Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 49

Jua Linasimama Tu

Jua Linasimama Tu

MTAZAME Yoshua. Anasema: ‘Jua, simama!’ Jua linasimama. Linakaa siku nzima katikati ya anga. Yehova anafanya hivyo! Lakini ebu tuone kwa nini Yoshua anataka jua liendelee kung’aa.

Wale wafalme wabaya watano katika nchi ya Kanaani wanapoanza kupigana na Wagibeoni, hao Wagibeoni wanamtuma mtu aende kumwomba Yoshua msaada. ‘Njoo kwetu upesi!’ asema. ‘Utuokoe! Wafalme wote wa vilimani wamekuja kupigana na watumishi wako.’

Mara hiyo Yoshua na wanajeshi wake wote wanakwenda. Wanasafiri usiku kucha. Wanapofika Gideoni, wale askari wa wafalme watano wanaogopa na kuanza kukimbia. Ndipo Yehova anaangusha mawe makubwa ya mvua kutoka angani. Askari wengi wanakufa kwa mvua ya mawe kuliko wanaouawa na wanajeshi wa Yoshua.

Yoshua anaona kwamba karibu jua litatua. Kutakuwa usiku, na askari wengi wa wafalme watano wabaya watakimbia. Ndiyo sababu Yoshua anamwomba Yehova na kusema: ‘Jua, simama!’ Jua linapoendelea kung’aa, Waisraeli wanashinda vita.

Kuna wafalme wabaya wengi zaidi katika Kanaani wanaochukia watu wa Mungu. Inamchukua Yoshua na jeshi lake karibu miaka sita kushinda wafalme 31 katika nchi hiyo. Kisha, Yoshua anahakikisha kwamba nchi ya Kanaani imegawanywa ili makabila yanayohitaji eneo, yapewe.

Kunapita miaka mingi, mwishowe Yoshua anakufa akiwa mwenye miaka 110. Wakati yeye na rafiki zake bado hai, watu wanamtii Yehova. Lakini watu hao wema wanapokufa, watu wanaanza kutenda mabaya na kutaabika. Huu ndio wakati wanapohitaji msaada wa Mungu.