Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 21

Yusufu Anachukiwa na Ndugu Zake

Yusufu Anachukiwa na Ndugu Zake

TAZAMA namna mvulana huyu hana furaha na tumaini. Ni Yusufu. Ndugu zake wamemwuza kwa wanaume hawa wanaokwenda Misri. Huko Yusufu atafanywa mtumwa. Sababu gani ndugu zake walifanya ubaya huo? Walikuwa na wivu.

Yakobo baba yao alimpenda sana Yusufu. Alimpendelea kwa kumshonea vazi refu ambalo ni zuri sana. Ndugu zake wakubwa 10 walipoona namna Yakobo alivyompenda sana Yusufu, walianza kuwa na wivu na kumchukia Yusufu. Lakini kulikuwako sababu nyingine pia ya kumchukia.

Yusufu aliota ndoto mbili. Katika ndoto zote mbili za Yusufu ndugu zake walimpigia magoti. Yusufu alipowasimulia ndugu zake ndoto hizo, chuki yao iliongezeka zaidi.

Basi siku moja ndugu wakubwa wa Yusufu walipokuwa wakichunga kondoo za baba yao, Yakobo alimwomba Yusufu aende kuona kama walikuwa salama. Ndugu za Yusufu walipomwona akija, wengine kati yao walisema: ‘Tumwue!’ Lakini Reubeni ndugu mkubwa wao wote, alisema, ‘Tusifanye hivyo!’ Badala yake walimkamata Yusufu wakamtupa katika shimo kavu.

Karibu na wakati huo wanaume fulani Waishmaeli wakaja. Yuda akawaambia ndugu zake hivi: ‘Na tumwuze kwa Waishmaeli hawa.’ Ndivyo wanavyofanya. Wanamwuza Yusufu kwa vipande 20 vya fedha. Lo! walikuwa bila huruma kama nini!

Ndugu zake watamwambia baba yao nini? Wanamwua mbuzi na kuchovya vazi zuri la Yusufu katika damu ya mbuzi huyo. Kisha wanampelekea Yakobo baba yao vazi hilo na kusema: ‘Tumeona hili. Ebu litazame, kama ni vazi la Yusufu.’

Yakobo anaona hivyo. ‘Mnyama mkali amemwua Yusufu,’ analia. Hivyo ndivyo ndugu za Yusufu wanavyotaka baba yao afikiri. Yakobo anahuzunika sana sana. Anaomboleza siku nyingi. Lakini Yusufu hakufa. Tuone yanayompata kule alikopelekwa.