Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 9

Dini ya Kweli Inaweza Kukufaidi Milele!

Dini ya Kweli Inaweza Kukufaidi Milele!

1. Itakuwaje ‘tukimkaribia Mungu’?

YEHOVA anawapenda wale wanaomtumikia, nawe ukimwabudu, yeye atakubariki sasa na wakati ujao. Biblia inasema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.”—Yakobo 4:8.

2. Tunaweza kumkaribiaje Mungu, na jambo hilo litakuwa na matokeo gani kwa sala zetu?

2 Ili kumkaribia Mungu ni lazima ujifunze na kutumia Neno lake. Yehova atasikiliza sala zako na kuzijibu ukisali kupatana na mapenzi yake. Mtume Mkristo Yohana aliandika: “Huu ndio uhakika ambao tunao kumwelekea yeye [Mungu], kwamba, hata iwe ni nini ambacho twaomba kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia. Zaidi, ikiwa twajua yeye hutusikia kwa habari ya chochote kile tunachoomba, twajua tutakuwa na mambo yaliyoombwa kwa kuwa tumeyaomba kwake.”—1 Yohana 5:14, 15.

3-7. Tunaweza kupataje hekima ya Mungu, nayo inaweza kutusaidiaje?

3 Zaidi ya hayo, unapomkaribia Mungu, atakupatia hekima ya kushughulika na mambo yanayotokea kila siku maishani. Biblia inasema: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu.”—Yakobo 1:5.

4 Hekima ya Mungu inaweza kukusaidiaje? Kwanza, inaweza kukusaidia kujua mambo yasiyompendeza Yehova. Unaweza pia kujua ni kwa nini mambo hayo ni mabaya na utafanya nini ili kuyaepuka. Ujuzi huo unaweza kukulinda usipatwe na matatizo mengi yanayowasumbua watu kwa jumla. Kwa mfano, kutii ushauri wa Mungu wa kuwa safi kiadili huwasaidia watu wake wasipate mimba haramu, magonjwa yanayoambukizwa kingono, na kuepuka kuvunjika kwa ndoa au ndoa zisizo na furaha.

5 Hekima ya Mungu inaweza kukusaidia katika njia gani nyingine? Hekima hiyo inaweza kukusaidia kupata faida kamili maishani. Inaweza kukusaidia ufanye maamuzi ya busara kuhusu mambo fulani, kama vile kutumia vizuri pesa zako. Utaweza kufuatia miradi inayofaa na kuacha ile isiyo na faida ya kudumu.

6 Hekima ya Mungu pia inaweza kukusaidia katika mahusiano yako na wengine. Maisha yako ya familia yanaweza kuwa yenye furaha zaidi. Unaweza kuwa na urafiki wa kweli na wenye kudumu pamoja na wengine na hata kuheshimiwa na wale wasiomtumikia Mungu.

7 Na zaidi ya hayo, kuwa na hekima ya Mungu kutaboresha maoni yako kuhusu maisha. Itakusaidia kukabiliana na matatizo na mambo yanayovunja moyo maishani. Pia, utakuwa na maoni yanayofaa na yenye usawaziko kuhusu wakati ujao. Maoni yanayofaa yatakusaidia uwe na afya njema kiakili na kimwili.—Mithali 14:30; Isaya 48:17.

8. Ukimtumikia Mungu, ni mambo gani ambayo hutaogopa?

8 Ukimtumikia Mungu wa kweli, hutakuwa na woga ambao huwasumbua wale wasiomtumikia. Hutawaogopa wafu kwa sababu unajua kwamba waliokufa wako makaburini na hawawezi kufanya lolote. Hutaogopa kufa kwa kuwa una uhakika na ahadi ya Mungu ya kuwafufua wafu. Na kwa kuwa unajua kwamba Mungu ni mwenye nguvu zote, hutaogopa uchawi au ulozi.—Yohana 8:32.

Wenye Haki Watairithi Dunia

9-11. Ni nani watakaoishi katika Paradiso, na ni nani ambao hawataishi humo?

9 Ukimkaribia Mungu, hutaogopa wakati ujao. Kama tulivyoona, Biblia ilitabiri mengi ya matatizo tunayoona duniani leo. Yehova anatuambia kwamba mambo hayo ni ya muda tu; hivi karibuni Ufalme wa Mungu utafanya dunia hii kuwa paradiso.—Luka 21:10, 11, 31; 23:43.

10 Wale wanaomkaribia Yehova na kumtumikia ndio tu watakaoishi katika Paradiso. Biblia inasema: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.

11 Wale wanaokataa kwa ukaidi kutii sheria za uadilifu za Mungu wataangamia milele. (2 Wathesalonike 1:8, 9) Hawatakuwapo tena. Wataangamia pamoja na Shetani na roho wake waovu katika kifo cha milele. (Ufunuo 20:10, 14) Lakini wale wanaojifunza kumhusu Yehova na kumtumikia watafurahia kuishi katika Paradiso duniani.

Wakati Ujao Mzuri Sana!

12. Biblia inasema nini kuhusu wakati ujao?

12 Yehova atawafanyia mambo mazuri sana wale wanaompenda! Hebu ona yale ambayo Neno lake linasema kuhusu maisha katika dunia Paradiso:

  • Chakula kingi: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.

  • Nyumba nzuri: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake.”—Isaya 65:21.

  • Kazi yenye kufurahisha: “Wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:22, 23.

  • Hakuna magonjwa: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.

  • Hakuna ulemavu: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.

  • Hakuna maumivu, maombolezo, kifo: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

  • Hakuna vita: “[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:9.

  • Uhai wa milele: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29..

13. Ni nani peke yake anayeweza kufanya dunia hii kuwa paradiso, na kwa nini?

13 Wanadamu hawawezi kutimiza mambo hayo, lakini Yehova ana uwezo wa kufanya lolote analosema. Hakuna kinachoweza kumzuia asifanye kile anachotaka kufanya. Biblia inasema: “Kwa Mungu hakuna tangazo lolote litakalokuwa lisilowezekana.”—Luka 1:37.

14. Unaweza kutembeaje katika barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele?

14 Kupitia Mashahidi wake, Yehova anawatolea watu kila mahali nafasi ya ‘kuingia kupitia lango jembamba’ na kutembea katika barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele. Na uwe kati ya watu wenye furaha wanaokubali mwaliko huo. Na ufuate dini ya kweli na kufurahia baraka za Yehova milele!—Mathayo 7:13, 14.