Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 3

Ni Nani Wanaoishi Katika Makao ya Roho?

Ni Nani Wanaoishi Katika Makao ya Roho?

1. Dini ya kiasili imelinganishwaje na mlima?

IMANI za kiasili za Waafrika zimelinganishwa na mlima. Juu kabisa kuna Mungu, ambaye ana nguvu nyingi zaidi za kiroho. Chini kidogo kuna miungu au roho wengine wadogo, ambao ni watumishi wa Mungu. Chini yao kuna wazazi wa kale waliokufa, ambao huzikumbuka familia zao duniani na kuzisaidia. Chini kabisa kuna roho wenye nguvu kidogo: wachawi, waaguzi, na walozi.

2. Msemo mmoja wa Kiafrika unaonyeshaje kwamba imani za kiasili huathiri dini?

2 Imani hizo za kiasili zimeathiri sana dini nyingine barani Afrika. Msemo mmoja wa Kiafrika unasema: “Kufuata Dini (ya Kikristo au Kiislamu) hakutuzuii kuabudu miungu yetu.”

3. Ni wapi tunapoweza kujifunza kweli kuhusu viumbe wanaoishi katika makao ya roho?

3 Je, imani za kiasili za Kiafrika zina ukweli gani? Biblia hutuambia kweli kuhusu viumbe wanaoishi katika makao ya roho.

Yehova, Mungu wa Kweli

4. Dini zilizo kubwa barani Afrika zinakubali nini?

4 Dini tatu kubwa barani Afrika hukubali kwamba kuna Mungu na kwamba yeye ndiye mkuu kuliko wote. Biblia husema kuwa yeye ndiye “Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu [“mwenye uwezo,” NW], mwenye kuogofya.” (Kumbukumbu la Torati 10:17) Waislamu pia wanaamini kuna Mungu mmoja aliye mkuu kuliko wote. Kuhusu dini za kiasili za Afrika, Profesa Geoffrey Parrinder anasema: “Waafrika wengi wamekuwa wakiamini kwamba kuna Mungu mkuu kuliko wote, baba wa miungu na wanadamu, muumba wa ulimwengu wote.”

5. Ni baadhi ya majina gani yanayotumiwa kumwita Mungu?

5 Hata hivyo, ingawa kila mahali watu wanamwamini Mungu, watu wengi hawamjui vizuri. Hatua ya kwanza ya kumjua mtu ni kulijua jina lake. Katika dini mbalimbali, watu hawaelewani kuhusu jina la Mungu. Kwa kawaida, Jumuiya ya Wakristo humwita Mungu, jina la cheo linalomaanisha “Mwenye Uwezo.” Waislamu wanamwita Allah. Majina ambayo wafuasi wa dini za kiasili humwita Aliye Mkuu Kuliko Wote hutofautiana kulingana na lugha zao. Katika kitabu chake, Concepts of God in Africa, John S. Mbiti anaorodhesha majina zaidi ya 500 ya Kiafrika ambayo yamepewa Mungu. Kwa mfano, katika Kiyoruba (Nigeria), Mungu anaitwa Olodumare; Wakikuyu (Kenya) humwita Ngai; nao Wazulu (Afrika Kusini) humwita Unkulunkulu.

6, 7. Jina la Mungu ni nani, na tunajuaje hivyo?

6 Mungu mwenyewe anasema jina lake ni nani? Mungu alipomwagiza Musa awaongoze Waisraeli kutoka Misri, Musa aliuliza: “Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? niwaambie nini?”—Kutoka 3:13.

7 Mungu alimwambia: “Mimi ni YEHOVA; nami nilimtokea Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kama Mungu Mwenyezi, bali kwa jina langu YEHOVA sikujulikana kwao.” (Kutoka 6:2, 3) Jina hilo linapatikana zaidi ya mara 7,000 katika Biblia, ingawa tafsiri fulani za Biblia zimeliondoa na badala yake zimetumia majina ya cheo kama “Mungu” au “Bwana.”

8. Yehova ni Mungu wa aina gani, nasi lazima tufanye nini iwapo tunataka kibali chake?

8 Yehova ni Mungu wa aina gani? Yeye ni roho, mweza yote, na mtukufu. Yeye ni mkuu kuliko wote, hakuna anayelingana naye wala aliye sawa na yeye. (Kumbukumbu la Torati 6:4; Isaya 44:6) Yehova alimwambia Musa hivi: “Mimi, BWANA, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [“anayesisitiza ujitoaji usiohusisha wengine,” NW].” Yaani, ili kupata kibali cha Yehova, ni lazima tumwabudu yeye peke yake. Hataki tuabudu kitu kingine chochote au mtu mwingine yeyote.—Kutoka 20:3-5.

Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu

9. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yesu si sawa na Yehova?

9 Leo watu wengi hawamjui Yesu vizuri. Wengi katika Jumuiya ya Wakristo wanaamini kwamba Yesu ni sehemu ya Utatu “Mtakatifu.” Lakini Biblia haifundishi kwamba Mungu ni watu watatu katika mmoja. Wala haifundishi kwamba Yesu ni sawa na Yehova. Yesu mwenyewe alisema: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.”—Yohana 14:28.

10. Yesu alikuwa wapi kabla ya kuja duniani?

10 Biblia hufundisha kwamba kabla ya kuishi duniani akiwa mwanadamu, Yesu aliishi mbinguni akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo. Yehova aliumba Adamu na Hawa duniani na pia akaumba viumbe wa roho mbinguni. Yesu ndiye kiumbe wa roho wa kwanza kuumbwa na Yehova.—Yohana 17:5; Wakolosai 1:15.

11. Yesu alizaliwa akiwa mwanadamu jinsi gani?

11 Miaka ipatayo 2,000 iliyopita, Yehova alihamisha uhai wa kiumbe huyu wa roho hadi katika tumbo la uzazi la bikira aitwaye Maria. Malaika Gabrieli alimwambia: “Utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe itakupasa kumwita jina lake Yesu. Naye atatawala akiwa mfalme . . . , na hakutakuwa na mwisho wa ufalme wake.”—Luka 1:31, 33. *

12. Sababu moja iliyofanya Yesu aje duniani ni nini?

12 Hivyo Yesu alizaliwa, akakua akawa mtu mzima, na kuwafundisha watu mapenzi na kusudi la Yehova. Alimwambia hivi gavana mmoja Mroma: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Kwa kufikiria yale aliyofundisha Yesu, tunaweza kujifunza kweli kuhusu mapenzi na kusudi la Mungu. Tunaweza kujifunza jinsi ya kupata kibali cha Mungu.

13. Ni nini sababu ya pili iliyofanya Yesu aje duniani?

13 Sababu ya pili iliyofanya Yesu aje duniani ni kutoa uhai wake wa kibinadamu kuwa fidia kwa ajili ya wanadamu. (Mathayo 20:28) Alifanya hivyo ili tuwekwe huru na dhambi tuliyorithi kutoka kwa babu yetu Adamu. Jambo hilo nalo linatuwezesha kuishi milele. Mtume Yohana aliandika: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:16.

14. (a) Ni jambo gani lililompata Yesu baada ya kufa akiwa mwanadamu? (b) Sasa Yesu ana cheo gani mbinguni?

14 Baada ya kifo chake akiwa mwanadamu, Yesu alifufuliwa na kwenda mbinguni, ambako alianza tena kuishi akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu. (Matendo 2:32, 33) Baadaye, Yehova alimpa “mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie.” (Danieli 7:13, 14) Yesu amefanywa kuwa Mfalme mwenye uwezo; yeye ni Mfalme wa serikali ya mbinguni ya Yehova. Hivi karibuni ataonyesha uwezo wake katika dunia yote.

Malaika, Wahudumu wa Mungu

15. Malaika waliumbwa wakati gani na wapi?

15 Mbali na Yehova na Yesu, kuna viumbe wengine wanaoishi katika makao ya roho. Yehova aliumba viumbe wengine wa roho wanaoitwa malaika. Gabrieli aliyezungumza na Maria ni mmoja wao. Malaika hawakuanza maisha yao wakiwa wanadamu duniani. Waliumbwa huko mbinguni muda mrefu kabla ya wanadamu kuumbwa duniani. (Ayubu 38:4-7) Kuna mamilioni ya malaika.—Danieli 7:10.

Malaika waaminifu hukataa kuabudiwa

16. Kwa nini wanadamu hawapaswi kuabudu malaika?

16 Malaika waaminifu hawataki tuwaabudu. Mtume Yohana alijaribu mara mbili kuabudu malaika, lakini wakamkemea, wakisema: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! . . . Abudu Mungu.”—Ufunuo 19:10; 22:8, 9.

17. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba malaika wanaweza kuwalinda watumishi wa Mungu, na kwa nini jambo hilo linafariji?

17 Malaika hawawatokei tena watu wa Mungu duniani, kama walivyofanya walipowakomboa mitume wa Yesu kutoka gerezani. (Matendo 5:18, 19) Hata hivyo, tukimwabudu Yehova kupatana na Neno lake, Biblia, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutalindwa na malaika zake wenye nguvu na wasioonekana. Biblia inasema: “Malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.” (Zaburi 34:7; 91:11) Kwa nini jambo hilo litufariji? Kwa sababu kuna maadui hatari katika ulimwengu wa roho wanaotaka kutuangamiza!

Shetani, Adui wa Mungu

18. (a) Kwa nini malaika mmoja alimwasi Mungu? (b) Malaika huyo mwasi alipewa majina gani?

18 Malaika wengine wa Mungu walikosa kuwa waaminifu kwake. Malaika hao walimwasi Mungu, wakawa maadui wake na wa watu wake duniani. Jambo hilo lilitokeaje? Malaika wote ambao Yehova aliumba walikuwa waadilifu na wema. Hata hivyo, mmoja wa wana hao wakamilifu wa roho alitaka watu wamwabudu naye akatenda kupatana na tamaa hiyo mbaya. Roho huyo mwovu alipewa jina Shetani, linalomaanisha “Mpinzani [wa Mungu].” Anaitwa pia Ibilisi, jina linalomaanisha “Mchongezi,” kwa kuwa yeye husema uwongo mbaya sana kumhusu Yehova.

19. Kwa nini Shetani alimtesa Yobu, naye alifanyaje hivyo?

19 Shetani huwakaza watu wajiunge naye katika kumwasi Mungu. Ona yale aliyomfanyia Yobu mtumishi mwaminifu wa Mungu. Yobu alikuwa tajiri sana. Alikuwa na kondoo 7,000, ngamia 3,000, ng’ombe-jike na ng’ombe-dume 1,000, na punda-jike 500. Alikuwa pia na watoto kumi na watumishi wengi. Kwanza, Shetani aliua mifugo ya Yobu na watumishi wake. Kisha akatokeza “upepo wenye nguvu” ulioharibu nyumba na kusababisha vifo vya watoto wote wa Yobu. Baadaye, Shetani alimtesa Yobu kwa “majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa.”—Ayubu 1:3-19; 2:7.

20. (a) Yobu alithawabishwaje kwa uaminifu wake? (b) Ingawa Yobu alikuwa mwaminifu kwa Mungu, Shetani amewafanyaje watu wengine wengi?

20 Licha ya jaribu hilo kali, Yobu aliendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu. Kwa hiyo Yehova alimponya na ‘kumpa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza.’ (Ayubu 42:10) Shetani alishindwa kuvunja uaminifu wa Yobu, lakini amefaulu kuwafanya watu wengine wengi wamwache Mungu. Biblia inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.”—1 Yohana 5:19.

21. (a) Shetani alionyeshaje tamaa yake ya kutaka kuabudiwa? (b) Kwa nini Yesu alikataa kumwabudu Shetani?

21 Shetani hutaka sisi tumwabudu. Alionyesha jambo hilo waziwazi wakati alipomjaribu Yesu miaka 2,000 hivi iliyopita. Biblia inasimulia: “Ibilisi akamchukua [Yesu] kwenda pamoja naye kwenye mlima ulioinuka juu isivyo kawaida, na kumwonyesha falme zote za ulimwengu na utukufu wazo, naye akamwambia: ‘Hakika nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.’” Yesu alikataa na kusema: “Enda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.’” (Mathayo 4:8-10) Yesu alijua sheria ya Yehova vizuri, naye alikataa kumwabudu Shetani.

Roho Waovu

22. Roho waovu wamewatendea wanadamu nini?

22 Malaika wengine walijiunga na Shetani katika kumwasi Mungu. Malaika hao waovu ni maadui wa watu duniani. Ni wakatili sana. Zamani walifanya watu fulani kuwa bubu na vipofu. (Mathayo 9:32, 33; 12:22) Waliwafanya wengine kuwa wagonjwa au watende kana kwamba wamerukwa na akili. (Mathayo 17:15, 18; Marko 5:2-5) Hata waliwatesa watoto.—Luka 9:42.

23. (a) Roho waovu wanataka wanadamu wafanye nini? (b) Shetani na roho waovu wamedanganya watu wafanye nini?

23 Kama Shetani, roho hao waovu pia hutaka kuabudiwa. Badala ya kukataa kuabudiwa na wanadamu na hivyo kuonyesha wanatambua kwamba Mungu pekee ndiye anayestahili kuabudiwa, wao wanatamani sana ibada hiyo, wanaitafuta, na kuiendeleza. Shetani na roho waovu hutumia udanganyifu, uwongo, na hofu ili kuwafanya watu wawaabudu. Bila shaka, si watu wengi wanaojua kwamba wanamwabudu Shetani na roho wake waovu. Watu wengi wangeshangaa sana kujua kwamba dini yao humtukuza Shetani. Na hata Biblia inaonya: “Vitu ambavyo mataifa huvidhabihu huwa wavidhabihu kwa roho waovu, na si kwa Mungu.”—1 Wakorintho 10:20.

24. Ni mbinu gani ambayo Shetani hutumia kuwadanganya watu?

24 Njia moja ambayo Shetani na roho wake waovu hutumia kufanya watu wawaabudu ni kueneza imani zisizo za kweli kuhusu wafu. Na tuone Biblia hufundisha nini kuhusu wafu.

^ fu. 11 Qurani inataja kuzaliwa kwa Yesu kimuujiza kwenye Sura ya 19 (Mariamu). Inasema: “Tukampelekea [Mariamu] Muhuisha Sharia yetu (Jibrili)—akajimithilisha kwake (kwa sura ya) binadamu aliye kamili. (Mariamu) akasema: ‘Hakika mimi najikinga kwa (Mwenyezi Mungu) Mwingi wa rehema (Aniepushe) nawe. Ikiwa unamuogopa Mungu (basi ondoka nenda zako).’ (Malaika) akasema: ‘Hakika mimi ni Mjumbe wa Mola wako: ili nikupe mwana mtakatifu.’ Akasema: ‘Nitawezaje kupata mtoto, hali hajanigusa mwanamume (yoyote kwa njia halali) wala mimi si (mwanamke) mwenye kuzini.’ (Malaika) akasema: ‘Ni kama hivyo (unavyosema; lakini) Mola wako amesema: “Haya ni sahali Kwangu, na ili Tumfanye Muujiza kwa wanaadamu na rehema itokayo kwetu (ndiyo tumefanya hivi);” na hili ni jambo lililokwisha hukumiwa.’”