Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 7

Ni Nani Wanaofuata Dini ya Kweli?

Ni Nani Wanaofuata Dini ya Kweli?

1. Ni lazima tufanye nini ili kumpendeza Mungu?

NI LAZIMA tuepuke kabisa dini isiyo ya kweli ili tuwe na uhusiano mzuri na wenye upendo pamoja Mungu. Ni lazima tufuate dini ya kweli. Leo mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanafanya hivyo.

2. Mashahidi wa Yehova wanaweza kupatikana wapi, na wanafanya kazi gani?

2 Kama Biblia ilivyotabiri, waabudu wa kweli wanafanyiza “umati mkubwa” ambao umetoka “katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Ufunuo 7:9) Katika nchi 235, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanawasaidia wengine wajifunze njia za upendo za Yehova na matakwa yake.

Kutambua Waabudu wa Kweli

3. Mashahidi wa Yehova humwabudu nani, nao huepuka ibada za aina gani?

3 Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba Yehova peke yake ndiye anayestahili kuabudiwa. Wao hukataa kuinamia sanamu au picha za kidini. (1 Yohana 5:21) Hawaabudu wafu kwa kushiriki kesha au sherehe nyingine zinazoendeleza imani za dini isiyo ya kweli na “mafundisho ya roho waovu.” (1 Timotheo 4:1) Hata hivyo, wao huwafariji waliofiwa kwa kuwaeleza ahadi ya Mungu kwamba wafu watafufuliwa katika dunia paradiso.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

4. Watu wa Mungu huuonaje uchawi?

4 Mashahidi wa Yehova huepuka uchawi na ulozi, kwa kuwa wanajua mambo hayo yanatokana na Ibilisi. Hawatumaini uchawi uwalinde bali wao humtumaini Yehova.—Mithali 18:10.

5. Ni katika njia gani Mashahidi wa Yehova “si sehemu ya ulimwengu”?

5 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake hawangekuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Yesu mwenyewe alikataa kujihusisha na siasa katika siku zake. (Yohana 6:15) Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na siasa, utukuzo wa taifa, au kung’ang’ania vyeo katika ulimwengu huu. Hata hivyo, wao hulipa kodi na kutii sheria za nchi wanamoishi.—Yohana 15:19; Waroma 13:1, 7.

6. Watumishi wa Mungu hufuata maagizo gani kuhusu ndoa na talaka?

6 Kwa sababu Mashahidi wa Yehova hutii agizo la serikali, wao huhakikisha kwamba ndoa zao zimeandikishwa kisheria. (Tito 3:1) Wao hutii agizo la Mungu na hivyo hawaoi wake wengi. (1 Timotheo 3:2) Na zaidi, kwa sababu wanafuata kanuni za Mungu, inakuwa vigumu kutalikiana au ndoa zao kuvunjika.

7. Mashahidi huonyeshanaje upendo?

7 Mashahidi wa Yehova wanapendana. Upendo huo, pamoja na upendo wao kwa Mungu, huwaunganisha kuwa udugu wa kweli, ingawa wametoka katika makabila na mataifa mbalimbali. Kunapotokea msiba au uhitaji fulani, Mashahidi wa Yehova huchukua hatua mara moja na kusaidiana. Mashahidi huonyesha upendo kwa jinsi wanavyoishi.—Yohana 13:35.

Mashahidi wa Yehova wameungana kuwa udugu wa ulimwenguni pote

8. Watu wa Mungu huepuka mazoea gani mabaya?

8 Watu wa Yehova hujitahidi sana kuishi kwa unyofu na kwa uaminifu. Wao huepuka wizi, uongo, ukosefu wa maadili, ulevi, na udanganyifu katika biashara. Waume hawawapigi wake zao. Kabla ya kuwa Mashahidi wa Yehova, baadhi yao walifanya mambo hayo, lakini kwa msaada wa Yehova wakaacha. ‘Walioshwa wakawa safi’ mbele za Mungu.—1 Wakorintho 6:9-11.

Watu Wanaofanya Mapenzi ya Mungu

9. Kitabu kimoja kilisema nini kuhusu dini za Kikristo zinazofuata tamaduni za Kiafrika?

9 Bila shaka, dini nyingi hudai kuwa za kweli. Huenda dini hizo zikataja kazi zenye nguvu ili kuthibitisha madai yao. Kwa mfano, kuhusiana na dini za Kikristo zinazofuata tamaduni za Kiafrika, kitabu fulani kinasema: “Kwa sehemu kubwa kazi ya wachawi imechukuliwa na [makundi mapya ya Kikristo]. . . . Wao hudai kwamba wanatabiri na kufanya miujiza. Manabii wao huona maono na kutafsiri ndoto. Wao hutumia maji matakatifu, mafuta matakatifu, majivu, mishumaa na uvumba ili kuponya na kuzuia magonjwa.”

10, 11. Kwa nini ile inayoitwa eti miujiza leo haionyeshi kwamba dini imekubaliwa na Mungu?

10 Wafuasi wa dini hizi hudai kwamba miujiza huthibitisha kwamba dini yao imekubaliwa na Mungu. Lakini hiyo inayoitwa eti miujiza haithibitishi kwamba dini imekubaliwa na Yehova. Shetani huwapa waabudu fulani wasio wa kweli nguvu za kufanya ‘kazi zenye nguvu.’ (2 Wathesalonike 2:9) Na zaidi ya hayo, Biblia ilitabiri kwamba zawadi za kimuujiza kutoka kwa Mungu, kama vile kutoa unabii, kuzungumza kwa lugha, na ujuzi wa kipekee, ‘zingeondolewa mbali.’—1 Wakorintho 13:8.

11 Yesu alionya: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbingu, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye katika mbingu ataingia. Wengi wataniambia katika siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya kazi nyingi zenye nguvu katika jina lako?’ Na bado ndipo hakika nitaungama kwao: Sikuwajua nyinyi kamwe! Ondokeni kwangu, nyinyi wafanyakazi wa uasi-sheria.”—Mathayo 7:21-23.

12. Ni nani watakaoingia katika Ufalme wa mbinguni?

12 Hivyo basi, ni nani watakaoingia katika Ufalme wa mbinguni? Ni wale wanaofanya mapenzi ya Yehova.

Wahubiri wa Ufalme wa Mungu

13. Mungu amewaagiza watu wake wafanye kazi gani leo, na ni nani wanaoifanya?

13 Mungu anataka watu wake wafanye nini leo? Yesu alisema: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Hii ndiyo kazi ambayo Mashahidi wa Yehova wanafanya kwa bidii.

14. Ufalme wa Mungu ni nini, na ni nani watakaotawala katika Ufalme huo?

14 Katika “dunia yote inayokaliwa,” Mashahidi wa Yehova hutangaza Ufalme wa Mungu kuwa serikali ya mbinguni ambayo itatawala dunia nzima kwa uadilifu. Wao hufundisha kwamba Yehova amemweka rasmi Kristo Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme huo, pamoja na watawala wenzake 144,000 ambao wamechaguliwa kutoka kwa wanadamu.—Danieli 7:14, 18; Ufunuo 14:1, 4.

15. Ufalme huo utaharibu nini?

15 Mashahidi hutumia Biblia kuonyesha watu kwamba Ufalme wa Mungu utaharibu ulimwengu wote wa Shetani. Dini isiyo ya kweli pamoja na mafundisho yake yanayomvunjia Mungu heshima na kumtukuza Ibilisi itaondolewa kabisa! (Ufunuo 18:8) Serikali za kibinadamu ambazo humpinga Mungu zitaondolewa pia! —Danieli 2:44.

16. Ni nani watakaokuwa raia wa Kristo Yesu, nao wataishi wapi?

16 Na zaidi ya hayo, Mashahidi wa Yehova hujulisha watu kwamba Yesu Kristo atawaletea faida nyingi wale wanaofanya yale ambayo Mungu anataka. Watakuwa raia zake duniani. Biblia inaahidi: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:12, 13.

17. Ni nani peke yao wanaotangaza Ufalme wa Mungu?

17 Hakuna kundi lingine la watu linalofanya mapenzi ya Mungu kwa kuhubiri habari njema za Ufalme. Mashahidi wa Yehova peke yao ndio hujulisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu duniani pote.