Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 25

Jamaa Inahamia Misri

Jamaa Inahamia Misri

YUSUFU hawezi kujizuia tena. Anawaambia watumishi wake wote waondoke chumbani. Anapokuwa peke yake pamoja na ndugu zake, Yusufu anaanza kulia. Twaweza kuwazia jinsi ndugu zake wanavyoshangaa, kwa sababu hawajui sababu analia. Mwishowe anawaambia hivi: ‘Mimi ni Yusufu. Je! baba yangu angali hai?

Ndugu zake wanashangaa sana hata hawawezi kusema. Wanaogopa. Lakini Yusufu anawaambia hivi: ‘Tafadhali njoni karibu zaidi.’ Wanapokaribia zaidi, anawaambia hivi: ‘Mimi ni ndugu yenu Yusufu, ambaye mliuza Misri.’

Yusufu anaendelea kusema kwa huruma hivi: ‘Msijilaumu kwa sababu mliniuza huku. Ni Mungu aliyenituma nije Misri niokoe maisha za watu. Farao amenifanya niwe mtawala wa nchi yote. Basi sasa fanyeni haraka mrudi kwa baba yangu mkamwambie hivyo. Mwambieni aje kukaa huku.’

Kisha Yusufu anawakumbatia ndugu zake, na kuwabusu wote. Farao anaposikia kwamba ndugu za Yusufu wamekuja anamwambia Yusufu hivi: ‘Na wachukue magari waende kumchukua baba na jamaa zao warudi huku. Nitawapa nchi iliyo bora zaidi katika Misri yote.’

Ndivyo walivyofanya. Hata unaweza kumwona Yusufu akimlaki baba yake anapofika Misri akiwa na jamaa yake yote.

Jamaa ya Yakobo imekuwa kubwa sana. Walipohama kwenda Misri wote walikuwa 70, kutia Yakobo na watoto wake na wajukuu wake. Lakini walikuwako pia wake, na labda watumishi wengi. Wote hao wakahama kwenda Misri. Wakaitwa Waisraeli, kwa sababu Mungu alikuwa amebadili jina la Yakobo kuwa Israeli. Waisraeli wakawa watu wa pekee sana kwa Mungu kama tutakavyoona baadaye.