Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 95

Hawakuvunjwa Moyo na Kitu Chochote

Hawakuvunjwa Moyo na Kitu Chochote

Mwanamume ambaye hangeweza kutembea alikuwa akiketi kwenye mwingilio wa lango la hekalu kila siku akiombaomba. Siku moja mchana, aliwaona Petro na Yohana wakienda hekaluni. Akawaambia: ‘Tafadhali ninaomba zawadi.’ Petro akamwambia: ‘Nina kitu bora cha kukupa zaidi ya fedha. Katika jina la Yesu simama na utembee!’ Kisha Petro akamsaidia kusimama, na mwanamume huyo akaanza kutembea! Umati ulifurahishwa sana na muujiza huo hivi kwamba watu wengi zaidi wakawa waamini.

Lakini makuhani na Masadukayo walikasirika. Waliwakamata mitume, wakawapeleka mahakamani, na kuwauliza: ‘Ni nani aliyewapa nguvu za kumponya mtu huyu?’ Petro akasema: ‘Tulipokea nguvu kutoka kwa Yesu Kristo, ambaye mlimwua.’ Viongozi wa kidini wakapaaza sauti: ‘Acheni kuzungumza kumhusu Yesu!’ Lakini mitume wakawaambia: Lazima tuzungumze kumhusu. Hatutaacha.’

Baada tu ya Petro na Yohana kuachiliwa huru, walienda kwa wanafunzi wengine na kuwaeleza kilichotukia. Wakasali pamoja, wakimwomba Yehova: ‘Tafadhali tusaidie tubaki imara ili tuendelee kufanya kazi yako.’ Yehova akawapa roho yake takatifu, na wakaendelea kuhubiri na kuponya. Watu wengi zaidi wakawa waamini. Masadukayo walikuwa na wivu sana hivi kwamba wakawakamata mitume na kuwatupa gerezani. Lakini wakati wa usiku, Yehova alimtuma malaika, ambaye alifungua milango ya gereza na kuwaambia mitume: ‘Rudini hekaluni, mkafundishe.’

Asubuhi iliyofuata, Sanhedrini, mahakama ya viongozi wa kidini, ikaambiwa: ‘Jela bado imefungwa, lakini wanaume mliowakamata hawapo! Wapo hekaluni wakiwafundisha watu!’ Kwa mara nyingine tena, mitume walikamatwa na kupelekwa mbele ya Sanhedrini. Kuhani mkuu akasema hivi: tuliwaagiza msizungumze kumhusu Yesu!’ Lakini Petro akajibu: ‘Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.’

Viongozi wa kidini walikasirika sana na wakataka kuwaua mitume. Lakini Farisayo aliyeitwa Gamalieli akasimama na kusema: ‘Iweni waangalifu! Huenda Mungu yupo pamoja na watu hawa. Je, kweli mnataka kupigana na Mungu?’ Wakasikiliza ushauri wake. Baada ya kuwapiga mitume kwa fimbo, wakawaagiza kwa mara nyingine waache kuhubiri, na kisha wakawaacha waende. Lakini hilo halikuwavunja moyo mitume. Waliendelea kwa ujasiri kuhubiri habari njema, katika hekalu na nyumba kwa nyumba.

“Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.”​—Matendo 5:29