Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 67

Yehoshafati Anamtumaini Yehova

Yehoshafati Anamtumaini Yehova

UNAJUA wanaume hawa ni nani na wanalofanya? Wanakwenda vitani, na wanaume walio mbele wanaimba. Lakini labda utauliza: ‘Kwa nini waimbaji hawana panga na mikuki ya vita? Ebu tuone.

Yehoshafati ni mfalme wa ufalme wa makabila mawili ya Israeli. Anakaa wakati mmoja na Mfalme Ahabu na Yezebeli wa ufalme wa makabila 10. Lakini Yehoshafati ni mfalme mzuri, na Asa baba yake alikuwa mfalme mzuri pia. Basi watu wa Ufalme wa makabila mawili wanafurahia maisha mema kwa miaka mingi.

Lakini sasa kunatokea jambo la kuogopesha watu. Wajumbe wanamjulisha Yehoshafati hivi: ‘Jeshi kubwa kutoka nchi za Moabu, Amoni na Mlima Seiri linakuja kukushambulia wewe.’ Waisraeli wengi wanakusanyika Yerusalemu wamwombe Yehova msaada. Wanakwenda katika hekalu, na huko Yehoshafati anasali hivi: ‘Ee Yehova Mungu wetu, hatujui la kufanya. Hatuna msaada juu ya jeshi hili kubwa. Twakutumaini utusaidie.’

Yehova anasikiliza, anamtuma mtumishi wake awaambie watu hivi: ‘Vita si yenu, bali ya Mungu. Ninyi hamtapigana. Tazameni tu, mwone jinsi Yehova atakavyowaokoa ninyi.’

Basi kesho yake Yehoshafati anawaambia watu hivi: ‘Mtumainini Yehova!’ Kisha anaweka waimbaji mbele ya askari zake, wakimsifu Yehova wanapotembea. Unajua linalotokea wanapokaribia vita? Yehova anafanya askari maadui wapigane wao kwa wao. Na Waisraeli wanapofika, kila askari adui amekufa!

Je! Yehoshafati hakuwa na akili kwa kumtumaini Yehova? Sisi pia tukimtumaini Yeye, tutakuwa na akili.