Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Siku ya Hukumu Ni Nini?

Siku ya Hukumu Ni Nini?

UNA maoni gani kuhusu Siku ya Hukumu? Watu wengi hufikiri kwamba mabilioni ya watu watasimamishwa mmoja-mmoja mbele ya kiti cha enzi cha Mungu. Kisha kila mmoja wao atahukumiwa. Baadhi yao wataishi kwa raha mbinguni, na wengine watateswa milele. Hata hivyo, masimulizi ya Biblia kuhusu hukumu ni tofauti kabisa. Kulingana na Neno la Mungu, si wakati wenye kutisha bali ni wakati wa tumaini na kurudisha hali nzuri.

Mtume Yohana anafafanua hivi Siku ya Hukumu katika Ufunuo 20:11, 12: “Nikaona kiti cha ufalme kikubwa cheupe na yeye aliyeketi juu yake. Dunia na mbingu zikakimbia kutoka mbele zake, na mahali popote hapakupatikana kwa ajili ya hizo. Nami nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya kile kiti cha ufalme, na vitabu vya kukunjwa vikafunguliwa. Lakini kitabu kingine cha kukunjwa kikafunguliwa; hicho ni kitabu cha uzima. Na wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika vile vitabu kulingana na matendo yao.” Hukumu hiyo itatekelezwa na nani?

Yehova Mungu ndiye Hakimu au Mwamuzi mkuu wa wanadamu. Hata hivyo, ana mwakilishi wa kufanya hukumu. Kulingana na Matendo 17:31, mtume Paulo alisema kwamba Mungu “ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi.” Hakimu huyo aliyewekwa rasmi ni Yesu Kristo aliyefufuliwa. (Yohana 5:22) Hata hivyo, Siku ya Hukumu itaanza lini? Itakuwa na urefu gani?

Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba Siku ya Hukumu itaanza baada ya vita vya Har–Magedoni, wakati ambapo mfumo wa Shetani utaharibiwa. * (Ufunuo 16:14, 16; 19:19–20:3) Baada ya Har–Magedoni, Shetani na roho wake waovu watafungiwa katika abiso kwa miaka 1,000. Wakati huo, wale 144,000 watahukumu na kutawala “wakiwa wafalme pamoja na Kristo kwa miaka elfu.” (Ufunuo 14:1-3; 20:1-4; Waroma 8:17) Siku ya Hukumu haitakuwa tukio la haraka la saa 24. Itachukua miaka 1,000.

Katika kipindi hicho cha miaka 1,000, Yesu Kristo ‘atahukumu walio hai na wafu.’ (2 Timotheo 4:1) “Walio hai” watakuwa “umati mkubwa” utakaookoka Har–Magedoni. (Ufunuo 7:9-17) Mtume Yohana aliwaona pia “wafu . . . wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi” cha hukumu. Kama alivyoahidi Yesu, “waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Kristo] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Watahukumiwa kwa msingi gani?

Katika njozi, mtume Yohana aliona ‘vitabu vya kukunjwa vikifunguliwa na wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika vile vitabu kulingana na matendo yao.’ Je, vitabu hivyo vya kukunjwa ni rekodi ya mambo ambayo watu walifanya zamani? Hapana, watu hawatahukumiwa kulingana na mambo ambayo walifanya kabla ya kufa. Tunajuaje? Biblia inasema: “Yeye ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” (Waroma 6:7) Hivyo, ni kana kwamba wale watakaofufuliwa wataanza upya. Kwa hiyo, vitabu vya kukunjwa vinawakilisha matakwa mengine ya Mungu. Ili waishi milele, wale watakaookoka Har–Magedoni na wale watakaofufuliwa watahitaji kutii amri za Mungu kutia ndani matakwa yoyote mapya ambayo huenda Yehova akafunua katika ile miaka 1,000. Hivyo, watu watahukumiwa kulingana na yale watakayotenda katika Siku ya Hukumu.

Wakati wa Siku ya Hukumu, mabilioni ya watu watapata fursa ya kujifunza kwa mara ya kwanza mapenzi ya Mungu na kuishi kupatana nayo. Hivyo, kutakuwa na kazi kubwa ya kuwaelimisha watu. “Wakaaji wa nchi yenye kuzaa hakika watajifunza uadilifu.” (Isaya 26:9) Hata hivyo, si wote watakaofanya mapenzi ya Mungu. Andiko la Isaya 26:10 linasema: “Hata mwovu akionyeshwa kibali, yeye hatajifunza uadilifu. Atatenda isivyo haki katika nchi ya unyoofu, naye hatauona ukuu wa Yehova.” Waovu hao wataangamizwa milele wakati wa Siku ya Hukumu.—Isaya 65:20.

Mwishoni mwa Siku ya Hukumu, wale wanadamu wengine ‘watakuwa hai’ kikamili kwa sababu watakuwa wakamilifu. (Ufunuo 20:5) Hivyo, katika Siku ya Hukumu, wanadamu watarudishwa katika hali ya ukamilifu waliyokuwa nayo mwanzoni. (1 Wakorintho 15:24-28) Kisha kutakuwa na jaribu la mwisho. Shetani atafunguliwa kutoka katika abiso na kuruhusiwa ajaribu kuwapotosha wanadamu kwa mara ya mwisho. (Ufunuo 20:3, 7-10) Wale watakaompinga wataona utimizo kamili wa ahadi hii ya Biblia: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Ndiyo, Siku ya Hukumu itakuwa baraka kwa wanadamu wote waaminifu!

^ fu. 1 Kuhusu Har–Magedoni, tafadhali angalia Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 594-595, 1037-1038 au Étude Perspicase, Buku la 1, ukurasa wa 1073-1075, Buku la 2, ukurasa wa 63-64; na sura ya 20 ya kitabu Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.