Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 34

Aina Mpya ya Chakula

Aina Mpya ya Chakula

UNAJUA watu wanaokota nini chini? Ni cheupe, na chembamba na chenye kupasuka vipande vyembamba. Ni chakula.

Umekuwa karibu mwezi mmoja tu tangu Waisraeli waondoke Misri. Wamo jangwani. Humo chakula kidogo kinamea, watu wanalia, wakisema: ‘Afadhali Yehova angetuua huko Misri. Tulikula huko kila chakula tulichotaka.’

Basi Yehova asema: ‘Nitatelemsha chakula kutoka angani.’ Ndivyo Yehova anafanya. Kesho yake Waisraeli wanapoona chakula hicho cheupe kilichoanguka, wanaulizana hivi: ‘Ni nini hiki?’

Musa anajibu: ‘Ndicho chakula ambacho Yehova amewapa mle.’ Watu wanakiita MANA. Utamu wake ni kama keki (mkate) nyembamba zenye asali.

‘Kila mtu aokote anachoweza kula,’ Musa anawaambia watu. Basi kila asubuhi wanaokota hivyo. Jua linapokuwa kali, ile mana iliyoachwa chini inayeyuka.

Pia Musa anasema: ‘Mtu asiweke mana ikae mpaka kesho.’ Lakini watu wengine hawasikii. Unajua inavyokuwa? Kesho yake ile mana waliyoweka inajaa wadudu, inaanza kunuka vibaya!

Walakini kuna siku moja katika juma ambayo Yehova anawaambia watu wakusanye mana nyingi mara mbili. Siku hiyo ni ya sita. Yehova anawaambia waweke akiba ya kesho, kwa sababu hataangusha mana yoyote siku ya saba. Wanapoweka akiba ya siku ya saba, haijai wadudu wala kunuka! Huo ni mwujiza mwingine.

Miaka yote ambayo Waisraeli walikuwa jangwani Yehova aliwalisha mana.