Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 8

Watu Wakubwa Mno Duniani

Watu Wakubwa Mno Duniani

IKIWA mtu angekuwa akikaribia kwako naye ni mrefu sana kama dari ya nyumba yenu, ungeona namna gani? Mtu huyo angekuwa mkubwa mno! Wakati mmoja kulikuwa watu wakubwa mno duniani. Biblia inaonyesha kwamba baba zao ni malaika waliotoka mbinguni. Lakini ilikuwa namna gani?

Kumbuka, Shetani malaika mbaya alikuwa akifanya matata. Hata alikuwa akigeuza malaika wa Mungu wawe wabaya. Mwishowe, malaika wengine walianza kumsikiliza Shetani. Waliacha kufanya kazi waliyopewa na Mungu huko mbinguni. Wakaja duniani na kujivika miili ya kibinadamu. Unajua sababu?

Biblia yasema wana hao wa Mungu waliona wanawake wazuri duniani wakataka kukaa pamoja nao. Kwa hiyo, wakaja duniani kuoa wanawake hao. Biblia inasema hilo lilikuwa kosa, kwa sababu Mungu aliumba malaika wakae mbinguni.

Malaika hao na wake zao walipozaa watoto, watoto hao walikuwa tofauti. Kwanza labda hawakuonekana tofauti sana lakini walizidi kuwa wakubwa na nguvu sana, mpaka wakawa wakubwa mno.

Watu hao walikuwa wabaya. Na kwa vile walivyokuwa wakubwa mno na nguvu sana, waliumiza watu. Walijaribu kumlazimisha kila mtu awe mbaya kama wao.

Henoko alikuwa amekufa, lakini sasa kulikuwako mtu mmoja duniani aliyekuwa mzuri. Mtu huyo ni Nuhu. Sikuzote alifanya mapenzi ya Mungu.

Wakati mmoja Mungu alimwambia Nuhu kwamba wakati wake umefika wa kuharibu watu wote wabaya. Lakini Mungu alitaka kumwokoa Nuhu, jamaa yake na wanyama fulani wengi. Na tuone namna alivyofanya hivyo.