Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 6

Je, Mungu Huzikubali Dini Zote?

Je, Mungu Huzikubali Dini Zote?

1. Neno la Mungu linaonyesha kuna aina zipi mbili za dini?

YESU alisema, “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Neno la Mungu linaonyesha kwamba kuna aina mbili tu za dini: moja ya kweli, na nyingine isiyo ya kweli; moja inayofaa, na nyingine isiyofaa; moja inayoongoza kwenye uhai, na nyingine inayoongoza kwenye uharibifu.

2. Maandiko yanaonyeshaje kwamba Mungu hapendezwi na dini zote?

2 Watu wengine hufikiri kwamba Mungu hupendezwa na dini zote. Maandiko yafuatayo ya Biblia yanaonyesha kwamba hilo si kweli:

  • “Wana wa Israeli walifanya tena yaliyo maovu mbele za macho ya BWANA, wakawatumikia Mabaali, na Maashtorethi, na miungu ya Shamu, na miungu ya Sidoni, na miungu ya Moabu, na miungu ya wana wa Amoni, na miungu ya Wafilisti; nao wakamwacha BWANA, wala hawakumtumikia yeye. Hasira za BWANA ziliwaka juu ya Israeli.” (Waamuzi 10:6, 7) Tukiabudu sanamu au miungu mingine yoyote isipokuwa Mungu wa kweli, hatutapata kibali cha Yehova.

  • “Watu hawa huniheshimu mimi [Mungu] kwa midomo yao, bali mioyo yao imeondolewa mbali nami. Ni bure kwamba wao hufuliza kuniabudu, kwa sababu wao hufundisha amri za watu kuwa mafundisho.” (Marko 7:6, 7) Ikiwa watu wanaodai kumwabudu Mungu wanafundisha mawazo yao wenyewe badala ya kufundisha yaliyo katika Biblia, ibada yao ni ya bure. Haikubaliwi na Mungu.

  • “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Ni lazima ibada yetu ipatane na ukweli wa Neno la Mungu.

Matunda ya Dini Zisizo za Kweli

3. Unaweza kutumia njia gani moja kutofautisha dini ya kweli na isiyo ya kweli?

3 Tunaweza kujuaje kama dini inampendeza Mungu? Yesu alisema: “Kila mti mwema hutokeza matunda bora, lakini kila mti uliooza hutokeza matunda yasiyofaa kitu . . . Basi, kwa kweli kwa matunda yao mtawatambua watu hao.” Yaani, ikiwa dini imetokana na Mungu itazaa matunda mema; lakini ikiwa imetokana na Shetani, itazaa matunda mabaya. —Mathayo 7:15-20.

4. Waabudu wa Yehova huonyesha sifa gani?

4 Dini ya kweli hutokeza watu wanaopendana na wanaowapenda wengine. Hiyo ni kwa sababu Yehova mwenyewe ni Mungu mwenye upendo. Yesu alisema: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” Je, dini zinatimiza takwa hilo la ibada ya kweli?—Yohana 13:35; Luka 10:27; 1 Yohana 4:8.

5. Ensaiklopedia moja inaelezaje biashara ya watumwa Waafrika?

5 Hebu fikiria biashara ya watumwa Waafrika. Kichapo The New Encyclopædia Britannica kinasema: “Kati ya mwaka wa 650 na 1905, Waafrika wapatao 18,000,000 walisafirishwa kupitia eneo la Waislamu la Sahara na Bahari ya Hindi kwenda kuuzwa kuwa watumwa. Kuanzia katikati ya karne ya 15 Wazungu kutoka Ulaya walianza kufanya biashara ya watumwa katika pwani ya Afrika magharibi, na kufikia mwaka wa 1867 Waafrika kati ya 7,000,000 na 10,000,000 walisafirishwa wakiwa watumwa kupelekwa Amerika Kaskazini na Kusini na visiwa vya Karibea.”

6. Dini ilihusikaje katika biashara ya watumwa?

6 Dini ilichukua msimamo gani wakati huo wa msukosuko barani Afrika ambapo wanaume, wanawake, na watoto walitenganishwa na familia zao, wakafungwa minyororo, wakatiwa alama kwa chuma chenye moto, na kununuliwa au kuuzwa kama ng’ombe? Bethwell Ogot anaandika hivi katika gazeti la Daily Nation la Nairobi, Kenya: “Wakristo na Waislamu wanafundisha kwamba wanadamu wanapaswa kuwa na umoja, lakini dini hizo mbili zilitokeza watu wenye ubaguzi wa rangi walioweka watumwa. Waislamu wa Mashariki ya Kati na vilevile Wakristo wa Magharibi wanapaswa kukiri kwamba wana hatia kwa sababu walishindwa kushutumu biashara ya watumwa na ubaguzi wa kijamii uliosababisha mateso makubwa kwa Waafrika kwa karne nyingi.”

Dini na Vita

7. Viongozi wa kidini wamehusikaje katika vita?

7 Dini isiyo ya kweli imeonyesha matunda yake yaliooza katika njia nyinginezo. Kwa mfano, ingawa Biblia husema, ‘mpende jirani yako,’ viongozi wa kidini kote ulimwenguni wameunga mkono vita na kuichochea kwa bidii.—Mathayo 22:39.

Dini isiyo ya kweli imehusika katika vita na biashara ya watumwa

8. (a) Viongozi wa kidini walichocheaje mauaji katika vita barani Afrika? (b) Pasta mmoja alisema nini kuhusu viongozi wa kidini wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Nigeria?

8 Inajulikana vizuri kwamba katika mwaka wa 1994, watawa kadhaa wa kike na pia makasisi walishiriki kuua katika mauaji makubwa ya watu yaliyotokea Rwanda. Dini pia imehusika sana katika vita vingine barani Afrika. Kwa mfano, wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyosababisha umwagikaji mwingi wa damu nchini Nigeria, dini za pande zote mbili ziliwachochea watu wapigane. Vita hivyo vilipokuwa vikiendelea, pasta mmoja alisema kwamba viongozi wa makanisa “wameacha kazi ambayo Mungu aliwapa.” Pia alisema: “Sisi tunaojiita makasisi wa Mungu tumekuwa makasisi wa Shetani.”

9. Biblia inasema nini kuhusu wahudumu wa Shetani?

9 Biblia inasema vivyo hivyo: “Shetani mwenyewe hufuliza kujigeuza umbo mwenyewe kuwa malaika wa nuru. Kwa hiyo si jambo kubwa ikiwa wahudumu wake pia wafuliza kujigeuza umbo wenyewe kuwa wahudumu wa uadilifu.” (2 Wakorintho 11:14, 15) Kama vile watu wengi waovu hujifanya kuwa watu wazuri, Shetani naye huwadanganya watu kupitia wahudumu wake ambao kazi zao ni mbovu na matunda yao yameoza ingawa wao huonekana kuwa waadilifu.

10. Viongozi wa kidini wamemkana Mungu jinsi gani?

10 Ulimwenguni pote, viongozi wa kidini wamehubiri upendo, amani, na wema, lakini wana chuki, wameshiriki katika vita, na hawamwogopi Mungu. Biblia huwafafanua vizuri inaposema: “Wao hutangaza hadharani wamjua Mungu, lakini wao humkana yeye kwa kazi zao.”—Tito 1:16.

Tokeni Katika “Babiloni Mkubwa”

11. Biblia inafafanuaje dini isiyo ya kweli?

11 Tunaweza kupata maoni ya Yehova kuhusu dini zisizo za kweli kwa kusoma kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Katika kitabu hicho, dini isiyo ya kweli inafafanuliwa kuwa mwanamke wa mfano ambaye anaitwa “Babiloni Mkubwa.” (Ufunuo 17:5) Ona jinsi Mungu anavyomfafanua:

  • “Kahaba mkubwa . . . ambaye wafalme wa dunia walifanya uasherati naye.” (Ufunuo 17:1, 2) Badala ya kuonyesha uaminifu kwa Mungu, dini isiyo ya kweli imejiingiza katika siasa na mara nyingi huambia serikali yale ambayo serikali hizo zinapaswa kufanya.

  • “Katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wote wale ambao wamechinjwa juu ya dunia.” (Ufunuo 18:24) Dini isiyo ya kweli imenyanyasa na kuua watumishi waaminifu wa Mungu na imesababisha vifo vya watu wengi sana vitani.

  • “Alijitukuza mwenyewe na kuishi katika anasa isiyo na aibu.” (Ufunuo 18:7) Dini isiyo ya kweli ina mali nyingi sana ambazo viongozi wake hutumia kuishi maisha ya anasa.

  • “Kwa zoea [lake] la kuwasiliana na roho mataifa yote yaliongozwa vibaya.” (Ufunuo 18:23) Kupitia fundisho lake lisilo la kweli kwamba nafsi haifi, dini isiyo ya kweli imewafanya watu wajiingize katika kila aina ya uwasiliani-roho na ulozi na imewafanya waogope wafu na kuabudu wazazi wa kale.

12. Biblia inatoa onyo gani kuhusu dini isiyo ya kweli?

12 Biblia inawaonya watu vikali wajitenge na dini isiyo ya kweli ikisema: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya tauni zake.”—Ufunuo 18:4, 5.

13. Ni nini kitakachoipata dini isiyo ya kweli na wale wanaoifuata?

13 Hivi karibuni, Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, ataharibiwa kabisa. Biblia inasema: “Katika siku moja tauni zake zitakuja, kifo na kuomboleza na njaa kali, naye atachomwa kabisa kwa moto, kwa sababu Yehova Mungu, aliyemhukumu, ni mwenye nguvu.” (Ufunuo 18:8) Ili kuepuka “kupokea sehemu ya tauni zake,” tunapaswa kuvunja kabisa uhusiano wowote na dini isiyo ya kweli, na kuepuka kabisa mazoea, sherehe na mafundisho ambayo humchukiza Mungu. Tunapaswa kufanya hivyo haraka. Maisha yetu yamo hatarini!—2 Wakorintho 6:14-18.