiwa tayari umeanzisha urafiki wa aina hiyo, inafaa ujiulize maswali mawili yafuatayo:

Udanganyifu wangu utakuwa na matokeo gani? Je, unakusudia kufunga ndoa pamoja na mtu huyo hivi karibuni? Evan, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Mtu anayeanzisha urafiki wa kimapenzi bila kuwa na nia ya kufunga ndoa, ni kama mtu anayepeleka kitu fulani sokoni bila nia ya kukiuza.” Ni nini kinachoweza kutokea? Methali 13:12 inasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Je, kwa kweli ungependa kumfanya mtu unayemjali augue moyoni? Unapaswa kufikiria jambo hili pia: Kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri kunakunyima mashauri yenye upendo kutoka kwa wazazi wako na watu wazima wengine wanaokujali. Kwa sababu hiyo kuna uwezekano mkubwa wa kutumbukia katika upotovu wa kingono.—Wagalatia 6:7.

Yehova Mungu ana maoni gani kuhusu yale ninayofanya? Biblia inasema: “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Kwa hiyo, ikiwa unaficha urafiki wako wa kimapenzi au wa rafiki yako, tayari Yehova anajua jambo hilo. Na ikiwa umedanganya, unapaswa kuhangaishwa na jambo hilo. Yehova Mungu anachukia sana udanganyifu. Kwa kweli, Biblia inataja waziwazi kwamba “ulimi wa uwongo” ni kati ya mambo ambayo anachukia!—Methali 6:16-19.

Kufunua Siri

Bila shaka ingekuwa vema uzungumze na wazazi wako au Mkristo mkomavu ikiwa una urafiki wowote wa siri. Na ikiwa una rafiki aliye na rafiki wa kimapenzi wa siri, usishiriki katika matendo yake kwa kumsaidia kuficha urafiki huo. (1 Timotheo 5:22) Ungehisi jinsi gani ikiwa urafiki huo ungesababisha madhara? Je, hungelaumika kwa kiasi fulani?

Tuseme rafiki yako ambaye ana ugonjwa wa kisukari anakula keki kwa siri. Utafanya nini ukijua jambo hilo lakini rafiki yako anakusihi usimwambie mtu yeyote? Utachukua hatua gani—utaficha jambo hilo au utachukua hatua ambayo inaweza kuokoa uhai wake?

Ndivyo ilivyo ikiwa unajua kwamba rafiki yako ana urafiki wa kimapenzi wa siri. Usiogope kwamba urafiki wenu utavunjika. Baada ya muda, rafiki wa kweli atatambua kwamba ulichukua hatua kwa sababu unamjali.—Zaburi 141:5.

Ni Siri au Ni Faragha?

Si siri zote zinazohusiana na urafiki wa kimapenzi zinazohusisha udanganyifu. Tuseme mwanamume kijana na mwanamke kijana wangependa kujuana vizuri zaidi lakini wanataka kufanya hivyo kwa siri kwa muda fulani. Labda kama kijana anayeitwa Thomas anavyosema, “hawataki kuulizwa-ulizwa maswali kama, ‘Mtafunga ndoa siku gani?’”

Mikazo kutoka kwa wengine inaweza kuwa hatari. (Wimbo wa Sulemani 2:7) Hivyo, mwanzoni mwa uhusiano, huenda kwa busara watu fulani wakaamua kutowajulisha wengine kuhusu urafiki wao. (Methali 10:19) Anna, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Hilo linawawezesha watu hao wawili kuwa na wakati wa kuamua ikiwa wanataka kuendeleza urafiki huo. Baada ya kufanya uamuzi huo, ndipo wanaweza kuwajulisha wengine.”

Wakati huohuo, haifai kuwaficha watu ambao wana haki ya kujua kuhusu urafiki huo, kama vile wazazi wako au wazazi wa rafiki yako. Ikiwa hutaki urafiki huo ujulikane, unapaswa kujiuliza ni kwa nini. Je, tayari umeona kwamba wazazi wako wana sababu ya kuukataa?

“Nilijua Hatua Ambayo Ninapaswa Kuchukua”

Jessica, aliyetajwa mwanzoni, alibadili maoni yake kuhusu kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri pamoja na Jeremy aliposikia kuhusu Mkristo mwingine ambaye alikuwa katika hali kama hiyo. “Baada ya kusikia jinsi Mkristo huyo alivyovunja urafiki huo,” Jessica anasema, “nilijua hatua ambayo ninapaswa kuchukua.” Je, ilikuwa rahisi kuvunja urafiki huo? Hapana! Jessica anasema: “Hakuna mvulana mwingine ambaye nimepata kumpenda kama nilivyompenda huyo. Nililia kila siku kwa majuma kadhaa.”

Hata hivyo, Jessica alijua kwamba anampenda Yehova. Na ingawa alikuwa amekengeushwa, alitaka sana kufanya lililo sawa. Baadaye, uchungu wa kuuvunja urafiki huo ulipungua. Jessica anasema: “Sasa uhusiano wangu pamoja na Yehova umekuwa mzuri sana kuliko wakati mwingine wowote. Ninashukuru sana kwamba anatupa mwongozo tunaohitaji kwa wakati unaofaa!”

KATIKA SURA INAYOFUATA

Tuseme kwamba uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi na umempata mtu unayempenda. Unaweza kujua jinsi gani kwamba anakufaa?

MAANDIKO MUHIMU

“Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.

PENDEKEZO

Si lazima utangazie ulimwengu mzima kuhusu urafiki wenu. Lakini waambie wale walio na haki ya kujua. Kwa kawaida watu hao wanatia ndani wazazi wako na wazazi wa rafiki yako.

JE, WAJUA . . .?

Ili uwe na urafiki wenye kudumu ni lazima uwe mwenye kutumainika. Wazazi wako hawatakutumaini ikiwa una urafiki wa kimapenzi wa siri, na kufanya hivyo kunadhoofisha msingi wa uhusiano wako pamoja na rafiki yako.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ikiwa nina urafiki wa kimapenzi wa siri na Mkristo mwenzangu, nita ․․․․․

Ikiwa rafiki yangu ana urafiki wa kimapenzi wa siri nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Fikiria tena  mambo matatu ambayo yameandikwa kwa herufi nzito katika ukurasa wa 22. Ni jambo gani kati ya mambo hayo linalofafanua jinsi unavyohisi nyakati fulani?

● Unaweza kushughulikia jinsi gani jambo hilo bila kuanzisha urafiki wa kimapenzi wa siri?

● Ikiwa ungejua kwamba rafiki yako ana urafiki wa kimapenzi wa siri, ungeshughulikia jambo hilo jinsi gani, na kwa nini ungechagua kulishughulikia hivyo?

[Blabu katika ukurasa wa 27]

“Nilivunja urafiki wa kimapenzi wa siri. Kusema kweli, haikuwa rahisi kwenda shuleni na kumwona mvulana huyo kila siku. Hata hivyo, Yehova Mungu anaona kila kitu, lakini sisi hatuwezi. Tunahitaji tu kumtegemea Yehova.’’—Jessica

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kuficha urafiki wa kimapenzi wa rafiki yako ni kama kujua kwamba rafiki yako mwenye ugonjwa wa kisukari anakula keki lakini husemi