Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 48

Wagibeoni Wenye Hekima

Wagibeoni Wenye Hekima

SASA miji mingi katika Kanaani inajitayarisha kupigana na Israeli. Wanadhani wanaweza kushinda. Lakini watu wa mji jirani wa Gibeoni hawadhani hivyo. Wanaamini Mungu anawasaidia Waisraeli, nao hawataki kupigana na Mungu. Basi unajua Wagibeoni hao wanafanya nini?

Wanajifanya kama wanakaa mbali sana. Basi wengine kati yao wanavaa nguo zilizopasuka-pasuka na viatu vilivyokwisha. Wanapakia punda zao mifuko ya zamani, na kuchukua mikate iliyokauka. Kisha wanamwendea Yoshua wakimwambia: ‘Tumetoka mbali sana, kwa kuwa tulisikia habari za Mungu wenu mkuu, Yehova. Tulisikia yote aliyowafanyia huko Misri. Basi viongozi wetu walituambia tutayarishe chakula cha safari tuje tukuambie: “Sisi ni watumishi wako. Utupe ahadi ya kwamba hutapigana na sisi.” Tazama nguo zetu zimekwisha kwa sababu ya safari ndefu na mkate nao umekauka.’

Yoshua na viongozi wengine wanawaamini Wagibeoni hao. Basi wanaahidi wasipigane nao. Lakini baada ya siku tatu wanajua kwamba kumbe Wagibeoni hao wanakaa karibu sana.

‘Mbona mlituambia mmetoka mbali sana?’ Yoshua anawauliza.

Wagibeoni wanajibu hivi: ‘Tulisema hivyo kwa sababu tuliambiwa kwamba Mungu wenu Yehova alikuwa ameahidi kuwapa ninyi nchi yote hii ya Kanaani. Tuliogopa kwamba labda mtatuua.’ Lakini Waisraeli wanafuata ahadi yao, wasiwaue Wagibeoni. Wanawafanya kuwa watumishi wao.

Mfalme wa Yerusalemu anakasirika kwa sababu Wagibeoni wamefanya amani na Israeli. Basi anawaambia wafalme wengine wanne hivi: ‘Njoni mnisaidie kupiga Gibeoni.’ Wafalme hao watano wanafanya hivyo. Je! Wagibeoni walionyesha akili kwa kufanya amani na Israeli? Tutaona.