Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 85

Yesu Aponya Siku ya Sabato

Yesu Aponya Siku ya Sabato

Mafarisayo walimchukia Yesu, na walitafuta sababu za kumkamata. Walidai kwamba hakupaswa kuponya wagonjwa siku ya Sabato. Katika siku fulani ya Sabato, Yesu alikutana na mwanamume kipofu akiombaomba barabarani. Yesu akawaambia wanafunzi wake: ‘Oneni jinsi nguvu za Mungu zitakavyomponya mwanamume huyu.’ Yesu akatema mate kwenye udongo, kisha, akaupaka kwenye macho ya yule mwanamume. Halafu akamwambia: “Nenda ukanawe katika dimbwi la Siloamu.” Mwanamume huyo akafanya kama alivyoagizwa, na kwa mara ya kwanza maishani akaanza kuona.

Watu walishangaa sana. Wakawa wakiulizana hivi: ‘Je, huyu ni yule aliyekuwa akiketi na kuombaomba au ni mtu mwingine anayefanana naye?’ Mwanamume huyo akawajibu: ‘Ni mimi niliyezaliwa kipofu!’ Nao wakamuuliza: ‘Ulipataje kuona?’ Alipowasimulia jambo lililotokea, wakampeleka kwa Mafarisayo.

Mwanamume huyo akawaambia Mafarisayo hivi: ‘Yesu alinipaka udongo katika macho, kisha, akaniambia niende nikanawe. Nilifanya hivyo, na sasa ninaona.’ Mafarisayo wakasema: ‘Ikiwa Yesu anaponya siku ya Sabato, basi nguvu zake hazitoki kwa Mungu.’ Wengine wakasema: ‘Ikiwa nguvu zake hazitoki kwa Mungu, asingeweza kuponya.’

Mafarisayo wakawaita wazazi wa mtu huyo na kuwauliza: ‘Ni nini kilichofanya mtoto wenu aanze kuona?’ Wazazi waliogopa kwa sababu Mafarisayo walikuwa wamesema kwamba mtu yeyote atakayemwamini Yesu angefukuzwa katika sinagogi. Kwa hiyo, wakawajibu hivi: ‘Hatujui. Muulizeni mwenyewe.’ Mafarisayo wakaendelea kumuuliza maswali yule mwanaume, hatimaye akasema: ‘Nimewaambia kila kitu. Kwa nini mnaendelea kuniuliza?’ Mafarisayo wakakasirika na kuamua kumfukuza.

Yesu akamtafuta mwanamume huyo na alipompata akamuuliza hivi: ‘Je, unamwamini Masihi?’ Mtu huyo akamjibu: ‘Ikiwa ningemjua ningemwamini.’ Yesu akamwambia: ‘Mimi ndiye Masihi.’ Kwa kweli, Yesu alimtendea mtu huyo kwa fadhili, sivyo? Licha ya kumponya, alimsaidia kuwa na imani.

“Mnakosea, kwa sababu hamjui Maandiko wala nguvu za Mungu.” ​—Mathayo 22:29