Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 21

Pigo la Kumi

Pigo la Kumi

Musa alimwahidi Farao kwamba hangeenda kumwona tena. Lakini kabla hajaondoka, akamwambia Farao hivi: ‘Katikati ya usiku, kila mzaliwa wa kwanza nchini Misri, kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao mpaka mzaliwa wa kwanza wa watumwa, atakufa.’

Yehova aliwaambia Waisraeli watayarishe mlo wa pekee. Alisema hivi: ‘Chinjeni kondoo dume au mbuzi wa mwaka mmoja, kisha mpake damu yake kwenye mlango wa nyumba zenu. Chomeni nyama hiyo na kuila pamoja na mkate usiotiwa chachu. Vaeni nguo na viatu na muwe tayari kuondoka. Nitawakomboa usiku wa leo.’ Hebu wazia jinsi Waisraeli walivyofurahi!

Katikati ya usiku, malaika wa Yehova alienda katika kila nyumba nchini Misri. Mzaliwa wa kwanza katika nyumba yoyote ambayo haikuwa imepakwa damu mlangoni, alikufa. Lakini malaika huyo alipita nyumba zilizokuwa zimepakwa damu. Kila mzaliwa wa kwanza alikufa katika familia zote nchini Misri, iwe ni za matajiri au maskini. Lakini hakuna mtoto Mwisraeli aliyekufa.

Hata mwana wa Farao mwenyewe alikufa. Farao hangeweza kuvumilia tena. Papo hapo akamwambia Musa na Haruni hivi: ‘Simameni. Ondokeni hapa. Nendeni mkamwabudu Mungu wenu. Chukueni wanyama wenu na mwende kabisa!’

Usiku huo, kukiwa na mwezi mpevu, Waisraeli waliondoka Misri wakiwa wamepangwa kulingana na familia na makabila yao. Kulikuwa na wanaume Waisraeli 600,000, pamoja na wanawake wengi na watoto. Pia, watu wengine wengi waliambatana nao ili wamwabudu Yehova. Hatimaye, Waisraeli walikuwa huru!

Ili kukumbuka jinsi ambavyo Yehova aliwakomboa, kila mwaka wangetayarisha mlo huo wa pekee. Mlo huo uliitwa Pasaka.

“Kwa sababu hii nimekuacha ubaki: ili nionyeshe nguvu zangu kuhusiana na wewe na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.”​—Waroma 9:17