Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 38

Wapelelezi 12

Wapelelezi 12

TAZAMA matunda ambayo wanaume hawa wanabeba. Tazama kichala kile cha zabibu kilivyo kikubwa. Kinataka wanaume wawili wakibebe kwa mti. Zitazame tini na yale makomamanga. Matunda hayo mazuri yalitoka wapi? Nchi ya Kanaani. Kumbuka, wakati mmoja Ibrahimu, Isaka na Yakobo walikaa Kanaani. Lakini kwa sababu kulikuwako njaa kuu, Yakobo na jamaa yake, walihama wakaenda Misri. Sasa, miaka kama 216 baadaye, Musa anawarudisha Waisraeli Kanaani. Wamefika mahali panapoitwa Kadeshi huko jangwani.

Watu wabaya wanakaa Kanaani. Basi Musa anawatuma wapelelezi 12, akiwaambia: ‘Nendeni mkaone ni watu wangapi wanaokaa huko, na wana nguvu gani. Mjue kama udongo unafaa mimea. Mhakikishe kurudisha matunda fulani.’

Wapelelezi hao wanaporudi Kadeshi, wanamwambia Musa hivi: ‘Ni nchi nzuri kweli kweli.’ Na kama ushuhuda wa hayo, wanamwonyesha Musa matunda fulani. Lakini wapelelezi 10 wanasema hivi: ‘Watu wanaokaa huko ni wakubwa na wenye nguvu sana. Tutauawa tukijaribu kuichukua nchi hiyo.’

Waisraeli wanaogopa kwa kusikia hayo. ‘Afadhali tungefia Misri au hata humu jangwani,’ wanasema. ‘Tutauawa vitani, wake zetu na watoto watatekwa nyara. Na tuchague kiongozi mpya mahali pa Musa, turudi Misri!’

Lakini wapelelezi wawili wanamtumaini Yehova, wanajaribu kuwatuliza watu. Ni Yoshua na Kalebu. Wanasema: ‘Msiogope. Yehova yuko pamoja na sisi. Itakuwa rahisi kuichukua nchi hiyo.’ Lakini watu hawasikii. Hata wanataka kuwaua Yoshua na Kalebu. Hilo lamkasirisha Yehova sana, anamwambia Musa hivi: ‘Hakuna yeyote kati ya watu hao kuanzia wale wenye miaka 20 na zaidi watakaoingia Kanaani. Wamekwisha kuiona miujiza niliyofanya huko Misri na jangwani, lakini bado hawanitumaini. Basi watatanga-tanga jangwani muda wa miaka 40 mpaka mtu wa mwisho afe. Yoshua (Yosua) na Kalebu peke yao wataingia Kanaani.’