Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 29

Sababu Musa Alikimbia

Sababu Musa Alikimbia

TAZAMA Musa anakimbia Misri. Unaweza kuwaona wanaume hao wanaomfuata? Unajua kwa nini wanataka kumwua Musa? Ebu tuone kama twaweza kujua.

Musa alikua katika nyumba ya Farao, mtawala wa Misri. Akawa mwenye akili na mkuu sana. Musa alijua kwamba yeye si Mmisri, bali wazazi wake ni watumwa Waisraeli.

Siku moja, alipokuwa mwenye miaka 40, Musa alamua kwenda kuona namna watu wake walivyokuwa. Walikuwa wakiteswa sana. Alimwona Mmisri akimpiga mtumwa Mwisraeli. Musa akatazama huku na huku, na alipokosa kumwona mtu yeyote, alimpiga Mmisri mpaka akafa, kisha Musa akaficha mwili wake katika mchanga.

Kesho yake Musa akatoka tena kuwaona watu wake. Alifikiri angeweza kuwasaidia wasiwe watumwa tena. Lakini aliona wanaume Waisraeli wakipigana, basi akamwambia yule aliyekuwa na kosa hivi: ‘Kwa nini unampiga sana ndugu yako?’

Mwanamume huyo akasema: ‘Nani aliyekufanya wewe uwe mtawala na hakimu wetu? Je! utaniua mimi kama ulivyomwua yule Mmisri?’

Musa akaogopa. Alifahamu kwamba watu wamejua alilomtenda yule Mmisri. Hata Farao alisikia habari hizo, naye akawatuma watu wakamwue Musa. Ndiyo sababu Musa alilazimika kukimbia Misri.

Musa alipoondoka Misri, alikwenda mbali kwenye nchi ya Midiani. Ndiko alikokutana na jamaa ya Yethro, akaoa binti yake mmoja jina lake Sipora. Musa akawa mchungaji wa kondoo za Yethro. Alikaa katika nchi hiyo ya Midiani kwa miaka 40. Sasa akawa mwenye umri wa miaka 80. Ndipo siku moja, Musa alipokuwa akichunga kondoo za Yethro, kulitokea ajabu moja iliyogeuza maisha yote ya Musa. Fungua ukurasa mwingine, tuone ajabu hiyo ni nini.