Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 2

Unawezaje Kujifunza Kweli Kumhusu Mungu?

Unawezaje Kujifunza Kweli Kumhusu Mungu?

1, 2. Ni mfano gani unaoonyesha uhitaji wa kuwa na njia fulani ya kuamua mambo ya kidini?

TUNAWEZA kumjuaje Mungu? Je, ni lazima tuchunguze mafundisho yote ya dini mbalimbali? Hiyo haiwezekani. Na hata kama inawezekana, tungejuaje mafundisho ya kweli?

2 Bila shaka, kwa kuwa kuna mafundisho mbalimbali kumhusu Mungu, tunahitaji njia ya kujua ukweli wa mambo, njia ambayo itakubaliwa na kila mtu. Kwa mfano: Tuseme kuna ubishi sokoni kuhusu urefu wa kitambaa fulani. Muuzaji anasema kwamba kitambaa hicho kina urefu wa meta tatu, lakini mnunuzi anasema kwamba kitambaa hicho hakifiki meta tatu. Ubishi huo unaweza kutatuliwaje? Kwa kupima urefu wa kitambaa hicho kwa utepe wa kupimia.

3. Kwa nini Biblia iliandikwa?

3 Je, kuna utepe wa kupimia, yaani, njia fulani tunayoweza kutumia kuamua mambo ya kidini? Ndiyo, tunaweza kutumia Biblia. Mungu aliagiza Biblia iandikwe ili watu kila mahali wajifunze kweli kumhusu yeye. Biblia imechapwa kwa wingi sana. Nayo imetafsiriwa, kwa sehemu au yote nzima, katika lugha zaidi ya 2,100. Karibu kila mtu anaweza kusoma kweli kumhusu Mungu katika lugha yake mwenyewe.

4. Biblia ina habari gani?

4 Biblia ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Inaeleza mambo ambayo hatungeweza kuyajua kutokana na chanzo kingine. Inaeleza juu ya viumbe wanaoishi katika makao ya roho. Inafunua mawazo ya Mungu, utu wake, na kusudi lake. Inaeleza kuhusu jinsi alivyoshughulika na watu kwa maelfu ya miaka. Inataja mambo yatakayotukia wakati ujao. Nayo inaonyesha jinsi ambavyo tunaweza kupata barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele.

Kwa Nini Uiamini Biblia?

5. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Biblia inapatana na sayansi?

5 Kuna sababu nyingi zinazoweza kutufanya tuamini kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Mungu. Sababu moja ni kwamba Biblia inapatana na sayansi. Zamani za kale, watu ulimwenguni pote walifikiri kwamba dunia ilikuwa imeshikiliwa na kitu fulani. Kwa mfano, zamani watu huko Afrika Magharibi waliamini kwamba dunia imeshikiliwa na nyoka aliyejikunja, akiwa amejikunja mara 3,500 juu ya dunia na mara 3,500 chini ya dunia. Hata hivyo, kupatana na sayansi, mwandishi mmoja wa Biblia aliandika zaidi ya miaka 3,500 iliyopita kwamba Mungu ‘anautundika ulimwengu pasipo kitu.’—Ayubu 26:7.

6. Ni uthibitisho gani mkubwa zaidi unaoonyesha kwamba Biblia ni kitabu cha Mungu?

6 Uthibitisho mkubwa zaidi unaoonyesha kwamba kwa kweli Biblia ni kitabu cha Mungu ni kutimizwa kikamili kwa utabiri wake kuhusu wakati ujao. Tofauti na watu wanaofanya uaguzi, kwa kweli Mungu anajua wakati ujao. Kila jambo analosema hutimia.

7. Ni unabii gani wa Biblia ambao ulitimizwa wakati uliopita?

7 Unabii mwingi sana wa Biblia ulitimizwa zamani. Kwa mfano, miaka 700 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu, Biblia ilisema kwa usahihi kwamba yeye angezaliwa katika mji wa Bethlehemu, na ikawa hivyo. (Mika 5:2; Mathayo 2:3-9) Mbali na unabii mwingine mwingi kumhusu Yesu, Biblia pia ilitabiri kwamba angezaliwa na bikira na mwishowe angesalitiwa kwa vipande 30 vya fedha. Unabii huo pia ulitimia. Bila shaka, hakuna mwanadamu ambaye angeweza kutabiri mambo hayo!—Isaya 7:14; Zekaria 11:12, 13; Mathayo 1:22, 23; 27:3-5.

8. Ni unabii gani wa Biblia unaotimizwa leo, nao unathibitisha nini?

8 Unabii mwingi wa Biblia unatimizwa leo. Hebu ona mifano michache:

  • “Taifa litainuka dhidi ya taifa [katika vita], na ufalme dhidi ya ufalme; na kutakuwa na matetemeko makubwa ya dunia, na katika mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kuambukiza na upungufu wa chakula.”—Luka 21:10, 11.

  • Kutakuwa na ‘ongezeko la uasi-sheria.’—Mathayo 24:12.

  • “Katika siku za mwisho . . . watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, . . . wasiotii wazazi, . . . wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, . . . wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.”—2 Timotheo 3:1-5.

Je, hukubali kwamba mambo haya yanatukia leo? Ukweli na usahihi wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba Biblia ni kitabu cha pekee, Neno la Mungu lililopuliziwa!—2 Timotheo 3:16.

Je, Biblia Imebadilishwa?

9, 10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu hakuwaruhusu watu waibadili Biblia?

9 Tuseme una kiwanda na kwamba umeandika sheria ambazo wafanyakazi wako wanapaswa kufuata. Ikiwa adui fulani angebadili sheria hizo, ungefanya nini? Je, hungerekebisha sheria zilizobadilishwa? Vivyo hivyo, Mungu hawaruhusu watu wabadili kweli ya Neno lake, Biblia.

10 Wale ambao wamejaribu kubadili mafundisho ya Neno la Mungu hawakufaulu. Tunapolinganisha Biblia tuliyo nayo sasa na nakala za Biblia za zamani, tunaona kwamba zinafanana. Jambo hilo linaonyesha kwamba katika miaka mingi ambayo imepita, Biblia haikubadilishwa.