Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 39

Fimbo ya Haruni Inamea Maua

Fimbo ya Haruni Inamea Maua

YATAZAME maua na lozi hizo zilizoiva zikimea katika fimbo hiyo. Hiyo ni fimbo ya Haruni. Maua na matunda hayo yalimea katika fimbo ya Haruni usiku mmoja tu! Ebu tuone sababu yake.

Waisraeli wamekuwa wakitanga-tanga jangwani kwa muda fulani sasa. Wengine kati ya watu hawataki Musa awe kiongozi, wala Haruni kuwa kuhani mkuu. Kora anafikiri hivyo, pia Dathani, Abiramu na viongozi wa watu 250. Wote hao wanakuja kumwambia Musa hivi: ‘Kwa nini wewe unajiweka juu ya wengine wetu?’

Musa anamwambia Kora na wafuasi wake hivi: ‘Kesho asubuhi mchukue makoleo ya moto mweke uvumba ndani yake. Ndipo mje kwenye hema ya Yehova. Tutaona ni nani ambaye Yehova atachagua.’

Kesho yake Kora na wafuasi wake 250 wanafika kwenye hema. Wengine wengi wanafuata ili wawaunge mkono wanaume hao. Yehova anakasirika sana. ‘Ondokeni kwenye hema za watu hao wabaya,’ Musa anasema. ‘Msishike mali yao.’ Watu wanasikiliza, na kuondoka kwenye hema za Kora, Dathani na Abiramu.

Kisha Musa anasema hivi: ‘Kwa hili mtajua ni nani ambaye Yehova amechagua. Ardhi itafunguka na kuwameza watu hawa wabaya.’

Mara Musa anapomaliza kusema, ardhi inafunguka. Hema ya Kora na mali yake na Dathani na Abiramu na wale walio pamoja nao wanazama, nayo ardhi inawafunika. Watu wanaposikia kilio cha hao wanaotumbukia katika ardhi, wanapiga kelele hivi: ‘Kimbieni! Ardhi isitumeze sisi pia!’

Kora na wafuasi wake 250 bado wako karibu na hema. Basi Yehova anapeleka moto, na wote wanateketezwa. Kisha Yehova anamwambia Eleazari mwana wa Haruni achukue makoleo ya moto ya watu hao waliokufa ayafanye yawe kifuniko chembamba cha madhabahu.

Yehova anataka wafahamu sana kwamba Haruni na wanawe ndio amechagua wawe makuhani. Basi anamwambia Musa hivi: ‘Mwambie kiongozi wa kila kabila la Israeli alete fimbo yake. Kisha weka kila moja ya fimbo hizo katika hema mbele ya sanduku la agano. Ile fimbo ya mtu niliyemchagua awe kuhani itamea maua.’

Musa anapotazama kesho yake, lo! fimbo ya Haruni imemea maua hayo na lozi zilizoiva! Basi unaona sasa kwa nini Yehova alifanya fimbo ya Haruni imee maua?