Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya Kumi na Tisa

Kaa Katika Upendo wa Mungu

Kaa Katika Upendo wa Mungu
  • Kumpenda Mungu kunamaanisha nini?

  • Tunawezaje kukaa katika upendo wa Mungu?

  • Yehova atawathawabishaje wale wanaokaa katika upendo wake?

Je, utamfanya Yehova awe kimbilio lako katika nyakati hizi zenye msukosuko?

1, 2. Tunaweza kupata wapi kimbilio salama leo?

WAZIA kwamba unatembea barabarani siku yenye dhoruba kali. Mawingu yanazidi kutanda. Radi inapiga na ngurumo zinasikika, kisha mvua kubwa inanyesha. Unakimbia huku na huku ukitafuta mahali pa kujikinga. Halafu, ng’ambo ya barabara unaona mahali pa kujikinga. Ni mahali imara, pakavu, na penye kuvutia. Unafurahi kama nini kupaona mahali hapo!

2 Tunaishi katika nyakati zenye msukosuko. Hali za ulimwengu zinaendelea kuzorota. Hata hivyo, kuna mahali salama, kimbilio linaloweza kutukinga. Ni wapi tunapoweza kupata kimbilio hilo? Biblia inafundisha hivi: “Nitamwambia Yehova: ‘Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtegemea.’”—Zaburi 91:2.

3. Tunawezaje kumfanya Yehova kuwa kimbilio letu?

3 Hebu wazia! Yehova, Muumba anayeutawala ulimwengu mzima, anaweza kuwa kimbilio letu. Anaweza kutulinda kwa kuwa yeye ana nguvu nyingi kuliko yeyote au chochote kinachoweza kutuumiza. Hata tukiumizwa, Yehova anaweza kuondoa madhara yote mabaya. Tunawezaje kumfanya Yehova kuwa kimbilio letu? Tunahitaji kumtumaini. Isitoshe, Neno la Mungu linatusihi: “Jitunzeni katika upendo wa Mungu.” (Yuda 21) Ndiyo, tunahitaji kukaa katika upendo wa Mungu kwa kudumisha kifungo cha upendo pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Ndipo tunapoweza kuwa na hakika kwamba yeye ni kimbilio letu. Tunawezaje kudumisha kifungo hicho?

ZINGATIA UPENDO WA MUNGU NA KUTENDA KUPATANA NAO

4, 5. Taja baadhi ya njia ambazo Yehova ameonyesha upendo kwetu.

4 Ili tuendelee kukaa katika upendo wa Mungu, tunapaswa kutambua jinsi Yehova ametuonyesha upendo wake. Fikiria baadhi ya mafundisho ya Biblia ambayo umejifunza katika kitabu hiki. Akiwa Muumba, Yehova ametupatia dunia iwe makao yetu yenye kupendeza. Ameijaza chakula na maji mengi, mali za asili, wanyama wenye kuvutia, na mandhari maridadi. Akiwa Mtungaji wa Biblia, Mungu ametujulisha jina lake na sifa zake. Isitoshe, Neno lake husema kwamba alimtuma Mwana wake mpendwa duniani na kuruhusu ateseke na kufa kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Zawadi hiyo ina maana gani kwetu? Inatupa tumaini la kuwa na maisha mazuri wakati ujao.

5 Pia tumaini letu la wakati ujao linategemea jambo fulani ambalo Mungu amefanya. Yehova amesimamisha serikali ya kimbingu, Ufalme wa Kimasihi. Karibuni itakomesha mateso yote na kuifanya dunia iwe paradiso. Hebu wazia! Tunaweza kuishi humo tukiwa na amani na furaha milele. (Zaburi 37:29) Kwa sasa, Mungu ametupa mwongozo wa kuishi maisha bora zaidi sasa. Pia ametupa zawadi ya sala, inayotusaidia kuwasiliana naye wakati wowote. Hizo ni baadhi ya njia chache tu ambazo Yehova ameonyesha upendo kwa wanadamu wote kwa ujumla na kwako wewe binafsi.

6. Unawezaje kuonyesha kwamba unathamini upendo ambao Yehova amekuonyesha?

6 Hebu fikiria swali hili: Nitaonyeshaje kwamba ninathamini upendo wa Yehova? Huenda wengi wakajibu, “Kwa kumpenda pia.” Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Yesu alisema kwamba hii ndiyo amri kuu zaidi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Bila shaka una sababu nyingi za kumpenda Yehova Mungu. Lakini je, kuhisi tu kwamba una upendo huo kunatosha kuonyesha kwamba unampenda Yehova kwa moyo, nafsi, na akili yako yote?

7. Je, kumpenda Mungu ni kuwa na hisia tu? Eleza.

7 Kama Biblia inavyoonyesha, kumpenda Mungu si hisia tu. Ingawa ni muhimu kuhisi kwamba unampenda Yehova, huo ni mwanzo tu wa kumpenda kikweli. Mti wa matunda hutokana na mbegu. Ikiwa unataka kula tunda, je, utatosheka tu mtu akikupa mbegu ya tunda hilo? Hapana! Vivyo hivyo, kuhisi kwamba unampenda Yehova Mungu ni mwanzo tu. Biblia inafundisha: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Ili tumpende Mungu kikweli, lazima tuzae matunda mazuri. Ni lazima tuonyeshe kwa matendo kwamba tunampenda.—Mathayo 7:16-20.

8, 9. Tunawezaje kuonyesha upendo na shukrani kwa Mungu?

8 Tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu tunaposhika amri zake na kufuata kanuni zake. Si vigumu kufanya hivyo. Sheria za Yehova si nzito bali zimekusudiwa kutusaidia kuishi maisha mazuri, yenye furaha, na yenye kuridhisha. (Isaya 48:17, 18) Tunapoishi kupatana na mwongozo wa Yehova, tunamwonyesha Baba yetu wa mbinguni kwamba tunathamini kikweli yale yote ambayo ametufanyia. Inasikitisha kwamba ni watu wachache ulimwenguni leo wenye uthamini kama huo. Hatutaki kukosa uthamini kama watu fulani walioishi wakati Yesu alipokuwa duniani. Yesu aliwaponya watu kumi wenye ukoma, lakini ni mmoja tu aliyerudi kumshukuru. (Luka 17:12-17) Bila shaka tungependa kuwa wenye shukrani kama yule mtu mmoja wala si kama wale wengine tisa wasio na shukrani!

9 Ni amri gani za Yehova tunazopaswa kutii? Tumezungumzia amri kadhaa katika kitabu hiki, hebu tujikumbushe chache. Kutii amri za Mungu kutatusaidia kukaa katika upendo wa Mungu.

MKARIBIE YEHOVA ZAIDI

10. Eleza kwa nini ni muhimu kuendelea kupata ujuzi juu ya Yehova Mungu.

10 Kujifunza juu ya Yehova ni hatua muhimu ya kumkaribia. Ni hatua inayopaswa kuendelea daima. Tuseme unaota moto wakati wa usiku wenye baridi, je, ungeuacha moto huo ufifie na kuzimika? Hapana. Utaendelea kuongeza kuni ili moto uendelee kuwaka. Huenda uhai wako unautegemea! Sawa na vile kuni huchochea moto, ndivyo “kumjua Mungu” kunavyoimarisha upendo wetu kwa Yehova.—Methali 2:1-5.

Kama moto, Upendo wako kwa Yehova unahitaji kuchochewa ili uendelee kuwaka

11. Mafundisho ya Yesu yalikuwa na matokeo gani kwa wanafunzi wake?

11 Yesu alitaka wanafunzi wake waendelee kuimarisha upendo wao kwa Yehova na Neno lake la kweli lenye thamani. Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wawili baadhi ya unabii ulio katika Maandiko ya Kiebrania ambao ulitimizwa maishani mwake. Matokeo yakawaje? Baadaye walisema hivi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia Maandiko?”—Luka 24:32.

12, 13. (a) Upendo wa watu wengi ulimwenguni kumwelekea Mungu na Biblia ukoje? (b) Tunawezaje kuendeleza upendo wetu?

12 Ulipojifunza kwa mara ya kwanza mambo ambayo Biblia inafundisha hasa, je, hukufurahi sana, ukawa na bidii na upendo mwingi sana kumwelekea Mungu? Bila shaka. Wengi wamehisi hivyo. Kazi kubwa sasa ni kuendelea kukuza na kuimarisha upendo huo. Hatutaki kuuiga ulimwengu. Yesu alitabiri hivi: “Upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Unawezaje kuendelea kumpenda Yehova na kweli zake zilizo katika Biblia?

13 Endelea kupata ujuzi juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Tafakari au fikiria kwa uzito mambo unayojifunza katika Neno la Mungu, na ujiulize: ‘Mambo hayo yananifundisha nini juu ya Yehova Mungu? Yananisaidiaje kumpenda Yehova zaidi kwa moyo, akili, na nafsi yangu yote?’ (1 Timotheo 4:15) Kutafakari juu ya mambo hayo kutakufanya umpende Yehova zaidi.

14. Sala inawezaje kutusaidia kuendelea kukaa katika upendo wa Yehova?

14 Njia nyingine ya kuimarisha upendo wako kwa Yehova ni kusali kwa ukawaida. (1 Wathesalonike 5:17) Katika Sura ya 17 ya kitabu hiki tulijifunza kwamba sala ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Kama vile uhusiano kati ya wanadamu husitawi kwa sababu ya kuwasiliana kwa uhuru na kwa ukawaida, uhusiano wetu na Yehova hukua na kuimarika tunaposali kwa ukawaida. Hatupaswi kusali kidesturi tu, tukirudia-rudia maneno yaleyale bila hisia wala maana yoyote. Tunapaswa kuzungumza na Yehova kama vile mtoto anavyozungumza na baba anayempenda. Bila shaka, tunataka kuzungumza kwa heshima, lakini waziwazi, kwa unyoofu, na kutoka moyoni. (Zaburi 62:8) Ndiyo, funzo la Biblia la kibinafsi na sala inayotoka moyoni ni mambo muhimu katika ibada yetu, nayo hutusaidia kuendelea kukaa katika upendo wa Mungu.

UWE NA SHANGWE KATIKA IBADA

15, 16. Kwa nini tuione kazi ya kuhubiri Ufalme kuwa pendeleo na hazina?

15 Funzo la Biblia la kibinafsi na sala ni matendo ya ibada ambayo tunaweza kufanya faraghani. Hata hivyo, na tuchunguze sehemu moja ya ibada yetu tunayofanya hadharani, yaani, kuzungumza na wengine kuhusu imani yetu. Je, tayari umezungumza na watu fulani kuhusu kweli za Biblia? Ikiwa ndivyo, haikosi umefurahia kufanya hivyo. (Luka 1:74) Tunapozungumza na wengine kweli ambazo tumejifunza juu ya Yehova Mungu, tunatimiza mgawo muhimu sana ambao Wakristo wote wa kweli wamekabidhiwa, yaani, mgawo wa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

16 Mtume Paulo aliiona huduma yake kuwa yenye thamani sana, aliiita hazina. (2 Wakorintho 4:7) Kazi bora unayoweza kufanya ni kuzungumza na watu juu ya Yehova Mungu na makusudi yake. Yeye ndiye Bwana bora zaidi, na kumtumikia huleta faida zisizo na kifani. Kwa kufanya kazi hiyo, unawasaidia watu wenye mioyo minyoofu wamkaribie Baba yetu wa mbinguni na kutembea katika barabara ya uzima wa milele! Hakuna kazi yenye kuridhisha kama hiyo. Isitoshe, kuhubiri juu ya Yehova na Neno lake huongeza imani yako na kuimarisha upendo wako kwake. Na Yehova anathamini jitihada zako. (Waebrania 6:10) Kufanya kazi hiyo kwa bidii kutakusaidia kuendelea kukaa katika upendo wa Mungu.—1 Wakorintho 15:58.

17. Kwa nini huduma ya Kikristo ni muhimu leo?

17 Tunapaswa kukumbuka kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme ni muhimu sana. Biblia inasema: “Lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii.” (2 Timotheo 4:2) Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo leo? Neno la Mungu linatuambia: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu. Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” (Sefania 1:14) Ndiyo, wakati wa Yehova kuharibu mfumo huu wote wa mambo unakaribia sana. Watu wanapaswa kuonywa! Wanapaswa kujua kwamba huu ndio wakati wa kumchagua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu wao. Mwisho ‘hautachelewa.’—Habakuki 2:3.

18. Kwa nini tumwabudu Yehova pamoja na Wakristo wa kweli?

18 Yehova anataka tumwabudu pamoja na Wakristo wa kweli. Ndiyo sababu Neno lake linasema hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Tunapokusanyika pamoja na waamini wenzetu katika mikutano ya Kikristo, tuna nafasi nzuri ya kumsifu na kumwabudu Mungu wetu tunayempenda. Pia tunajengana na kutiana moyo.

19. Tunawezaje kuimarisha vifungo vya upendo katika kutaniko la Kikristo?

19 Tunaposhirikiana na waabudu wa Yehova, tunaimarisha vifungo vya upendo na urafiki kutanikoni. Tunapaswa kuzingatia wema wa wengine, kama Yehova anavyozingatia wema wetu. Usitazamie waamini wenzako wawe wakamilifu. Kumbuka kwamba wote wamefikia viwango tofauti vya ukomavu wa kiroho, na kwamba kila mmoja wetu hufanya makosa. (Wakolosai 3:13) Jitahidi kufanya urafiki na wale wanaompenda Yehova sana, nawe utafanya maendeleo ya kiroho. Ndiyo, kumwabudu Yehova pamoja na ndugu na dada zako wa kiroho kutakusaidia kukaa katika upendo wa Mungu. Yehova huwathawabishaje wale wanaomwabudu kwa uaminifu na kukaa katika upendo wake?

JITAHIDI KUPATA “UZIMA ULIO WA KWELI”

20, 21. “Uzima ulio wa kweli” ni nini, na kwa nini tumaini hilo ni zuri?

20 Yehova huwathawabisha watumishi wake waaminifu kwa kuwapa uzima, au uhai. Hata hivyo, ni uhai wa aina gani? Je, kweli uko hai sasa? Wengi wetu wangejibu, “Ndiyo.” Kwani, si tunapumua, tunakula, na kunywa? Bila shaka, tuko hai. Na tunapokuwa na furaha, huenda tukasema, “Haya ndiyo maisha!” Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba, katika maana halisi, hakuna mwanadamu yeyote ambaye ana uzima wa kweli.

Yehova angependa upate “uzima ulio wa kweli.” Je, utaupata?

21 Neno la Mungu linatuhimiza ‘tuushike imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Timotheo 6:19) Maneno hayo yanaonyesha kwamba tuna tumaini la kupata “uzima ulio wa kweli” wakati ujao. Ndiyo, tutakapokuwa wakamilifu, tutakuwa na uzima wa kweli, kwa maana tutaishi kama Mungu alivyokusudia tuishi. Tutakapoishi katika paradiso duniani tukiwa na afya kamili, amani, na furaha, ndipo tutakapofurahia “uzima ulio wa kweli”—uzima wa milele. (1 Timotheo 6:12) Je, hilo si tumaini zuri?

22. Unawezaje ‘kushika imara uzima ulio wa kweli’?

22 Tunawezaje ‘kushika imara uzima ulio wa kweli’? Akizungumzia jambo hilohilo, Paulo aliwahimiza Wakristo “wafanye mema” na “wawe matajiri katika matendo mazuri.” (1 Timotheo 6:18) Basi, ni wazi kwamba tunahitaji kutumia kweli ambazo tumejifunza katika Biblia. Lakini je, Paulo alimaanisha kwamba “uzima ulio wa kweli” ni malipo ya kutenda mema? Hapana, kwa maana tumaini hilo zuri hutegemea “fadhili zisizostahiliwa” kutoka kwa Mungu. (Waroma 5:15) Hata hivyo, Yehova anapenda kuwathawabisha wale wanaomtumikia kwa uaminifu. Angependa upate “uzima ulio wa kweli.” Wale wanaokaa katika upendo wa Mungu ndio watakaopata uzima huo wa milele, wenye furaha na amani.

23. Kwa nini ni muhimu kukaa katika upendo wa Mungu?

23 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, ninamwabudu Mungu kupatana na maagizo yake yaliyo katika Biblia?’ Ikiwa tunafanya hivyo kila siku, basi tunatembea katika njia inayofaa. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ni kimbilio letu. Atawaokoa watu wake waaminifu katika siku hizi za mwisho zenye taabu za mfumo huu wa kale wa mambo. Pia, Yehova atatukomboa na kutuingiza katika mfumo mpya mtukufu ulio karibu. Tutakuwa na shangwe iliyoje kuishi wakati huo! Na tutakuwa na furaha iliyoje kwa kuwa tulifanya maamuzi yanayofaa katika siku hizi za mwisho! Ukifanya maamuzi yanayofaa sasa, utapata “uzima ulio wa kweli,” uzima ambao Yehova Mungu alikusudia, kwa umilele wote!