Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 28

Punda wa Balaamu Azungumza

Punda wa Balaamu Azungumza

Waisraeli walikuwa wamekaa nyikani kwa karibu miaka 40. Walikuwa wameshinda miji mingi yenye nguvu. Sasa, wakiwa wamepiga kambi kwenye nyanda za Moabu mashariki ya Mto Yordani, wakati ulikuwa umefika wa kuingia katika Nchi ya Ahadi. Balaki, mfalme wa Moabu, aliogopa kwamba wangemyang’anya nchi yake. Kwa hiyo, akamwomba mwanamume anayeitwa Balaamu aje Moabu ili awalaani Waisraeli.

Lakini Yehova akamwambia Balaamu: ‘Usiwalaani Waisraeli.’ Kwa hiyo, Balaamu akakataa kwenda Moabu. Mfalme Balaki akamwalika mara ya pili na akamwahidi atampa chochote alichotaka. Lakini bado Balaamu akakataa. Kisha Mungu akamwambia hivi: ‘Unaweza kwenda, lakini useme tu jambo ambalo nitakuambia useme.’

Balaamu akapanda punda wake na kwenda upande wa kusini kuelekea Moabu. Alipanga kuwalaani Waisraeli, hata ingawa Yehova alikuwa amemwambia asifanye hivyo. Malaika wa Yehova akatokea barabarani mara tatu. Ingawa Balaamu hakumwona malaika huyo, punda wake alimwona. Mara ya kwanza, punda akatoka barabarani na kuingia shambani. Mara ya pili, punda akaanza kujifinya kwenye ukuta wa mawe na hivyo kuufinya mguu wa Balaamu ukutani. Mara ya mwisho, punda akalala katikati ya barabara. Kila mara, Balaamu alimpiga punda wake kwa fimbo.

Baada ya mara ya tatu, Yehova akamfanya punda azungumze. Punda akamuuliza Balaamu hivi: ‘Kwa nini unaendelea kunipiga?’ Balaamu akasema: ‘Umenitendea kama mjinga. Ikiwa ningekuwa na upanga ningekuua.’ Punda akasema: ‘Nimekuwa nikikubeba kwa miaka mingi. Je, nimewahi kukutendea hivi?’

Kisha Yehova akamruhusu Balaamu amwone malaika. Malaika akasema hivi: ‘Yehova alikuonya usiende kuwalaani Waisraeli.’ Balaamu akasema: ‘Nimekosea. Nitarudi nyumbani.’ Lakini malaika akasema: ‘Unaweza kwenda Moabu, lakini useme tu kile ambacho Yehova atakuambia useme.’

Je, Balaamu alikuwa amejifunza jambo lolote? Hapana. Baada ya hapo, Balaamu alijaribu kuwalaani Waisraeli mara tatu, lakini mara zote tatu Yehova akamfanya awabariki. Mwishowe, Waisraeli wakashambulia Moabu, na Balaamu akauawa. Je, haingekuwa afadhali ikiwa Balaamu angemsikiliza Yehova tangu mwanzo?

“Mjilinde na kila aina ya pupa, kwa sababu hata mtu anapokuwa na vitu vingi uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.”​—Luka 12:15