Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 31

Musa na Haruni Wanamwona Farao

Musa na Haruni Wanamwona Farao

MUSA aliporudi Misri, akamwambia Haruni ndugu yake habari ya miujiza yote. Musa na Haruni walipowaonyesha Waisraeli miujiza hiyo, watu wote wakaamini kwamba Yehova alikuwa nao.

Kisha Musa na Haruni wakaenda kumwona Farao. Wakamwambia: ‘Yehova Mungu wa Israeli anasema, “Waruhusu watu wangu waende mwendo wa siku tatu, wakaniabudu jangwani.”’ Lakini Farao akajibu hivi: ‘Mimi simwamini Yehova. Na sitawaruhusu Waisraeli waende.’

Farao alikasirika, kwa sababu watu walitaka wapewe ruhusa ya kwenda kumwabudu Yehova. Basi akawalazimisha wafanye kazi ngumu hata zaidi. Waisraeli wakamlaumu Musa kwa sababu waliteswa vibaya sana, naye Musa akahuzunika. Lakini Yehova akamwambia asisumbuke. ‘Nitamfanya Farao aruhusu watu wangu waende,’ Yehova akasema.

Musa na Haruni wakaenda kumwona Farao tena. Wakati huu walifanya mwujiza. Haruni akaitupa fimbo yake chini, nayo ikawa nyoka mkubwa. Lakini watu wenye akili wa Farao pia wakazitupa fimbo zao chini, nyoka wakatokea. Lakini, ebu tazama! Nyoka wa Haruni anakula wale nyoka wa watu wenye akili. Hata hivyo Farao hataki kuwaruhusu Waisraeli waende.

Basi wakati wa Yehova ukafika wa kuonyesha yeye ana uwezo kuliko Farao. Unajua alivyofanya? Ni kwa kuleta mapigo 10 au taabu kubwa, juu ya Misri.

Baada ya mapigo mengi kidogo, Farao akaagiza Musa aitwe, na kusema: ‘Lizuie pigo, nami nitawapa ruhusa Waisraeli waende.’ Lakini pigo hilo lilipozuiwa, Farao aligeuza nia yake. Hakuwaruhusu watu waende. Lakini, mwishowe, baada ya pigo la 10, Farao alifukuza Waisraeli.

Je! Unajua mapigo hayo 10 yalikuwa gani? Fungua ukurasa unaofuata tuone.