Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 1

Je, Dini Zote Hufundisha Kweli?

Je, Dini Zote Hufundisha Kweli?

1. Ni zipi baadhi ya dini zinazofuatwa barani Afrika?

KARIBU kila mtu barani Afrika anakubali kwamba ni muhimu kumwabudu Mungu. Lakini watu hawakubaliani juu ya jinsi ya kumwabudu. Baadhi yao huabudu misikitini, huku wengine wakiabudu kwenye sehemu za kuabudia za kiasili. Wengine huenda kanisani. Lakini ni makosa kufikiri kwamba kuna dini tatu tu barani Afrika. Waislamu wana sheria na imani zinazotofautiana. Dini za kiasili hutofautiana sana katika sehemu mbalimbali. Kuna migawanyiko mikubwa hata zaidi kati ya makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo. Kotekote barani Afrika, kuna makanisa mengi madogo-madogo ambayo yamejitenga na yale makanisa makubwa.

Dini Yetu Inapaswa Kutegemea Kweli

2. (a) Kwa kawaida ni nini kinachoamua dini ya mtu? (b) Ni mambo gani ambayo hayathibitishi kwamba dini yetu inampendeza Mungu?

2 Ni nini kinachoamua jinsi watu watakavyoabudu? Watu wengi hukubali dini ya wazazi wao. Matukio ya kale pia huamua dini ambayo watu wanafuata leo. Kitabu The Africans—A Triple Heritage chasema: “Uislamu ulienea kaskazini mwa Sahara kupitia uvamizi, . . . nao Ukristo ukaenea kusini mwa Sahara kwa njia hiyohiyo. Uislamu ulienezwa kaskazini mwa Sahara kwa upanga, nao Ukristo ukaenezwa kusini mwa Sahara kwa bunduki.” Hata hivyo, wengi wetu huamini kwamba dini yetu inampendeza Mungu. Lakini dini haiwezi kuwa ya kweli kwa sababu tu wazazi wetu wanaifuata au kwa sababu wazazi wetu wa kale walilazimishwa na taifa fulani la kigeni waifuate.

3-5. Ni mfano gani unaotusaidia kuona kwamba si dini zote zinazofundisha kweli?

3 Ingawa dini zote hudai kwamba zina mwongozo wenye kutegemeka kuhusu kumtumikia Mungu, mafundisho ya dini hizo hutofautiana. Dini hufundisha mambo mengi yanayotofautiana kumhusu Mungu na mambo anayotaka tufanye. Hebu fikiria mfano huu: Tuseme umepata kazi katika kampuni fulani kubwa. Unapoenda kazini siku ya kwanza, unaelezwa kwamba mkubwa wa kampuni ameenda likizo. Hivyo unawauliza wafanyakazi watatu unachopaswa kufanya. Mfanyakazi wa kwanza anakuambia kwamba mkubwa anataka ufagie sakafu. Wa pili anakuambia kwamba unapaswa kupaka jengo rangi. Naye watatu anakuambia uwapelekee watu barua.

4 Kisha unawauliza wafanyakazi hao kuhusu mkubwa wa kampuni hiyo. Wa kwanza anakuambia kwamba mkubwa huyo ni kijana mrefu na mkali. Wa pili anakuambia kwamba yeye ni mzee mfupi na mwenye fadhili. Watatu anakuambia kwamba mkubwa huyo si mwanamume bali ni mwanamke. Yaelekea utaamua kwamba wafanyakazi wote watatu hawasemi kweli. Ikiwa unataka kuendelea kufanya kazi katika kampuni hiyo, yaelekea utafanya uchunguzi fulani ili kumjua vizuri mkubwa huyo na yale anayotaka ufanye.

5 Dini ziko hivyo. Kwa kuwa kuna mafundisho mengi sana kumhusu Mungu na mambo anayotaka tufanye, tunapaswa kuhakikisha kwamba ibada yetu inapatana na kweli. Lakini tunawezaje kujifunza kweli kumhusu Mungu?