Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 51

Ruthu na Naomi

Ruthu na Naomi

UTAONA kitabu kinachoitwa Ruthu (Ruta) katika Biblia. Ni hadithi juu ya jamaa iliyokaa wakati Waisraeli walipokuwa na waamuzi. Ruthu ni mwanamke kijana kutoka nchi ya Moabu; si wa taifa la Mungu la Israeli. Lakini Ruthu anapopata habari za Mungu wa kweli Yehova, anampenda sana sana. Naomi ni mwanamke mzee aliyemsaidia Ruthu amjue Yehova.

Naomi ni Mwisraeli. Yeye na mumewe na wana wawili walihama kwenda Moabu ilipotokea njaa katika Israeli. Ndipo siku moja mume wa Naomi akafa. Baadaye wana wa Naomi wakaoa wasichana wawili Wamoabi, Ruthu na Orʹpa. Lakini baada ya miaka kama 10 hivi, wana wawili wa Naomi wakafa. Lo! Naomi alihuzunika sana, na wasichana wawili pia! Sasa Naomi atafanya nini?

Siku moja Naomi anaamua kurudi kwa watu wake. Ruthu na Orʹpa wanataka kukaa naye, wanafuata. Lakini wakiisha kusafiri kidogo, Naomi anageuka na kuwaambia wasichana hao wawili hivi: ‘Rudini kwenu mkakae na mama zenu.’

Naomi anawabusu wasichana hao, akiwaambia kwa heri. Kwa hiyo wanaanza kulia, kwa sababu wanampenda Naomi sana sana. Wanasema: ‘Sivyo! Sisi tutakwenda nawe kwa watu wako.’ Lakini Naomi anajibu hivi: ‘Ni lazima mrudi, binti zangu. Itakuwa bora ninyi kukaa kwenu.’ Orʹpa anaanza kurudi kwao. Lakini Ruthu akataa kurudi.

Naomi anageuka na kumwambia: ‘Orʹpa amekwenda. Wewe pia nenda kwenu.’ Lakini Ruthu ajibu: ‘Usiniambie nikuache! Acha niende nawe. Mahali uendapo nitakwenda, mahali unapokaa nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako, Mungu wangu. Mahali ambapo utakufa nitakufa, na kuzikwa hapo.’ Ruthu anaposema hivyo, Naomi anaacha.

Mwishowe wanawake hao wawili wanafika Israeli. Wanakaa huko. Mara hiyo Ruthu anaanza kufanya kazi mashambani, maana ni wakati wa kuvuna shayiri. Mwanamume mmoja jina lake Boazi anamruhusu akusanye shayiri katika mashamba yake. Unamjua mama ya Boazi? Ni Rahabu wa Yeriko.

Siku moja Boazi anamwambia Ruthu hivi: ‘Nimesikia habari zako zote, jinsi umehurumia Naomi. Najua ulivyoacha baba na mama yako na nchi yako ukaja kukaa na watu ambao hukujua zamani. Yehova akubariki!’

Ruthu anajibu hivi: ‘Unanionyesha fadhili nyingi, bwana. Umenifariji kwa maneno yako mazuri.’ Boazi anampenda Ruthu sana sana, na muda si muda wanaoana. Jambo hili lamfurahisha Naomi kama nini! Lakini Naomi anafurahi hata zaidi wakati Ruthu na Boazi wanapopata mwana wao wa kwanza, jina lake Obedi. Baadaye Obedi anakuwa babu ya Daudi, ambaye tutajua habari zake nyingi baadaye.

Kitabu cha Biblia cha Ruthu(Ruta).