Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 83

Yesu Analisha Maelfu ya Watu

Yesu Analisha Maelfu ya Watu

Siku moja, muda mfupi kabla ya Pasaka ya mwaka wa 32 W.K., mitume walikuwa wametoka kwenye kampeni ya kuhubiri. Kwa kuwa walikuwa wamechoka, Yesu na mitume wake walipanda mashua kuelekea Bethsaida ili wakapumzike. Lakini mashua ilipokaribia ufukweni, Yesu akaona maelfu ya watu wakiwa wanamsubiri. Ingawa Yesu alitaka yeye na mitume wake wapate nafasi ya kuwa peke yao, aliwakaribisha watu hao kwa fadhili. Aliwaponya wagonjwa wao, na kisha akaanza kuwafundisha. Siku nzima, Yesu aliwafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. Ilipofika jioni, mitume wakamwambia hivi: ‘Bila shaka, watu wana njaa. Waache waende zao ili wakatafute chakula.’

Yesu akasema: ‘Si lazima waondoke. Ninyi wapeni chakula.’ Mitume wakauliza: ‘Unataka tukawanunulie mikate?’ Filipo, ambaye alikuwa mmoja wa mitume akasema hivi: ‘Hata ikiwa tungekuwa na pesa nyingi hatungeweza kununua mikate kwa ajili ya watu wote hawa.’

Yesu akauliza: ‘Tuna chakula kiasi gani?’ Andrea akamjibu: ‘Tuna mikate mitano na samaki wawili wadogo. Lakini kwa kweli chakula hicho hakitoshi.’ Yesu akasema: ‘Leteni hapa hiyo mikate na samaki.’ Kisha, akawaambia umati wakae kwenye vikundi vya watu 50 na 100. Yesu akachukua mikate na samaki, akatazama juu mbinguni, na kusali. Kisha, akawapatia mitume, nao wakawagawia watu. Wanaume 5,000 pamoja na wanawake na watoto waliokuwepo, wakala mpaka wakashiba. Baada ya hapo, mitume wakakusanya chakula kilichokuwa kimebaki, kwa hiyo hakuna chochote kilichotupwa. Wakajaza vikapu 12. Huo ulikuwa muujiza wa kustaajabisha, sivyo?

Watu walifurahi sana hivi kwamba wakataka kumfanya Yesu awe mfalme wao. Lakini Yesu alijua kwamba wakati wa Yehova kumweka awe mfalme haukuwa umefika. Kwa hiyo, akawaruhusu watu waondoke na kuwaagiza mitume waende upande ule mwingine wa Bahari ya Galilaya. Mitume walipanda mashua, lakini Yesu akaenda mlimani akiwa peke yake. Kwa nini? Kwa sababu alitaka kusali kwa Baba yake. Hata alipokuwa na mambo mengi sana, Yesu alitenga wakati wa kusali.

“Msifanye kazi kwa ajili ya chakula kinachoharibika, bali kwa ajili ya chakula kinachodumu kwa ajili ya uzima wa milele, ambacho Mwana wa binadamu atawapa ninyi.”​—Yohana 6:27