Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 36

Ahadi ya Yeftha

Ahadi ya Yeftha

Waisraeli walimwasi tena Yehova na kuanza kuabudu miungu ya uwongo. Hata hivyo, miungu hiyo haikuwasaidia waliposhambuliwa na Waamoni. Waisraeli waliteseka kwa miaka mingi. Hatimaye, wakamwambia hivi Yehova: ‘Tumekutendea dhambi. Tafadhali tuokoe kutoka kwa adui zetu.’ Kisha, wakaziharibu sanamu zao na kuanza tena kumtumikia. Yehova hakutaka kuona wakiendelea kuteseka.

Shujaa aliyeitwa Yeftha alichaguliwa ili awaongoze Waisraeli kupigana na Waamoni. Yeftha alimwahidi Yehova hivi: ‘Ukitusaidia kushinda vita hivi, nitakaporudi nyumbani, nitakupa mtu wa kwanza kuja kunipokea.’ Yehova alisikiliza sala ya Yeftha na akamsaidia kushinda vita.

Yeftha aliporudi nyumbani, binti yake, mtoto wake pekee, ndiye alikuwa mtu wa kwanza kuja kumpokea. Alikuwa akicheza dansi na kupiga tari. Yeftha angefanya nini? Alikumbuka ahadi yake na kusema hivi: ‘Ole, binti yangu! Umenivunja moyo. Nilitoa ahadi kwa Yehova. Ili kuitimiza, ninapaswa kukupeleka Shilo ukatumikie kwenye maskani.’ Binti yake akamwambia hivi: ‘Baba, ikiwa umetoa ahadi kwa Yehova, unapaswa kuitimiza. Ninaomba uniruhusu niende milimani na rafiki zangu wa kike kwa miezi miwili. Baada ya hapo nitaenda Shilo.’ Binti ya Yeftha alitumikia kwa uaminifu kwenye maskani muda wote wa maisha yake. Kila mwaka rafiki zake walienda kumtembelea.

“Anayempenda baba au mama kuliko anavyonipenda hanistahili.”​—Mathayo 10:37