Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Somo La 10

Jinsi ya Kupata Dini ya Kweli

Jinsi ya Kupata Dini ya Kweli

Ukitaka kuwa rafiki ya Mungu, ni lazima ushirikiane na dini inayokubaliwa na Mungu. Yesu alisema kwamba “waabudu wa kweli” wangemwabudu Mungu kwa kupatana na “kweli.” (Yohana 4:23, 24) Kuna njia moja tu ya kweli ya kumwabudu Mungu. (Waefeso 4:4-6) Dini ya kweli huongoza kwenye uhai udumuo milele, na dini isiyo ya kweli huongoza kwenye uharibifu.—Mathayo 7:13, 14.

Unaweza kuitambua dini ya kweli kwa kuwaangalia washiriki wake. Kwa kuwa Yehova ni mwema, lazima waabudu wake wa kweli wawe watu wema. Kama vile mchungwa mwema huzaa machungwa mema, vivyo hivyo dini ya kweli hutokeza watu wema.—Mathayo 7:15-20.

Rafiki za Yehova wanaiheshimu sana Biblia. Wanajua kwamba Biblia imetoka kwa Mungu. Wao huruhusu mambo ambayo inasema yaongoze maisha yao, yatatue matatizo yao, na yawasaidie kujifunza juu ya Mungu. (2 Timotheo 3:16) Wao hujitahidi kutenda mambo wanayofundisha.

Rafiki za Yehova hupendana. Yesu aliwaonyesha watu upendo kwa kuwafundisha juu ya Mungu, na kwa kuwaponya wale waliokuwa wagonjwa. Washiriki wa dini ya kweli pia huwapenda watu wengine. Kama vile Yesu, hawawadharau maskini wala watu wa kabila tofauti. Yesu alisema kwamba watu wangewajua wanafunzi wake kwa jinsi wanavyopendana.—Yohana 13:35.

Rafiki za Mungu huheshimu jina la Mungu, Yehova. Ikiwa mtu fulani angekataa kutumia jina lako, je, angekuwa rafiki yako wa karibu? La! Tunapokuwa na rafiki, sisi hulitumia jina lake nasi huwaambia wengine mambo mema juu yake. Kwa hiyo, wale wanaotaka kuwa rafiki za Mungu wapaswa kulitumia jina lake na kuzungumza na wengine juu yake. Yehova anataka sisi tufanye hivyo.—Mathayo 6:9; Waroma 10:13, 14.

Kama alivyofanya Yesu, rafiki za Mungu huwafundisha watu juu ya Ufalme wa Mungu. Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni itakayoifanya dunia kuwa paradiso. Rafiki za Mungu huwaeleza wengine habari njema hizo juu ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuwa rafiki za Mungu. Wao wanaiheshimu Biblia nao wanapendana. Pia, wao hutumia na kuheshimu jina la Mungu na kuwafundisha wengine juu ya Ufalme wa Mungu. Mashahidi wa Yehova ndio wanaofuata dini ya kweli duniani leo.