Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 4

Wazazi Wetu wa Kale Wako Wapi?

Wazazi Wetu wa Kale Wako Wapi?

1, 2. Watu wengi wanaamini nini kuhusu wazazi waliokufa?

WATU wengi sana barani Afrika wanaamini kwamba kifo si mwisho wa maisha bali ni badiliko tu linalomwezesha mtu kuendelea na maisha mahali pengine. Wengi wanafikiri kwamba wazazi wao wa kale walihama ulimwengu wenye kuonekana na kwenda ulimwengu usioonekana, yaani walihama ulimwengu wa wanadamu na kwenda ulimwengu wa roho.

2 Inaaminika kwamba wazazi hao wa kale, au roho zao, huhakikisha kwamba familia zao duniani wanaendelea kuishi na wana ufanisi. Kulingana na maoni hayo, roho za wazazi wa kale ni marafiki wao wenye nguvu nyingi, wanaoweza kuleta mavuno mazuri, kuleta hali njema, na kuwakinga wasipatwe na mabaya. Wazazi hao wa kale wakipuuzwa au kukasirishwa, inasemekana kwamba wanaweza kusababisha misiba kama vile ugonjwa, umaskini, na maafa.

3. Watu fulani huabudu wazazi wa kale jinsi gani?

3 Watu walio hai hufuata mila na desturi fulani ili kuwaheshimu na kudumisha uhusiano mzuri na roho za wazazi wa kale. Mambo hayo huonekana mara nyingi kwenye desturi za mazishi, kama vile kesha na sherehe zinazofanywa baada ya mazishi. Wazazi wa kale huabudiwa kwa njia nyingine pia. Kwa mfano, kabla ya kunywa pombe, watu fulani humwaga kiasi kidogo chini kwa ajili ya wazazi wao wa kale. Pia, baada ya mlo kupikwa, chakula fulani huachwa katika nyungu ili wazazi hao waliokufa wakija wapate chakula.

4. Watu wengi huamini nini kuhusu nafsi?

4 Watu wengine huamini kwamba watu walio hai wana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Inasemekana kwamba mtu akiwa mzuri, nafsi yake huenda mbinguni au peponi, lakini mtu akiwa mbaya, inasemekana kwamba nafsi yake huhukumiwa kwenda motoni. Mara nyingi watu huchanganya fundisho hilo na mapokeo. Kwa mfano, nyakati nyingine matangazo ya vifo katika magazeti husema kwamba mtu “ameaga dunia” au “ameitwa.” Imani hizo zinatokana na lile fundisho kwamba nafsi, au roho, huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Biblia husema nini kuhusu jambo hilo?

Nafsi na Roho

5, 6. Nafsi ni nini kulingana na Biblia?

5 Biblia inaonyesha kwamba nafsi si kitu kilicho ndani ya mtu; nafsi ni mtu mwenyewe. Kwa mfano, Mungu alipomwumba Adamu, “mtu [huyo] akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Adamu hakupewa nafsi; yeye alikuwa nafsi, mtu kamili.

6 Hiyo ndiyo sababu Biblia fulani hutumia maneno “mwanadamu,” “kiumbe,” au “mtu” badala ya neno “nafsi,” ambalo lilitumiwa kutafsiri neno la lugha ya awali. Tunasoma kwamba nafsi zinaweza kuzaliwa. (Mwanzo 46:18) Watu wanaweza kula. (Mambo ya Walawi 7:20) Nafsi zinaweza kufunga. (Zaburi 35:13) Nafsi zinaweza kuzimika au kukamatwa. (Yona 2:7, Zaire Swahili Bible; Zaburi 7:5) Watu wanaweza kuibwa. (Kumbukumbu la Torati 24:7). Maneno “nafsi” na “mtu” yanamaanisha kitu kimoja.

7. Ni maandiko gani ya Biblia yanayoonyesha kwamba nafsi inaweza kufa?

7 Kwa kuwa nafsi ni mtu mwenyewe, mtu anapokufa, nafsi hufa pia. Andiko la Ezekieli 18:4 (ZSB) linasema: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” Pia, andiko la Matendo 3:23 linasema: “Kwa kweli, nafsi yoyote [au, mtu] isiyomsikiliza Nabii huyo itaangamizwa kabisa kutoka miongoni mwa watu.” Kwa hiyo nafsi si kitu kinachoendelea kuishi baada ya mwili kufa.

8. Roho iliyo ndani ya wanadamu ni nini?

8 Roho si sawa na nafsi. Roho ni nguvu ya uhai iliyo ndani ya wanadamu ambayo huwawezesha kutimiza shughuli za maisha. Roho ni kama umeme. Nguvu za umeme zinaweza kuzungusha upepeo au kufanya friji iwe baridi lakini umeme peke yake hauwezi kuzungusha hewa au kufanya vitu viwe baridi. Kwa njia hiyohiyo, roho yetu hutuwezesha kuona, kusikia, na kufikiri. Lakini roho peke yake haiwezi kufanya mambo hayo bila macho, masikio, au ubongo. Hiyo ndiyo sababu Biblia husema hivi kuhusu mwanadamu: “Pumzi [“roho,” NW] yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:4.

9. Ni nini ambacho nafsi na roho hazifanyi?

9 Kwa hiyo, kulingana na Biblia, nafsi na roho hazitoki mwilini mtu anapokufa na kuendelea kuishi katika makao ya roho.

Hali ya Wafu

10. Biblia inasema nini kuhusu hali ya wafu?

10 Hivyo, basi, wafu wako katika hali gani? Kwa kuwa Yehova ndiye aliyewaumba wanadamu, yeye pia anajua kile ambacho hutupata tunapokufa. Neno lake hufundisha kwamba wafu hawana uhai, hawawezi kusikia, kuona, kuongea, wala kufikiria chochote. Biblia inasema:

  • “Wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5.

  • “Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja.”—Mhubiri 9:6.

  • “Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko [kaburini] uendako wewe.”—Mhubiri 9:10.

11. Baada ya Adamu kufanya dhambi, Yehova alimwambia nini?

11 Fikiria yale ambayo Biblia inasema kuhusu mzazi wetu wa kwanza, Adamu. Yehova alimwumba Adamu “kwa mavumbi ya ardhi.” (Mwanzo 2:7) Kama Adamu angalitii sheria ya Yehova, angaliishi milele kwa furaha duniani. Hata hivyo, Adamu alivunja sheria ya Yehova, na adhabu ikawa kifo. Adamu alienda wapi alipokufa? Mungu alimwambia: ‘Utairudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.’—Mwanzo 3:19.

12. Ni nini kilichompata Adamu alipokufa?

12 Adamu alikuwa wapi kabla Yehova hajamwumba kutoka mavumbini? Hakuwapo. Kwa hiyo Yehova aliposema kwamba Adamu ‘angeirudia ardhi,’ Alimaanisha kwamba Adamu angerudi katika hali ya kukosa uhai kama vile mavumbi. Adamu hakuendelea kuishi katika ulimwengu wa roho. ‘Hakuiaga dunia’ kwenda katika makao ya roho ya wazazi wa kale. Hakuenda mbinguni wala motoni. Alirudi katika ile hali ya kutokuwa na uhai; hali ya kutokuwapo.

13. Ni nini huwapata wanadamu na wanyama wanapokufa?

13 Je, jambo hilo huwapata wanadamu kwa ujumla? Ndiyo. Biblia inaeleza: “[Wanadamu na wanyama] huendea mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.”—Mhubiri 3:19, 20.

14. Kuna tumaini gani kwa wafu?

14 Biblia inaahidi kwamba Mungu atawaamsha wafu waishi katika dunia paradiso. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Lakini jambo hilo litatukia wakati ujao. Wakati huu wafu wamelala usingizi wa kifo. (Yohana 11:11-14) Hatupaswi kuwaogopa wala kuwaabudu, kwa kuwa hawawezi kutusaidia wala kutudhuru.

15, 16. Shetani hujaribuje kufanya watu waamini kwamba wafu hawajakufa?

15 Fundisho kwamba hatufi ni uwongo ambao huenezwa na Shetani Ibilisi. Ili kuwafanya watu waamini uwongo huo, yeye na roho wake waovu hujaribu kuwadanganya watu waamini kwamba ugonjwa na matatizo mengine husababishwa na roho za wafu. Ni kweli kwamba matatizo fulani husababishwa na roho waovu. Pia ni kweli kwamba matatizo mengine hayasababishwi na roho waovu. Hata hivyo, si kweli kwamba wale wanaolala usingizi wa kifo wanaweza kutudhuru.

16 Kuna njia nyingine ambayo roho waovu hutumia kujaribu kuwadanganya watu wafikiri kwamba yale ambayo Biblia husema kuhusu kifo si kweli. Wao hudanganya watu wafikiri kwamba wameona wafu au kuongea nao. Roho waovu hufanya hivyo kupitia maono, ndoto, watu wanaowasiliana na roho, au njia nyinginezo. Hata hivyo, watu hawawasiliani na wafu, bali huwasiliana na roho waovu wanaojifanya kuwa watu waliokufa. Hiyo ndiyo sababu Yehova huwashutumu vikali watu ambao huwasiliana na roho na wale ambao hutafuta habari kutoka kwa wafu.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Zekaria 10:2.