Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 40

Musa Anaupiga Mwamba

Musa Anaupiga Mwamba

MWAKA baada ya mwaka unapita—miaka 10, miaka 20, miaka 30, miaka 39! Waisraeli wangali jangwani. Lakini miaka hiyo yote Yehova anawaangalia watu wake. Anawalisha mana. Anawaongoza mchana kwa nguzo ya wingu, na usiku kwa nguzo ya moto. Na wakati wa miaka yote hiyo mavazi yao hayamaliziki na miguu haipati vidonda.

Sasa ndio mwezi wa kwanza wa mwaka wa 40 tangu waondoke Misri. Tena Waisraeli wanapiga kambi katika Kadeshi. Hapo ndipo walipokuwa wakati wapelelezi 12 walipotumwa kwenda kwenye nchi ya Kanaani karibu miaka 40 iliyopita. Miriamu dada yake Musa anakufa katika Kadeshi. Na kama zamani, matata yanatokea hapa.

Watu hawawezi kupata maji. Hivyo wanamlilia Musa hivi: ‘Afadhali tungekufa. Kwa nini ukatutoa Misri kuja mahali hapa pabaya pasipomea kitu? Hakuna nafaka, hakuna tini, hakuna zabibu, hakuna komamanga. Wala hakuna maji ya kunywa.’

Musa na Haruni wanapokwenda kwenye hema wakasali, Yehova anamwambia Musa hivi: ‘Wakusanye watu. Kisha mbele yao wote useme na mwamba ule. Maji mengi yatatoka watu na wanyama wao wote wanywe.’ Basi Musa anakusanya watu, na kusema: ‘Sikilizeni, ninyi msiomtumaini Mungu! Je! Haruni na mimi tuwatolee maji katika mwamba huu?’ Kisha Musa anaupiga mwamba huo mara mbili kwa fimbo, maji mengi yatiririka katika mwamba huo. Kuna maji mengi ya kunywa watu wote na wanyama.

Lakini Yehova anawakasirikia Musa na Haruni. Unajua kwa nini? Kwa sababu Musa na Haruni walisema kwamba wao watatoa maji katika mwamba. Lakini Yehova ndiye aliyetoa. Na kwa vile Musa na Haruni hawakusema kweli hiyo, Yehova anasema kwamba atawaadhibu. ‘Hamtawaingiza watu wangu Kanaani,’ anasema.

Upesi Waisraeli wanaondoka Kadeshi. Baada ya kitambo kidogo wanafika kwenye Mlima Hori. Huko ndiko Haruni alikufa juu ya kilele cha mlima. Anakufa akiwa mwenye miaka 123. Waisraeli wanahuzunika sana, na watu wote wanamlilia Haruni muda wa siku 30. E·le·aʹzari mwanawe anakuwa kuhani mkuu wa pili wa taifa la Israeli.