Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 18

Yakobo Anakwenda Harani

Yakobo Anakwenda Harani

UNAWAJUA wanaume hawa ambao Yakobo anazungumza nao? Akiisha kusafiri siku nyingi, Yakobo alikutana nao penye kisima. Walikuwa wakichunga kondoo zao. Yakobo akauliza: ‘Mnatoka wapi?’

‘Harani,’ wakasema.

‘Mnamjua Labani?’ Yakobo akauliza.

‘Ndiyo,’ wakajibu. ‘Tazama anakuja Raheli binti yake akiwa na kondoo zake.’ Unamwona Raheli (Rakeli) yule anakuja kutoka mbali?

Yakobo alipomwona Raheli akiwa na kondoo za mjomba wake, alikwenda kuondoa jiwe katika kisima ili kondoo wanywe maji. Kisha Yakobo akambusu Raheli na kujijulisha kwake. Raheli alifurahi sana, akaenda nyumbani kumwambia Labani baba yake.

Labani alifurahi sana Yakobo akae naye. Yakobo alipoomba kumwoa Raheli, Labani alifurahi. Lakini, alimwomba Yakobo afanye kazi katika shamba lake miaka 7 ili apewe Raheli. Yakobo alifanya hivyo kwa sababu alimpenda sana Raheli. Lakini ulipofika wakati wa arusi, unajua ilivyokuwa?

Labani alimpa Yakobo Lea binti yake mkubwa badala ya Raheli. Yakobo alipokubali kumfanyia Labani kazi muda wa miaka mingine saba, Labani alimpa Raheli pia awe mke wake. Siku hizo Mungu aliruhusu wanaume wawe na wake wengi. Lakini sasa, kama Biblia inavyoonyesha, imempasa mwanamume awe na mke mmoja tu.