Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 67

Kuta za Yerusalemu

Kuta za Yerusalemu

Acheni turudi nyuma miaka michache. Nehemia, mtumishi wa Mfalme Artashasta, alikuwa Mwisraeli aliyeishi katika jiji la Uajemi la Shushani. Ndugu ya Nehemia aliporudi kutoka Yuda, alimletea habari mbaya: ‘Watu waliorudi Yerusalemu hawana usalama. Malango na kuta za jiji zilizoharibiwa na Wababiloni hazijajengwa.’ Nehemia alisikitika. Alitaka kwenda Yerusalemu kuwasaidia, hivyo, akasali kwamba mfalme amruhusu aondoke.

Baadaye, mfalme akagundua kwamba Nehemia hakuwa na furaha. Akasema: ‘Sijawahi kukuona ukiwa umehuzunika. Kuna tatizo gani?’ Nehemia akamwambia: ‘Kwa nini nisihuzunike wakati jiji letu, Yerusalemu, limefanywa ukiwa?’ Mfalme akamwuliza hivi: ‘Ungependa nikufanyie nini?’ Mara moja, Nehemia akasali kimya-kimya. Kisha akamwambia: ‘Tafadhali, niruhusu niende kujenga upya kuta za Yerusalemu.’ Mfalme Artashasta akampa Nehemia ruhusa ya kwenda, na akamhakikishia kwamba atakuwa salama katika safari hiyo ndefu. Pia, akamfanya Nehemia kuwa gavana wa Yuda na kumpa mbao kwa ajili ya malango ya jiji.

Nehemia alipofika Yerusalemu, akachunguza kuta za jiji. Kisha akawakusanya makuhani na watawala na kuwaambia hivi: ‘Hali hii inasikitisha. Tunahitaji kufanya kazi.’ Watu wakakubali, na wakaanza kujenga upya kuta za jiji.

Lakini baadhi ya maadui wa Israeli waliwadhihaki, na kusema: ‘Mbweha anaweza kubomoa ukuta mnaojenga.’ Wafanyakazi walipuuza dhihaka zao na kuendelea kujenga. Basi ukuta ukaendelea kuwa mrefu na imara zaidi.

Maadui kutoka maeneo mbalimbali wakapanga kulishambulia jiji la Yerusalemu ghafula. Wayahudi waliposikia kuhusu mipango hiyo, wakaogopa sana. Lakini Nehemia akawaambia hivi: ‘Msiogope. Yehova yupo pamoja nasi.’ Akaweka walinzi kulinda wafanyakazi, na maadui wao hawakuweza kuwashambulia.

Katika siku 52 tu, ujenzi wa kuta na malango ukakamilika. Nehemia akawaleta Walawi wote Yerusalemu kwa ajili ya kuzindua ukuta huo. Akawapanga katika makundi mawili ya waimbaji. Wakapanda ukuta wakitumia ngazi zilizo kwenye Lango la Chemchemi na wakaenda pande tofauti kuzunguka jiji. Wakamwimbia Yehova kwa matoazi, vinanda, na vinubi. Ezra akaenda na kundi moja, na Nehemia akaenda na lile lingine, mpaka walipokutana hekaluni. Watu wote, yaani, wanaume, wanawake, na watoto, wakamtolea dhabihu Yehova na kusherehekea. Sauti zao za kushangilia zilisikika mbali sana.

“Silaha yoyote itakayofanywa dhidi yako haitafanikiwa.”​—Isaya 54:17