Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 47

Je, Uko Tayari Kubatizwa?

Je, Uko Tayari Kubatizwa?

Tayari umejifunza mambo mengi kumhusu Yehova katika funzo lako la Biblia. Labda umefanya mabadiliko fulani ili kufuata mambo uliyojifunza. Hata hivyo, huenda kuna sababu inayokuzuia kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Katika somo hili, tutazungumzia baadhi ya mambo yanayoweza kumzuia mtu kubatizwa na jinsi unavyoweza kushinda changamoto hizo.

1. Unahitaji kuwa na ujuzi mwingi kadiri gani kabla ya kubatizwa?

Ili ubatizwe, unahitaji kuwa na “ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Hilo halimaanishi kwamba kabla ya kubatizwa unapaswa kujua majibu ya maswali yote ya Biblia ambayo huenda watu wakakuuliza. Hata Wakristo ambao walibatizwa miaka mingi iliyopita bado wanaendelea kujifunza. (Wakolosai 1:9, 10) Lakini unahitaji kuelewa mafundisho ya msingi ya Biblia. Wazee wa kutaniko watakusaidia kujua ikiwa una ujuzi wa kutosha.

2. Unapaswa kuchukua hatua gani kabla ya kubatizwa?

Kabla ya kubatizwa, unapaswa ‘kutubu na kugeuka.’ (Soma Matendo 3:19.) Hilo linamaanisha kwamba unajuta sana kwa sababu ya dhambi ulizofanya zamani na unamwomba Yehova akusamehe. Vilevile, unaepuka kabisa mwenendo mbaya na kuazimia kuishi maisha yanayomfurahisha Mungu. Isitoshe, unaanza kushirikiana na kutaniko kwa kuhudhuria mikutano na kuhubiri ukiwa mhubiri ambaye hajabatizwa.

3. Kwa nini hupaswi kuruhusu woga ukuzuie?

Huenda wengine wakahisi kwamba hawawezi kuishi kulingana na ahadi waliyomtolea Yehova. Ni kweli kwamba wakati mwingine utakosea, kama ilivyokuwa kwa wanaume na wanawake waaminifu wanaotajwa katika Biblia. Lakini Yehova hatarajii watumishi wake wawe wakamilifu. (Soma Zaburi 103:13, 14.) Anafurahi kuona ukijitahidi kufanya mambo mazuri kulingana na uwezo wako, naye atakusaidia! Yehova anatuhakikishia kwamba hakuna kitu ‘kinachoweza kututenga na upendo wake.’​—Soma Waroma 8:38, 39.

CHIMBA ZAIDI

Ona jinsi kumjua Yehova vizuri zaidi na kukubali msaada wake kunavyoweza kukusaidia kushinda mambo ambayo yanaweza kukuzuia kubatizwa.

4. Mjue Yehova vizuri zaidi

Unahitaji kumjua Yehova vizuri kadiri gani kabla ya kubatizwa? Unahitaji kuwa na ujuzi unaokuchochea kumpenda na kutamani kumfurahisha. Onyesha VIDEO ili uone jinsi ambavyo wanafunzi wa Biblia ulimwenguni pote wamefanya hivyo. Kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Katika video hiyo, ni nini kilichowasaidia wanafunzi hao wa Biblia wajitayarishe kwa ajili ya ubatizo?

Soma Waroma 12:2, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, una shaka yoyote kuhusu mafundisho ya Biblia au ikiwa Mashahidi wa Yehova wanafundisha ukweli?

  • Ikiwa una shaka, unaweza kufanya nini?

5. Shinda mambo yanayoweza kukuzuia kubatizwa

Tunapoamua kujiweka wakfu na kubatizwa, sisi sote hukabili changamoto. Ili kuona mfano, onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, Narangerel alihitaji kushinda vizuizi gani ili aanze kumtumikia Yehova?

  • Kumpenda Yehova kulimsaidiaje kushinda vizuizi hivyo?

Soma Methali 29:25 na 2 Timotheo 1:7, kisha mzungumzie swali hili:

  • Tutapata wapi ujasiri wa kushinda vizuizi?

6. Uwe na hakika kwamba Yehova atakusaidia

Yehova atakusaidia kufanya mambo yanayomfurahisha. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, ni nini kilichofanya mwanafunzi huyo wa Biblia asite kubatizwa?

  • Alijifunza jambo gani ambalo lilimsaidia kumtegemea Yehova zaidi?

Soma Isaya 41:10, 13, kisha mzungumzie swali hili:

  • Unawezaje kuwa na hakika kwamba utatimiza ahadi unayotoa unapojiweka wakfu?

7. Onyesha shukrani kwa upendo ambao Yehova amekuonyesha

Kadiri unavyozidi kufikiria jinsi Yehova anavyokupenda, ndivyo utakavyozidi kuwa mwenye shukrani na kutamani kuendelea kumtumikia milele. Soma Zaburi 40:5, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ni baraka gani kutoka kwa Yehova ambazo hasa zinakuchochea kumshukuru?

Nabii Yeremia alimpenda Yehova na neno lake, na alithamini sana kuwa na pendeleo la kutangaza jina la Yehova. Alisema hivi: “Neno lako likawa furaha na shangwe ya moyo wangu, kwa maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Yehova Mungu.” (Yeremia 15:16) Jibu maswali haya:

  • Kwa nini ni pendeleo la pekee kuwa Shahidi wa Yehova?

  • Je, ungependa kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova?

  • Je, kuna jambo lolote linalokuzuia kubatizwa?

  • Unafikiri unahitaji kufanya nini ili ufikie lengo la kubatizwa?

WATU FULANI HUSEMA: “Ninaogopa kwamba nikibatizwa nitashindwa kutimiza mambo ambayo niliahidi.”

  • Je, unahisi hivyo?

MUHTASARI

Yehova atakusaidia ushinde jambo lolote linalokuzuia kubatizwa.

Ungejibuje?

  • Unahitaji ujuzi mwingi kadiri gani kuhusu Biblia kabla ya kubatizwa?

  • Huenda ukahitaji kufanya mabadiliko gani kabla ya kubatizwa?

  • Kwa nini hupaswi kuruhusu woga ukuzuie kubatizwa?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza mambo ambayo yanapaswa kuwa msingi wa uamuzi wako wa kubatizwa.

“Je, Uko Tayari Kubatizwa?” (Mnara wa Mlinzi, Machi 2020)

Jifunze jinsi ya kushinda changamoto hususa zinazoweza kukuzuia kubatizwa.

“Ni Nini Kinachonizuia Kubatizwa?” (Mnara wa Mlinzi, Machi 2019)

Ona jinsi mwanamume fulani alivyoshinda vizuizi vikubwa ili abatizwe.

‘Kwa Nini Unasita Kubatizwa?’ (1:10)

Mwanzoni, mwanamume anayeitwa Ataa alisita kubatizwa. Ona jambo lililomchochea achukue hatua hii muhimu.

Je, Kweli Ninastahili Baraka Hizi Zote? (7:21)